Maaskofu wa Kanisa Katoliki Kanda ya Mashariki nchini Tanzania,wamesema ili kuendeleza
Ibada na heshima kwa Ekaristi Takatifu wameridhia kufanya Kongamano la Ekaristi Takatifu
kila baada ya miaka mitatu, kwa njia hiyo Kongamano mwaka 2019 litafanyika katika
Jimbo Katoliki Zanzibar.
Hayo yametolewa hayo wakati wa kilele cha Kongamano la Ekaristi Takatifu Kanda ya
Mashariki lililofanyika hivi karibuni katika viwanja vya Msimbazi, Jimbo Kuu Katoliki
Dar es Salaam Tanzania. Wakati wa maadhimisho hayo, Kardinali Polycap Pengo, Askofu
Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam amesoma maazimio hayo na kuthibitisha kuwa,Kongamano
la Ekaristi Takatifu mwaka huu,limekuwa ni neema na baraka kwa waamini wote walioshiriki
maadhimisho hayo na kwa Kanisa kwa ujumla.
Na katika kuendeleza neema na baraka hizo za Mungu kwa taifa kama Maaskofu wa Kanda ya Mashariki, baada ya kupokea maoni na mapendekezo kutoka kwa waamini, makleri na wanakongamano wote, wamekubaliana kufanya Adhimisho la Kongamano la Ekaristi katika Kanda ya Mashariki kila baada ya miaka mitatu. Kutokana na hilo azimio Kongamano la pili la Ekaristi Takatifu katika Kanda ya Mashariki litafanyika Jimbo Katoliki Zanzibar Juni 2019. Hata hivyo ametoa pia sababu ya kutofanyika 2020 kwamba, ni mwaka wa uchanguzi Mkuu katika nchi ya tanzania ambapo wasiweze kuchangnanya mambo mawili pamoja.
Halikadhalika amesema,ili kuendeleza ibada na heshima kwa Ekaristi Takatifu maaskofu
hao wameazimia kuwepo na kuendelezwa kwa makanisa ya kuabudu daima Ekaristi Takataifu,
ambamo Ekaristi Takatifu itawekwa na kuabudiwa kwa masaa 24 kila siku. Makanisa hayo
yajengwe kwenye majimbo yote ya Kanda ya Mashariki na waamini wanaombwa kujitokeza
kwa wingi kwenda kuabudu Ekaristi Takatifu ili waweze kuchota neema ya ukombozi.
Maazimio mengine yaliyotolewa ni kwamba ili kuendeleza malezi ya kiimani kwa watoto
na kuwezesha kutambua na kuthamini nafasi ya Ekarist i Takatifu katika maisha ya kikristo
washiriki wa kongamano hilo wameazimia kuzifanya familia na parokia zao kuwa vituo
vya katekesi na mafundisho endelevu na kina ya imani kuhusu Ekaristi Takatifu kwa
watoto wao.
Hivyo wito ni kwa kwa mapadri, watawa, makatekista, wazazi na walezi wote kusitawisha
utume wa Utoto Mtakatifu na kuwawezesha watoto wote kuwa washiriki wa Shirika hilo
la Utoto Mtakatifu ambalo ni chombo muhimu cha kukuza imani na moyo wa umisisonari
kwa watoto wetu.
Na wakitazama juu ya familia Kardinali Pengo,amesisitiza juu ya Wanandoa wanaojiandaa
kupokea sakramenti ya ndoa na wale ambao tayari wamepokea Sakramenti hiyo wapewe katekesi
na mafundisho ya kina kuhusu Ekaristi Takatifu ili watambue kuwa furaha na upendo
wa ndoa zao zinategemea moja kwa moja muungano wao na Yesu wa Ekaristi. Bila Ekaristi
Takatifu hakuna uhai wa kimungu ndani ya familia. Kadhalika ili kuwezesha waamini
kuwa na ibada za mara kwa mara za Ekaristi Takatifu, parokia zote katika Kanda ya
mashariki zinapaswa kuwa na utaratibu wa kufanya ibada na kuabudu Ekaristi Takatifu
mara moja kwa juma. Waamini wajitokeze kwa wingi kushiri ibada hizo.
Kilele cha Kongamano hilo kilikuwa cha namna yake ambapo palikuwa na maandamano
ya Ekaristi Takatifu kutoka maeneo mbalimbali ya Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam
Tanzania hadi Msimbazi kwa maadhimisho hayo.
Kongamano hilo lilianza tarehe 10-12 Novemba 2017, na kuudhuriwa na maelfu ya waamini
wakiwemo maaskofu, mapadri na waamini walei kutoka majimbo yanayounda Kanda hiyo ya
Mashariki ambayo ni Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Ifakara, Tanga, Morogoro, Zanzibar
na Mahenge. Mkuu wa Kanda hiyo ni Askofu Mkuu Polycarp Pengo.
All the contents on this site are copyrighted ©. |