2018-06-07 14:06:00

Maaskofu Ethiopia: Mungu ametoa jukumu kwa wafuasi kulinda watoto !


Mwakilishi wa Kitume huko Jimma Bonga nchini Ethiopia, Askofu Mkuu Markos Gebremedhin, (CM) wakati wa uzinduzi rasmi wa Siasa ya utetezi na ulinzi wa watoto kwa upande wa Kanisa Katoliki Ethiopia na ikiwa ndiyo mwanzo wa huduma ya wahudumu waliopewa shughuli hiyo, amesema, wafuasi wote wa Kristo wamepewa jukumu la kulinda na kusaidia makuzi ya watoto.  Katika hotuba yake, Askofu Gebremedhin ameweka wazi kueleza hata tabia mbaya na manyanyaso wanayopata watoto wadogo duniani, wakiwemo hata nchiniEthiopia. Askofu amesema ukosefu wa utekelezwaji na unyanyasaji wa watoto kama vile: manyanyaso kimwili, adhabu kimwili, kazi za utoto, biashara ya watoto, nyanyaso za kijinsia na kihisia,kisaikolojia, ukosefu wa utambuzi katika familia juu ya haki za watoto wao, kama vile hata haki za kukua, elimu na afya, ndiyo mambo msingi yanayopelekea  athari kubwa za kisaikolojia, na hata kuwafanya vijana kukua kwa shida na wakati mwingine kusabibisha kujiua wenyewe.
 
Ili kupambana na janga hili, Askofu amethibitisha kwamba, Baraza la Maaskofu wa Ethiopia wamekabidhi Sekretarieti Kuu ya Baraza la Maaskofu Ethiopia (ECS) kutengenza Waraka juu ya utetezi na ulinzi wa watoto ili kuweza kuutumia  kama chombo madhubuti, kiongozi katika kuhamasisha mapadre, watawa, walimu, makatekista na viongozi wa vijana na zaidi ambao wanasoma katika taasisi katoliki. Aidha askofu Gebremedhin amethibitisha, Kanisa Katoliki la Ethiopia, kwa sasa wanajikita kuhakikisha usalama, ustawi na hadhi ya watoto, katika kutafuta mahitaji msingi na lazima na utoaji wa elimu iliyo bora. Kwa maana hiyo wametoa ofisi maalum kwa ajili hiyo, katika Barazal a maaskofu wa Ethiopia, ili kutetea watoto na watu wazima walioathirika. Wakati huhuo pia wameunda Kamati ya uendeshaji kwa ngazi ya kitaifa na wawakilishi kutoka kila sekta ya sheria ya Kanisa.

Wakati wa kuwakilisha waraka huo kuhusu Siasa kwa ajili ya kutetea na kulinda watoto wa Kanisa Katoliki, askofu ameelezea jinsi gani kama maaskofu katoliki wa Ethiopia wamefikiria kuhusika ili kuweka kipaumbele cha matatizo na kuongeza juhudi za Kanisa la ulimwenguni kuelekea suala la kulinda watoto wadogo ili waweze kuishi mahali a usalama, watoto na watu wazima walioathirka na ampo inahitaji juhudi za watu wote. Katika kuhusiana na suala la utetezi na ulinzi wa watoto, kuna hata suala linalohusu utelekezaji wa watoto. Kutelekezwa maana yake wazazi au wakubwa kutomtimizia mtoto mahitaji muhimu kama vile makazi mazuri, chakula, elimu, nguo au matibabu. Pia kutowasimamia watoto na kuwaacha wapweke kwa muda mrefu. Unyanyasaji wa kimwili maana yake mzazi au mlezi kumuumiza mtoto kwa kumchapa, kumsukuma sukuma. Unyanyasaji wa kiakili maana yake kuharibu hisia ya mtoto. Hii hutokea pale unapo waambia hawapendwi, kuwachukia mda wote, kuwatishia kuwapiga. Pia kumruhusu mtoto kutazama manyanyaso anayofanyiwa mtu katika familia, kama vile mama yao.

Kwahiyo unyanyasaji wa akili ni mbaya kwa watoto na huwafanya wajihisi ni wanyonge. Unyanyasaji wa kijinsia ni pale mtu anapomuingiza mtoto kwenye maswala ya kingono. Watoto huwa wanalazimishwa na kutishiwa ili wafanye kazi hii. Unyanyasaji wa kijinsia hupelekea dosari kwa watoto katika maisha yao. Ndoa za utotoni na ndoa za kulazimishwa Kuoa au kuolewa chini ya miaka 18 ni kosa kisheria. Kuna baadhi ya matatizo huruhusu mtoto wa miaka 16 au 17 kuoa au kolewa lakini awe na kibali cha mahakama. Pia ni kosa kumlazimisha mtu wa umri wowote kuoa au kuolewa. Ndoa za kulazimisha humfanya muhusika kutokuwa huru kwa sababu walimfokea, walimtisha au walimchochea.

