2017-02-20 12:00:00

Papa Francisko kutembelea Kanisa Anglikani Roma, 26 Februari 2017


Dr. Greg Burke, Msemaji mkuu wa Vatican amethibitisha kwamba, Jumapili tarehe 26 Februari 2017, Saa 10: 00 majira ya jioni kwa saa za Ulaya, Baba Mtakatifu Francisko atatembelea na hatimaye kusali kwenye Kanisa la Kianglikani la Watakatifu wote lililoko mjini Roma. Hizi ni juhudi za Baba Mtakatifu Francisko katika kudumisha mchakato wa majadiliano ya kiekumene yanayosimiwa katika: Damu ya mashuhuda na waungama dini ya Kikristo; Uekumene wa sala unaofumbatwa katika tafakari ya Neno la Mungu linalomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu ili kujenga umoja na udugu katika Kristo Yesu; Uekumene wa maisha ya kiroho unaojikita katika kuthaminiana; na hatime, Uekumene wa huduma kwa maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, ili kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao! Hawa ni wakimbizi na wahamiaji, maskini wa hali na kipato!

Baba Mtakatifu Francisko akiwa Kanisani hapo atasali pamoja na wenyeji wake Masifu ya Jioni pamoja na kurudia tena ahadi za Ubatizo; watapeana amani na hatimaye, kusali pamoja sala ya Baba Yetu, muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Yesu. Hii italiwa ni fursa kwa Makanisa ya Watakatifu Wote ya Kanisa Katoliki na Watakatifu wote wa Kanisa Anglikani kushirikiana kama ndugu. Baadaye, Baba Mtakatifu atapata pia nafasi ya kubadilisha mawazo na wenyeji wake pamoja na kubadilishana zawadi!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.