2018-02-07 17:28:00

Mh. Padre Willem Christiaans, OSFS ateuliwa kuwa Askofu, Namibia


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa Padre Willem Christiaans, OSFS, kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Keetmanshoop, lililoko nchini Namibia. Kabla ya uteuzi huu Askofu mteule Willem Christiaans alikuwa ni Msimamizi wa kitume wa Jimbo Katoliki la Keetmanshoop. Alizaliwa tarehe 12 Februari 1961 huko Gabis, Karasburg, Jimbo Katoliki la Keetmanshoop. Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa akaweka nadhiri zake za daima tarehe 23 Januari 1988 na kupewa Daraja Takatifu ya Upadre 10 Desemba 1988.

Katika maisha na utume wake kama Padre, Askofu mteule Willem Christiaans amewahi pia kuwa ni mkurugenzi wa wanafunzi wanaojiandaa kuingia hatua ya Unovisi Shirikani kwake; Mkurugenzi wa wasomi wa Shirika, Mkuu wa Shirika Kikanda tangu mwaka 1993 hadi mwaka 2005, kwa vipindi vitatu mfululizo. Kuanzia mwaka 2005 hadi mwaka 2013 amekuwa Paroko, Makamu wa Askofu, Mkurugenzi wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa na tarehe 26 Julai 2017 akateuliwa kuwa Msimamizi wa Kitume wa Jimbo Katoliki la Keetmanshoop, lililoko nchini Namibia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.