2017-05-30 06:50:00

Kanisa Barani Afrika: Chombo cha haki, amani na upatanisho!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Kupaa Bwana, Mbinguni, tarehe 25 Mei 2017, alikutana na kuzungumza na wakleri pamoja na watawa wa Jimbo Katoliki la Bata, huko Equatorial Guinea kwa kukazia utambulisho wao kama Kanisa familia ya Mungu inayowajibika, dhana iliyotiliwa mkazo sana katika maadhimisho ya Sinodi ya kwanza ya Maaskofu kwa ajili ya Kanisa la Afrika. Huu ni mwaliko wa kuendelea pia kushikamana na Kanisa la kiulimwengu katika mchakato mzima wa uinjilishaji, lakini kwa namna ya pekee na Askofu wao Juan Matogo Oyama.

Kardinali Filoni anawapongeza wakleri na watawa kuwa mchakato mzima wa uinjilishaji unaofumbatwa katika ushuhuda wa huduma makini katika sekta ya elimu, afya, ustawi na maendeleo endelevu ya watu wa Mungu nchini Equatorial Guinea: dhamana, utume na asili ya Kanisa ambalo linatumwa na Kristo Yesu ili kuinjilisha. Uinjilishaji ni sehemu ya vinasaba vya maisha, utume na changamoto kwa Kanisa linalohamasishwa kuwa ni shuhuda na chombo cha uwepo wa Kristo kati pamoja na watu wake! Ushuhuda huu unaoneshwa kwa namna ya pekee kwa njia ya wakleri na watawa wanaojitahidi kuishi mashauri ya Kiinjili kama njia ya kutaka kufanana zaidi na Kristo.

Kardinali Filoni pamoja na mambo mengine, anaendelea kukazia umuhimu wa ushuhuda wenye mvuto na mashiko kwa ajili ya maisha na utume wa Mama Kanisa. Wanakumbushwa kwamba wao wanapaswa kwa hakika kuwa ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa; vyombo na mashuhuda wa huduma ya upatanisho, haki na amani kwa familia ya Mungu Barani Afrika. Mambo msingi yaliyovaliwa njuga na Mababa wa Sinodi mbili za Maaskofu kwa ajili ya Afrika. Katika mapambazuko ya millenia ya tatu ya Ukristo, Mtakatifu Yohane Paulo II anawataka waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kutubu na kuongoka ili kuchuchumilia utakatifu wa maisha, ili kuweza kuwa na sauti ya kimaadili ndani ya jamii inayowazunguka.

Maisha na utume wa wakleri na watawa ndani ya Kanisa yanaweza kuchanua na kuzaa matunda mengi ikiwa kama yanabubujika kutoka katika utakatifu wa maisha, kumbe, hata katika shida na mahangaiko yao, wanapaswa kutweka hadi kilindini. Wawe waaminifu kwa mashauri ya Kiinjili, tayari kuwatangazia maskini Habari Njema ya Wokovu na kuendelea kuwa ni mashuhuda wa furaha ya Injili, haki na amani. Wajitahidi kushinda kishawishi cha uchu wa mali na madaraka, daima wakionesha upendo na mshikamano kwa maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Waoneshe upendo na ukarimu kwa njia ya ushuhuda wa Injili ya upendo.

Kardinali Filoni anasikitika kusema kwamba, kwa miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na wimbi kubwa sana la Wakleri kuhama nchi zao na kukimbilia kwenda Ulaya na Marekani! Kuna tabia ya baadhi ya mapadre na watawa kukataa kwenda kufanya utume kwenye maeneo ya vijijini, kwani wanataka kuponda raha mijini, eti kufa kwaja! Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, wanatafuta kwanza Ufalme wa Mungu na mengine yote watapewa kwa ziada, vinginevyo watajikuta wakiwa wamemezwa na malimwengu na huko ndiko kwenye kilio na kusaga meno!

Kumbe, uaminifu kwa mashauri ya Kiinjili, upendo katika kutangaza na kushuhudia Injili, huduma makini kwa familia ya Mungu kwa njia ya karama ya mashirika husika pamoja na maadhimisho ya mafumbo ya Kanisa ni muhimu sana kwa maisha na wito wa wakleri na watawa ndani ya Kanisa. Wahakikishe kwamba, wanatumia nguvu, akili, uwezo na utajiri wa maisha yao ya kiroho katika mchakato mzima wa uinjilishaji. Mapadre na watawa wajenge na kudumisha umoja, upendo na mshikamano unaodhihirishwa katika maisha ya kijumuiya; fursa makini ya kumsikiliza Roho Mtakatifu, tayari kusoma alama za nyakati.

Hii ni njia muafaka ya kupambana na ukabila usiokuwa na tija wala mvuto kwa ustawi na maendeleo ya familia ya Mungu. Mapadre washikamane na Askofu wao mahalia tayari kutangaza na kushuhudia furaha ya Injili. Waoneshe utii unaofumbatwa katika Injili na kwamba uongozi na madaraka ni kwa ajili ya huduma kwa familia ya Mungu na wala si vinginevyo! Daima Msalaba wa Kristo uwe ni alama na kielelezo makini cha utii na huduma makini kwa familia ya Mungu. Ikumbukwe kwamba, uchu wa mali na madaraka kama anavyokaza kusema Baba Mtakatifu Francisko ni hatari sana kwa maisha, wito na utume wa Kipadre ndani ya Kanisa.

Mihimili ya uinjilishaji iwe ni mashuhuda amini wa utii, usafi kamili na ufukara, kielelezo makini cha furaha ya Injili. Utakatifu wa maisha unafumbatwa katika sala, tafakari makini ya Neno la Mungu linalomwilishwa katika matendo ya huruma: kiroho na kimwili; kwa kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya mafumbo ya Kanisa, kwa ibada na uchaji; kwa kupokea na kutoa Sakramenti ya huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake. Daima watambue kwamba, Kristo Yesu anaendelea kuambatana nao katika safari ya maisha yao, kama ilivyokuwa kwa wanafunzi wa Emau!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.