Sakramenti ya Ndoa ni mahali patakatifu panapojenga na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kifamilia. Hapa ni mahali muafaka pa kuishi na kumwilisha huruma ya Mungu katika maisha ya mwanadamu! Wito wa ndoa familia ni zawadi, tena ni zawadi kubwa sana kutoka kwa Mungu, zawadi amabayo inahitaji upendo na heshima na hasa kwa wanandoa wenyewe. Baba Mtakatifi katika Waraka wa kitume “Misericordia et misera” yaani Huruma na amani, anatuambia; zawadi ya ndoa ni wito mkubwa, ambapo mwanaume na mwanamke kwa neema ya Kristo huitikia wito wa upendo, ambao umejaa ukarimu, uaminifu na subira. Na huu ndiyo wito utengenezao uzuri wa familia, na uzuri huu unaletwa na upendo,na hii ndiyo furaha ya Kanisa, anatuambia Baba Mtakatifu.
Wito wa ndoa na familia ni safari ya maisha, safari imwelekezayo Mkristo, mwanaume na mwanamke, kuishi kwa uaminifu na kupendana kwa muda wa maisha yao yote, na kuahidi uaminifu huu baina yao na Mungu. ila daima ikumbukwe, pia mara nyingi safari hii ya maisha inakumbwa na mahangaiko mengi, mateso, usaliti na upweke hasi unaopelekea mtu kukata na kujikatia tamaa ya maisha, kiasi hata cha kuchungulia kaburi, jambo ambalo linahitaji sana neema ya Kimungu katika kuyapita hayo. Neema ya Sakramenti ya Ndoa siyo tu kwa ajili ya kuimarisha familia, bali pia ni sehemu ya kipekee ya kuishi huruma ya Mungu, pamoja na fadhila za kikristo ambapo hutoa mwonekano chanya wa familia. Jubilee ya mwaka wa huruma ya Mungu umeleta mwanga na mwonekano mpya wa familia na hasa katika kuishi huruma ya Mungu, huruma ambayo huiwezesha kila familia kusimama na kuishi kadri ya upendo wa Mungu.
Katika kuishi huruma ya Mungu, yatupasa kukumbuka ya kuwa kila mmoja wetu anao utajiri wa uzuri na ubaya katika maisha yake, na hicho ndicho kinfanyacho kila mmoja kuwa tofauti na mwingine, ila huruma ya Mungu yatuunganisha na kutuleta pamoja katika upendo. Upendo huu ndiyo ufanyao wanandoa kuishi pamoja bila kuona tofauti baina yao, na hivyo kushiriki kikamilifu katika maisha ya familia kama sehemu ya watu wa Mungu wanaosafiri bila kuchoka kuelekea kwenye ufalme wa Mungu uliojaa haki, upendo, msamaha na huruma.
Mwaka Mtakatifu wa Jubilee ya huruma ya Mungu, unawakumbusha, wanandoa kuangalia na kuishi maisha ya Liturujia na sala katika mwonekano wa huruma ya Mungu. Na katika hili, ni dhahiri kwamba ni Mungu mwenyewe awezae kutoa matumaini, kwani hakuna chochote au yeyote awezaye kumtenganisha mtu na upendo wa Mungu. Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu sasa umeisha na Mlango Mtakatifu umefungwa, lakini mlango wa huruma ya Mungu katika moyo wa mkristu utabaki daima kuwa wazi. Mwaka wa jubilee ya huruma ya Mungu umetufundisha kwamba Mungu humjia mwanadamu katika huruma ili pia huyu mwanadamu apate kumwendea mwanadamu mwingine kama kaka na dada katika huruma.
Hivyo, kutamani kuishi katika Kristo au karibu na kristo, ni sambamba na kuwa karibu kwa kila Mkristo kama ndugu na hii inatupa upendeleo kutoka kwa Mungu kama alama ya kweli ya huruma ya Mungu. Hapa moyo wa huruma ya Mungu hukutana na Moyo wa mwanadamu, na hivyo moyo wa mwanadamu hupata uponyaji kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kumbe, zawadi ya wito wa ndoa na familia, unahitaji neema, neema itokayo kwa Mungu, na ndoa hupokea zawadi na zawadi hii ni watoto, na watoto hawa huitaji malezi mazuri, afya njema pamoja na elimu. Hivyo kila mmoja ajitahidi kulipokea hili na kuliishi na hivyo kupata neema na baraka katika maisha ya ndoa, na yote yajengeke katika upendo. Kwa kumalizia Baba Mtakatifu anatualika tuishi kwa vitendo maneno haya; kwa upendo ninaishi, kwa msamahana nimefanywa upya na kwa huruma nimefanywa kuwa chombo cha huruma ya Mungu.
Kutoka katika studio za Radio Vatican, ni mimi Pd. Agapiti Amani, ALCP/OSS.
All the contents on this site are copyrighted ©. |