2018-01-03 13:48:00

Baraza la Makanisa Ulimwenguni lina laani mashambulizi nchini Nigeria


Baraza la Makanisa Ulimwenguni limelaani mashambulizi yaliyofanywa na Kikundi cha Boko Haram nchini Nigeria dhidi ya Wakristo waliokuwa wanarejea makwao baada ya kuhudhuria maadhimisho ya Sherehe ya Mkesha wa Bikira Maria Mama wa Mungu, Siku ya 51 ya Kuombea Amani Duniani na Mwaka Mpya 2018. Watu 16 wamepoteza maisha katika Kanisa moja huko mjini Omuku, Kusini mwa Nigeria, mapema Jumatatu asubuhi, tarehe Mosi, Januari 2018. Dr. Olav Fykse Tveit katika salam zake za rambi rambi anasikitika sana kuona waamini wakitendewa ukatili kama huo baada ya kutoka kwenye Ibada, kuomba neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu ili kuanza vyema Mwaka Mpya 2018, lakini wamekutwa na mauti katika mazingira ya kutatanisha. 

Baraza la Makanisa Ulimwenguni lina laani mauaji ya watu wasiokuwa na hatia. Umefika wakati kwa familia ya Mungu nchini Nigeria kuanza kutembea katika mwanga wa haki na amani kwa watu wote; kwa kusimama kidete kulinda na kudumisha utu wa wote, uhuru wa kuabudu, ulinzi na usalama. Baraza la Makanisa Ulimwenguni linawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuendelea kuwakumbuka waliopoteza maisha katika shambulio hili na wale ambao wamejeruhiwa vibaya ili waweze kupona na kurejea tena katika maisha yao ya kila siku! Taarifa ya Jeshi la Polisi kutoka Nigeria inaonesha kwamba, kumekuwepo pia mashambulizi katika miji ya Kirigani na Oboh.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.