Mbali na masuala ya Kanisa la Ethiopia kujikita kwa sasa katika harakati za kulinda na kutetea watoto, taarifa nyingine inasema kuwa, Ethiopia imeahidi kutekeleza makubaliano ya amani na Eritrea. Nchi hiyo imekubali bila masharti yoyote kutekeleza makubaliano ya amani ya Algiers yaliyoipa jirani yake Eritrea maeneo yaliyokuwa wakizozania tokea vita vilivyodumu miaka miwili vya 1998. Chama tawala kimesema Ethiopia imeamua kutekeleza makubaliano hayo ya amani ya Algiers yanayohusu mpaka wa Eritrea na Ethiopia bila ya masharti yoyote, kulingana na kituo cha televisheni ya taifa Fana. Taarifa hilo limesema litafanya kazi kwa bidii kuyatekeleza makubaliano hayo.

Tangazo hilo linamaanisha Ethiopia inakubali uamuzi wa ugawaji wa mipaka wa makubaliano hayo ya Algiers wa mwaka 2000 ulioipa Eritrea haki ya kumiliki maeneo waliokuwa wakiyazozania ikiwa ni pamoja na mji wa Badme. Lakini hadi hivi sasa Ethiopia bado imeweka wanajeshi wake katika eneo hilo. Lakini inakumbukwa kuwa maelfu ya watu waliuawa wakati wa vita vya miaka miwili vilivyoanza mwaka 1998. Aidha, mapema hii tarehe 5 Jini 2018, wabunge wa Ethiopia walipiga kura ya kuunga mkono kuondoa hali ya hatari iliyokuwa imetangazwa nchini humo, japokuwa Wabunge wanane walikataa kupiga kura kabisa.

Hali hiyo ya hatari ya hivi karibuni iliwekwa katikati ya mwezi Februari baada ya kutokea maandamano makubwa dhidi ya serikali katika maeneo ya Oromia na Amhara. Hatua za kukubali makubaliano hayo ya amani na Eritrea na kuondosha hali ya hatari ni mabadiliko muhimu ya hivi karibuni chini ya uongozi wa waziri mkuu mpya Abiy Ahmed, ambaye amezungumzia wazi juu ya haja ya kuleta mageuzi nchini humo. Hali kadhalika, waziri mkuu huyo amewaachilia huru wafungwa wa kisiasa na kuanzisha mazungumzo na makundi ya upinzani tokea kuingia madarakani mwezi Aprili. Mbali na hayo, Ethiopia pia tarehe 5 Juni 2018  imesema kuwa, shirika lake la simu linaloendeshwa na serikali pamoja na shirika la usafiri wa ndege yatakaribisha uwekezaji wa sekta binafsi.

Ni sera muhimu ambayo inatarajiwa kupunguza udhibiti wa serikali katika uchumi wa nchi. Taifa hilo la Afrika Mashariki lenye idadi ya watu wapatao milioni 100, linaongoza barani Afrika kwa kuwa na uchumi unaodhibitiwa na serikali. Muungano tawala wa EPRDF, ambao umekuwa madarakani tokea 1991, kwa muda mrefu umekuwa ukiunga mkono uchumi unaodhibitiwa na serikali. Lakini muungano huo tarehe 5 Juni 2018, umesema  kwamba Ethiopia inahitaji mageuzi ya kiuchumi ili kupata ukuaji wa haraka na kuimarisha mauzo yake ya nje ya nchi. Milango pia itafunguliwa kwa wawekezaji binafsi katika mashirika mengine yaliyo kwenye mikono ya serikali kama vile shirika la reli, kiwanda cha sukari, mahoteli na viwanda mbalimbali vya uzalishaji. Abiy anatajwa kuwa chini ya shinikizo la kutimiza matarajio ya umma. Katika miezi miwili iliyopita amekuwa akitembelea maeneo mbalimbali ya Ethiopia akiahidi kushughulikia malalamiko ya raia kuhusu ukosefu wa haki za kisiasa na kiraia unaoshuhudiwa nchini humo.

Na Sr Angela Rwezaula 
Vatican News








All the contents on this site are copyrighted ©.