2018-02-10 17:08:00

Waziri Mkuu wa Estonia akutana na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 9 Februari 2018 amekutana na kuzungumza na Waziri mkuu Jüri Ratas wa Estonia, ambaye pia alibahatika baadaye kukutana na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Monsinyo Antoine Camilleri, Katibu mkuu msaidizi wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.  Katika mazungumzo yao, kati ya Baba Mtakatifu na Waziri mkuu wa Estonia, wameridhishwa na uhusiano mzuri wa kidiplomasia uliopo kati ya Vatican na Estonia bila kusahau mchango wa Kanisa katika ustawi, maendeleo na mafao ya wananchi wa Estonia. 

Baadaye, Baba Mtakatifu na mgeni wake, waliyaelekeza mawazo yao kwenye masuala ya kitaifa na kikanda, lakini zaidi kuhusu utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote pamoja na changamoto ya wimbi kubwa la wakimbizi na wahamiaji duniani. Hatimaye, waligusia pia mchakato wa Jumuiya ya Kimataifa katika kukabiliana na kinzani, migogoro na mipasuko ya kijamii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S

Vatican News!

 

 








All the contents on this site are copyrighted ©.