2017-04-12 06:56:00

Papa Francisko anaipongeza Radio Renascenca kwa kuadhimisha Miaka 80


Radio Renascenca inayomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki nchini Ureno inaadhimisha kumbu kumbu ya miaka 80 tangu ilipoanza kupasua mawimbi, ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu miongoni mwa familia ya Mungu inayozungumza kugha ya kireno! Radio hii imekuwa ni chombo muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa katika tasnia ya habari! Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Askofu mkuu Angelo Becciu, Katibu mkuu msaidizi wa Vatican na kusomwa na Askofu mkuu Rino Passigato, Balozi wa Vatican nchini Ureno anawapongeza wadau mbali mbali ambao wamejisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa watu wa mataifa! Radio hii imekuwa ni chombo ambacho kimeliwezesha Kanisa kupandikiza mbegu ya Habari Njema ya Wokovu katika akili na nyoyo za watu, kiasi cha kuyachachua mahusiano ya kidugu; sanjari na kukuza pamoja na kudumisha huruma ya Mungu inayomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu.

Baba Mtakatifu anaendelea kukaza akisema, Radio Renascenca imekuwa ni msanii wa pekee ambaye amewawezesha waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema kusali, kutafakari sanjari na kusaidia mchakato wa Uinjilishaji kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya kijamii. Kilele cha maadhimisho haya, kilikuwa, Jumatatu tarehe 10 Aprili 2017 kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Kardinali Josè Macario do Nascimento Clemente, Patriaki wa Jimbo kuu la Lisbon, Ureno. Kwa sasa Radio hii inajumuisha makundi makubwa manne yaani: Renascenca, RFM, Mega hits na Radio SIM, ambayo yanaadhimisha pia kumbu kumbu ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwake chini ya mwamvuli wa Radio Renascenca, Mama yao wote! Kwa miaka yote hii, chombo hiki kimekuwa na manufaa makubwa katika mchakato mzima wa Uinjilishaji; upashanaji wa habari kadiri ya mwanga wa Injili sanjari na burudani ya kukata na shoka!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.