2017-08-18 13:31:00

Watu wa DRC wakumbwa na baa la njaa na watoto kupata chanjo ya Surua


Wakati machafuko na watu kutawanywa kukiendelea nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC , watu milioni 7.7 wanakabiliwa na njaa kubwa.Hayo yametolewa na mashirika ya Umoja wa Mataifa, la chakula na kilimo FAO na la mpango wa chakula duniani WFP. Katika ripoti yao mpya iliyotolewa 16 Agosti 2017 mashirika hayo yanasema hilo ni ongezeko la asilimia 30 katika kipindi cha mwaka mmoja . Ripoti hiyo inayotathimini hali ya uhakika wa chakula (IPC) imetaja kati ya Juni 2016 na Juni 2017 , idadi kubwa ya watu walio katika dharura ya kutokuwa na uhakika wa chakula daraja la 4 na la 3 linalokaribia baa la njaa na kuhitaji msaada wa haraka wa chakula, imeongezeka kwa watu milioni 1.8. kutoka milioni 5.9 na kufikia watu milioni 7.97.

FAO na WFP wanasema zaidi ya mtu mmoja kati ya 10 wanaoishi vijijini wanakabiliwa na njaa ya kupindukia. Hali hii imechangiwa na machafuko yanayoendelea katika majimbo ya Kasai na Tanganyika ambako watu zaidi ya milioni 1.4 wamelazimika kufungasha virago na kuzikimbia nyumba zao. Aidha  Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP na washirika wake World Vision wamezindua operesheni ya dharura Jumatano 16 Agosti 2017 ya kugawa chakula kwa wakimbizi wa ndani 42,000 kwenye majimbo ya Kasai nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC.
Kwa mujibu wa WFP katika maeneo yanayofikika wanapanga kuwasaidia watu 25,000 Kasai ya Kati na 17,000 mkoa wa Kasai katika siku chache zijazo. Hata hivyo shirika hilo limesema linahitaji dola milioni 17.3 ili kuharakisha operesheni hiyo ambayo jumla inawalenga watu 250,000 wasiojiweza majimbo ya Kasai na Kasai ya  Kati kuanzia Septemba hadi Desemba mwaka huu.Mgao huo wa chakula umeanza katika mji wa Tshilumba na utaendelea mwezi wote huu. 

Wakati huo huo ikiukwaji wa sheria za kimataifa unaathari kubwa hasa katika maeneo yenye mizozo na kusabishamatatizo makubwa ya ulinzi na usalama kimataifa. Katika ujumbe maalumu wa siku ya kimataifa ya usaizidi wa kibinadamu, shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya wanawake (UN Women) limesema athari zake hazisemeki, kwani ni  mabomu na makombora yanasambaratishwa mashuleni, mahospitalini, masoko na maeneo ya kuabudu.Ni watoto wengi wanaopolewa kwenye vifusi vya nyumba zao kila kunapokucha huku maelfu ya wasichana wakiendelea kuwa hatarini na ndoa za utotono na shuruti aidha  wavulana wakishinikizwa kuingia vitani na makundi yenye silaha, wakati huo ukatili wa kingono ukizidi kusambaratisha maisha ya wanawake na wasichana.

Shirika hilo linasema katika siku ya kumbukumbu hiyo, msisitizo unatolewa kwamba raia na wahudumu wa misaada sio walengwa katika mizozo , ni lazima dunia ishikamane kubadili hali ya simanzi na huzuni  iliyotawala kwa raia waliojikuta katikati ya mizozo wasiyoijua chanzo chake. Aidha limewapongeza wahudumu wa misaada ya kibinadamu kwa mchango wao mkubwa katika kunusuru Maisha ya mamilioni ya watu hao.

Sr Angela Rwezaula
Idhaa ya Kiswahili ya Radio vatican

 








All the contents on this site are copyrighted ©.