2018-05-12 17:35:00

Wadau wa tasnia ya habari kuzeni: nidhamu, uadilifu, weledi na taaluma


Njia ya mawasiliano ya jamii zimekuwa ni gumzo la mwaka kila pembe ya dunia, lakini ka bahati mbaya, ni watu wachache sana ambao wako tayari kusimama na kutafakari kwa kina na mapana dhamana na umuhimu wa mawasiliano yanayosimikwa katika weledi. Leo hii, kuna utitili wa vyombo vya mawasiliano kuanzia kwenye mitandao ya kijamii, wavuti na tovuti, lakini kiboko yao ni tovuti inayowapatia nafasi waandishi wa habari kutekeleza dhamana na wajibu wao kwa kuzingatia nidhamu, taaluma, uadilifu pamoja na uwajibikaji, ili kukuza uandishi wa habari wenye ubora.

Hii ni sehemu ya ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko alioliandikia Gazeti la “La Stampa” linalochapishwa kila siku nchini Italia. Pamoja na mambo mengine, Baba Mtakatifu amekazia uandishi wa habari unaozingatia sheria kanuni na maadili ya kazi, kwa kujitahidi daima kutoa habari njema inayoweza “kuona madini ya almasi hata katika makinikia”; habari ambazo zimepyaishwa ili kuleta matumaini, kwa watu waliokata tamaa, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa wale wasiokuwa na sauti, watu wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, hawa ndio wale watu wasiokuwa na nguvu ya kiuchumi!

Baba Mtakatifu anakaza kusema, habari inapaswa kusimulia hali changamani zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu mamboleo, bila kutumbukia katika kishawishi cha habari za kupiga propaganda! Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko  kwamba, gazeti hili ambalo linaboresha mwonekano wake wa nje pamoja na “Vatican Insider” sehemu inayojishughulisha zaidi na masuala ya kidini na maisha ya kiroho, yasaidie kuwapatia wasomaji wake habari njema na nzuri!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!

 








All the contents on this site are copyrighted ©.