2017-11-06 16:54:00

Papa:Tumsifu Mungu anayetoa zawadi ya wito bila kuuondoa kamwe!


Kila mmoja amechaguliwa na Bwana Mungu. Na kila mmoja anachukua ahadi ya Bwana alivyo toa ahadi ya kwamba tembea katika uwepo wangu na kutii na mimi nitakufanyia hivyo. Kila mmoja wetu anafanya agano na Bwana, lakini unaweza kuamua kufanya au kuacha maana unao uhuru wa kuchagua.
Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko Jumatatu tarehe 6 Novemba 2017 wakati wa mahubiri yake katika Kikanisa cha Mtakatifu Martha mjini Vatican. Baba Mtakatifu akitafakari masomo ya Siku  na hasa katika somo la kwanza anaendelea kufafanua zaidi kuwa, Bwana anapotoa zawadi haiondoi tena kwa maana ya kuitoa leo na kesho kuchukua tena. Mungu anapoita,  ule wito unabaki maisha yote.

Akiendelea na uchambuzi wa barua ya Mtakatifu Paulo kwa Waroma anasisitiza, kuna zawadi tatu katika historia ya ukombozi yaani zawadi na wito wa watu wa Mungu. Lakini zawadi hizo hazirudishwi mara zitolewapo na Bwana Mungu kwa maana Mungu ni mwaminifu anasema Baba Mtakatifu!
Akizitaja  zawadi hizo, anasema ya kwanza  ni zawadi ya kuchaguliwa, zawadi ya ahadi na zawadi ya agano. Zawadi hizo zilitendeka  kwa Ibrahimu Baba wa Imani  na ndivyo hata sisi tunajaliwa na Mwenyezi Mungu. Baba Mtakatifu anaongeza, kila mmoja wetu amechaguliwa na Mungu. Kila mmoja wetu anachukua ahadi ambayo Bwana alihaidi kwa watu wake akisema,”tembea katika uwepo wangu na kunitii  na mimi nitakufanyia hivyo.

Kila mmoja anafanya agano na Bwana, lakini kila mmoja yuko huru kufanya hivyo  au kutokufanya, Baba Mtakatifu anathibitisha. Na hiyo anaongeza,  linaweza likawa hata swali la kujiuliza ndani ya nafsi zetu je namna gani ya kufanya uchaguzi huo? je mimi ninahisi kuchanguliwa au ninahisi kuwa mkristo kwa bahati mbaya? je ninaishije ahadi yaani ahadi za ukombozi wa safari yangu? je mimi ni mwaminifu wa agano hilo kama Yeye alivyo mwaminifu?
Kwa upande wa uaminifu ambao Mungu anaonesha kwetu sisi, ni lazima kutafakari kwa kina  juu ya hisia za ukarimu wa Bwana, anayetutunza , anayetutafuta tunapokwenda mbali naye anasema Baba Mtakatifu!

Akielezea zaidi juu ya barua ya Mtakatifu Paulo katika kuchaguliwa na Mungu , anasema mtume anarudia mara nne katika maneno mawili ya kutotii na huruma. Lakini kumbuka kuwa, mahali palipo na mojawapo, lazima iendane na nyingine kwa maana ndiyo safari ya ukombozi wetu.
Hiyo ina maana, katika aina tatu za safari , yaani safari ya kuchaguliwa, kuelekea katika ahadi na agano daima vitafuatana na dhambi na kutokutii, lakini dhidi ya kutokutii ipo daima huruma ya Mungu. Ni sawa na hatua ya safari yetu kuelekea katika ukomavu. Daima kuna huruma kwa sababu Bwana ni mwaminifu na kamwe haondoi zawadi ambazo amekwisha itoa.

 Je ni kwasababu gani zawadi hizi haziondolewi? Baba Mtakatifu anasema,  mbele ya udhaifu wetu na dhambu zetu, daima ipo huruma. Hata Mtume Paulo anapofika katika tafakari hilo, anapiga hatua mbele kwa maana hatoi maelezeo bali anaabudu. Ina maana ya kuabudu , kusifu kwa kimya mbele ya fumbo la kutokutii na huruma inayotufanya tuwe huru, na mbele ya uzuri wa zawadi ambazo hazitolewi kama ile ya kuchaguliwa, ahadi na agano. 
Na mwisho  Baba Mtakatifu anatoa wito ya kwamba, itakuwa vema na wajibu wa kutafakari kwa siku ya leo juu ya kuchaguliwa kwetu, ahadi ya Bwana anayo kwetu sisi,  pia jinsi gani ninaishi agano na Bwana.

Je Neno la Bwana linajikitaje ndani ya maisha yangu ambalo ni huruma ya Bwana mbele ya dhambi  na kutotiii kwangu? Ninao uwezo wa kusifu Mungu kwa mema mengi aliyoitendea? ....Na zaidi kila mmoja leo hii asifu na kuabudu  bila kusahau daima zawadi  na wito wambao Mungu ametoa bila kuuondoa.


Sr Angela Rwezaula
Idhaa ya kiswahili ya radio Vatican

 








All the contents on this site are copyrighted ©.