Kila mmoja amechaguliwa na Bwana Mungu. Na kila mmoja anachukua ahadi ya Bwana
alivyo toa ahadi ya kwamba tembea katika uwepo wangu na kutii na mimi nitakufanyia
hivyo. Kila mmoja wetu anafanya agano na Bwana, lakini unaweza kuamua kufanya au kuacha
maana unao uhuru wa kuchagua.
Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko Jumatatu tarehe 6 Novemba 2017 wakati wa mahubiri
yake katika Kikanisa cha Mtakatifu Martha mjini Vatican. Baba Mtakatifu akitafakari
masomo ya Siku na hasa katika somo la kwanza anaendelea kufafanua zaidi kuwa, Bwana
anapotoa zawadi haiondoi tena kwa maana ya kuitoa leo na kesho kuchukua tena. Mungu
anapoita, ule wito unabaki maisha yote.
Akiendelea na uchambuzi wa barua ya Mtakatifu Paulo kwa Waroma anasisitiza, kuna
zawadi tatu katika historia ya ukombozi yaani zawadi na wito wa watu wa Mungu. Lakini
zawadi hizo hazirudishwi mara zitolewapo na Bwana Mungu kwa maana Mungu ni mwaminifu
anasema Baba Mtakatifu!
Akizitaja zawadi hizo, anasema ya kwanza ni zawadi ya kuchaguliwa, zawadi ya ahadi
na zawadi ya agano. Zawadi hizo zilitendeka kwa Ibrahimu Baba wa Imani na ndivyo
hata sisi tunajaliwa na Mwenyezi Mungu. Baba Mtakatifu anaongeza, kila mmoja wetu
amechaguliwa na Mungu. Kila mmoja wetu anachukua ahadi ambayo Bwana alihaidi kwa watu
wake akisema,”tembea katika uwepo wangu na kunitii na mimi nitakufanyia hivyo.
Kila mmoja anafanya agano na Bwana, lakini kila mmoja yuko huru kufanya hivyo
au kutokufanya, Baba Mtakatifu anathibitisha. Na hiyo anaongeza, linaweza likawa
hata swali la kujiuliza ndani ya nafsi zetu je namna gani ya kufanya uchaguzi huo?
je mimi ninahisi kuchanguliwa au ninahisi kuwa mkristo kwa bahati mbaya? je ninaishije
ahadi yaani ahadi za ukombozi wa safari yangu? je mimi ni mwaminifu wa agano hilo
kama Yeye alivyo mwaminifu?
Kwa upande wa uaminifu ambao Mungu anaonesha kwetu sisi, ni lazima kutafakari kwa
kina juu ya hisia za ukarimu wa Bwana, anayetutunza , anayetutafuta tunapokwenda
mbali naye anasema Baba Mtakatifu!
Akielezea zaidi juu ya barua ya Mtakatifu Paulo katika kuchaguliwa na Mungu , anasema
mtume anarudia mara nne katika maneno mawili ya kutotii na huruma. Lakini kumbuka
kuwa, mahali palipo na mojawapo, lazima iendane na nyingine kwa maana ndiyo safari
ya ukombozi wetu.
Hiyo ina maana, katika aina tatu za safari , yaani safari ya kuchaguliwa, kuelekea
katika ahadi na agano daima vitafuatana na dhambi na kutokutii, lakini dhidi ya kutokutii
ipo daima huruma ya Mungu. Ni sawa na hatua ya safari yetu kuelekea katika ukomavu.
Daima kuna huruma kwa sababu Bwana ni mwaminifu na kamwe haondoi zawadi ambazo amekwisha
itoa.
Je ni kwasababu gani zawadi hizi haziondolewi? Baba Mtakatifu anasema, mbele
ya udhaifu wetu na dhambu zetu, daima ipo huruma. Hata Mtume Paulo anapofika katika
tafakari hilo, anapiga hatua mbele kwa maana hatoi maelezeo bali anaabudu. Ina maana
ya kuabudu , kusifu kwa kimya mbele ya fumbo la kutokutii na huruma inayotufanya tuwe
huru, na mbele ya uzuri wa zawadi ambazo hazitolewi kama ile ya kuchaguliwa, ahadi
na agano.
Na mwisho Baba Mtakatifu anatoa wito ya kwamba, itakuwa vema na wajibu wa kutafakari
kwa siku ya leo juu ya kuchaguliwa kwetu, ahadi ya Bwana anayo kwetu sisi, pia jinsi
gani ninaishi agano na Bwana.
Je Neno la Bwana linajikitaje ndani ya maisha yangu ambalo ni huruma ya Bwana mbele ya dhambi na kutotiii kwangu? Ninao uwezo wa kusifu Mungu kwa mema mengi aliyoitendea? ....Na zaidi kila mmoja leo hii asifu na kuabudu bila kusahau daima zawadi na wito wambao Mungu ametoa bila kuuondoa.
Sr Angela Rwezaula
Idhaa ya kiswahili ya radio Vatican
All the contents on this site are copyrighted ©. |