2017-05-04 12:04:00

Wanajeshi 40 wa Kikosi cha ulinzi na usalama Vatican kula kiapo!


Wanajeshi  40 wa Kikosi cha Ulinzi na Usalama cha Vatican, maarufu kama “Swiss Guards”, Jumamosi jioni tarehe 6 Mei 2017 baada ya kuhitimu mafunzo yao katika mfumo mpya, watakula kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro kitakachopokelewa na Monsinyo Paolo Borgia, mwakilishi wa Katibu mkuu wa Vatican. Viongozi wakuu kiserikali na kikanisa watahudhuria. Kardinali Gerhard Muller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa ndiye atakayeongoza Ibada ya Misa Takatifu itakayoadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.

Ijumaa jioni tarehe 5 Mei 2017, Kikosi cha ulinzi na usalama cha Vatican, kitaadhimisha mkesha wa Siku kuu hii kwa Masifu ya jioni yatakayoadhimishwa kwenye Kanisa la “Santa Maria della Pietà” lililoko mjini Roma na baadaye Uwanja wa Mashuhuda wa Imani wa Roma, kutafuatia sherehe ya kuweka shada la maua kwenye mnara wa kumbu kumbu ya Askari 147 kutoka Uswiss waliofariki dunia kunako mwaka 1527 wakati wa kumlinda Khalifa wa Mtakatifu Petro. Tangu wakati huo, hawa wamekuwa ni walinzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro mjini Vatican. Ni Askari wakakamavu, nadhifu, wapole na waungwana wanaotekeleza dhamana na wajibu wao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji mkubwa kwa ajili ya Papa, waamini na mahujaji wanaofika mjini Vatican kwa shughuli mbali mbali!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.