2018-06-19 14:23:00

Njaa kubwa inakumba watu wa Afrika hasa katika kanda yote ya Sahel !


Hali ya chakula eneo la Sahel inasikitisha kwa mujibi wa ombi lilotolewa na mjini New York Marekani na mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu (OCHA), Bwana Mark Lowcock wakati akitoa maelezo kuhusu hali ya kibinadamu ilivyo kwa sasa katika eneo hilo. Nchi hizo sita kwenye eneo hilo ni Burkina Faso, Chad, Mali, Mauritania, Niger na Senegal ambapo amesema zinakabiliwa na uhaba wa chakula. Amethibitisha kuwa ni takriban watu milioni 6 wanapambana vikali kuweza kutimiza mahitaji yao ya kila siku na kuongeza kuwa utapiamlo uliokithiri unatishia maisha ya watoto milioni 1.6, hiyo ikiwa ni kiwango cha asilimia 50 tangu mwaka jana na hakijawahi kushuhudiwa  tangu mgogoro wa 2012.

Bwana Lowcock amesema kuwa ingawa anatiwa moyo na juhudi za washirikawao za kuzidisha operesheni kutokana na ishara za mwanzo, bado hali inaendelea kuzorota  hivyo kuna umuhimu wa msaada zaidi kutoka kwa wahisani. Mgogoro wa sasa wa chakula ulichochewa na  ukosefu wa mvua  mwaka 2017 na hivyo kusababisha uhaba wa maji, mazao na chakula cha mifugo nakufa kwa mifugo mingi.

Ameongeza kuwa hali hii  iliwafanya wafugaji kuhama mapema kuliko  kawaida jambo ambalo limetokea  baada ya kipindi cha miaka 30. Kuhusu chakula, mkuu huyo wa OCHA amesema kuwa uhaba wa chakula umesababisha familia nyingi kupunguza  kiwango cha  mlo wa kila siku huku wengine wamewaondoa watoto wao mashuleni na wameachana na hudumamuhimu za matibabu, wakifunga mkaja kuweza kuhifadhi pesa za kununulia chakula. OCHA inasisitiza, idadi ya  watu wanaohitaji chakula pamoja na msaada mwingine  inaweza kuongezeka hadi milioni 6.5 mwezi Septemba mwaka huu.

Ombi la Umoja wa Mataifa la kusaidia nchi za Sahel limefadhiliwa na asilimia 26 tu  ambapo, Lowcok asema, wiki iliyopita alitoa  dola milioni 30 kutoka mfuko wa masuala ya dharura,  ili zisaidie katika eneo hilo, na hivyo kuomba msaada zaidi kutoka kwa wahisani akisema kuwa bado wanaweza kuepusha mabaya zaidi. Hata hivyo pia naye Dominik Stillhart, Mkuu wa Tume ya kimataifa ya Msalaba Mwekendu wakati wa ziara yake hivi katibuni nchini Somalia mahali ambapo mwanzo watu 250,000 walikufa kutokana na njaa, amesema“tunatoa wito kwa ajili ya jumuiya ya kimataifa ili watu wasiendelee kufa kwa ajili ya ukosefu wa chakula.

Na Sr Angela Rwezaula
 Vatican News








All the contents on this site are copyrighted ©.