2018-02-13 07:41:00

Jumatano ya Majivu ni mwanzo wa Kipindi cha Kwaresima!


Jumatano ya Majivu ni mwanzo wa Kipindi cha Kwaresima ambapo waamini wanapakwa majivu yanayowakumbusha kwamba, wao ni mavumbi na mavumbini watarudi, changamoto kubwa ni kupyaisha maisha ya kiroho kwa njia ya: Sala na sadaka. Ni wakati wa kujichimbia katika tafakari ya Neno la Mungu pamoja na matendo ya huruma: kiroho na kimwili. Hii ni  njia muafaka ya kujiandaa kikamilifu ili kukutana na Kristo Mfufuka aliye hai katika Neno lake, Sakramenti za Kanisa na kwa njia ya huduma makini kwa jirani sehemu muhimu sana ya mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu hapa duniani.

Waamini wajitahidi kufunga ili kuratibu vilema vyao na kwa kuepuka dhambi za mazoea na hatimaye, wamwombe na kujiaminisha kwa Roho Mtakatifu ili aweze kuwakirimia toba na wongofu wa ndani unaowaletea upya wa maisha, tayari kutembea katika mwanga wa Kristo Mfufuka baada ya siku 40 za maisha ya kiroho jangwani! Kipindi cha Kwaresima yaani Siku 40 ni safari ya maisha ya kiroho inayojikita katika: imani, matumaini na mapendo.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Kipindi cha Kwaresima ni wakati muafaka wa kujiandaa ili kuadhimisha Pasaka ya Bwana, muda wa neema na kisakramenti cha wongofu wa ndani kinachotangaza na kutekeleza uwezekano wa kumwongokea Mwenyezi Mungu kwa moyo na maisha yote! “Na kwa sababu ya kuongezeka kwa maasi, upendo wa wengi utapoa” (Rej. Mt. 24:12) ndiyo kauli mbiu inayoongoza Ujumbe wa Kwaresima kwa mwaka 2018. Katika ujumbe huu, Baba Mtakatifu anazungumzia kuhusu manabii wa uongo, moyo uliopooza kwa ubaridi; umuhimu wa sala, matendo ya huruma na kufunga ili kuwasha moto wa Fumbo la Pasaka kwa kuabudu Ekaristi Takatifu na kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho!

Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Francisko Siku ya alhamisi, tarehe 15 Februari 2018, kuanzia saa 3:30 majira ya asubuhi kwa saa za Ulaya atakutana na kuzungumza na Wakleri wa Jimbo kuu la Roma, kama sehemu ya utekelezaji wa mapokeo ya Jimbo kuu la Roma, ambapo Wakleri wanakutana na Askofu wao ili kuanza safari katika jangwa la maisha ya kiroho. Askofu mkuu Angelo De Donatis, Makamu Askofu wa Jimbo kuu la Roma anasema, hiki kitakuwa ni kipindi cha kuadhimisha Liturujia ya Kitubio cha jumla pamoja na kutoa nafasi kwa wakleri kuweza kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho. Baadaye, Baba Mtakatifu atazungumza na Wakleri wenzake kwa faragha, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, mjini Roma.

Askofu mkuu Angelo De Donatis, anawaalika waamini wa Jimbo kuu la Roma kutafakari kwa kina na mapana kuhusu magonjwa ya maisha ya kiroho, yaliyopembuliwa wakati wa Kongamano la Kichungaji, Jimbo kuu la Roma, tarehe 18 Septemba 2017 mintarafu: Uchumi unaowatenga watu, saratani ya ubinafsi na uchoyo; malumbano yasiyokuwa na tija wala mashiko kati ya Wakristo; hali ya watu kujikatia tamaa ya maisha pamoja na waamini kukengeuka na kumezwa mno na malimwengu. Kumbe, Kwaresima ni kipindi kilichokubalika kwa waamini kufanya tathmini ya kina, kushirikishana na kujitakasa, tayari kutoka kifua mbele ili kutangaza na kushuhudia “Furaha ya Injili”.

Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume “Evangelii gaudium” yaani “Furaha ya Injili” anawataka waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuondokana kabisa na uchumi unaobagua, uchu wa mali na madaraka na kwamba, fedha inapaswa kutumika kwa ajili ya huduma na wala si chombo cha kutawala na kuwanyanyasa watu. Waamini wajitahidi kujenga na kudumisha umoja, usawa, udugu na mshikamano, sanjari na utamadunisho, ili tunu msingi za maisha ya Kiinjili ziweze kupenya katika mila, desturi na tamaduni za watu kwa kuondoa yale yote yanayosigana na Injili ya Kristo ili kupyaisha maisha ya watu!

Baba Mtakatifu anaikumbusha mihimili ya uinjilishaji juu ya changamoto na matatizo mbali mbali wanayoweza kukutana nayo katika hija ya maisha na utume wao. Changamoto kubwa inajikita katika maisha ya kiroho: ubinafsi na utepetevu wa maisha ya kiroho, hali ya kukata tamaa ya maisha, kwa kuwa na mahusiano tenge na Kristo Yesu, Bwana na Mwalimu; kwa kumezwa mno na malimwengu, migogoro na kinzani zisizokuwa na tija wala mashiko kwa ustawi, maendeleo na mafao ya Kanisa. Tafakari hii iwasaidie waamini kuweza kuwa na sera na mbinu mkakati wa pamoja, utakaoweza kuwasilishwa kwa Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Kongamano la Kichungaji, Jimbo kuu la Roma. Waamini wakumbuke daima kwamba, wagonjwa ndio wanaomhitaji daktari. Kumbe, wanaweza kutweka hadi kilindini huku wakiwa wamejipyaisha kwa ari na moyo mkuu, tayari kutangaza Injili ya Fumbo la Pasaka, kwa walimwengu wote!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.