2018-01-14 14:06:00

Papa Francisko anawaalika waamini kumsindikiza kwa sala!


Hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Chile kuanzia tarehe 15 – 18 Januari 2018 inaongozwa na kauli mbiu “Amani yangu nawapa”. Baba Mtakatifu anatarajiwa kutembelea Peru kuanzia tarehe 19 – 22 Januari 2018 kwa kuongozwa na kauli mbiu “Umoja wa matumaini”. Baba Mtakatifu wakati wa sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 14 Januari 2018 amewaomba waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kumsindikiza kwa njia ya sala na sadaka yao wakati wa hija yake ya kiutume huko Amerika ya Kusini.

Kama ilivyo desturi yake, Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi jioni, tarehe 13 Januari 2018 alikwendenda kusali kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mkuu lililoko hapa mjini Roma, ili kujikabidhi kwa Bikira Maria, Afya ya Warumi, anapoanza hija yake ya ishirini na mbili kimataifa, huko Amerika ya Kusini. Hizi ni taarifa zilizotolewa na Dr. Greg Burke, Msemaji mkuu wa Vatican. Hivi karibuni, Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican katika mahojiano maalum na Vatican News alikiri kwamba, hija ya Baba Mtakatifu Francisko huko Amerika ya Kusini inakabiliwa na changamoto pevu, ambazo anataka kuzivalia njuga, kwa kuwashirikisha amani inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake, ili hatimaye, waweze kujenga umoja na udugu katika matumaini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.