2017-01-25 14:19:00

Jimbo kuu la Tabora na mchakato wa majadiliano ya kiekumene!


Askofu mkuu Paul Ruzoka wa Jimbo kuu la Tabora, Tanzania katika mahojiano na Radio Vatican hivi karibuni anasema,  majadiliano ya kiekumene ndani ya Kanisa ni kati ya mada zilizopembuliwa na kutolewa maamuzi na Sinodi ya kwanza ya Jimbo kuu la Tabora iliyoadhimishwa hivi karibuni kwa kuongozwa na kauli mbiu “Yesu hu seba” yaani “Yesu ni taa ya uhai wa  imani yetu”. Kanisa linatambua kwamba, Kristo Yesu nidye muasisi wake na kwamba, aliunda: Kanisa moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume. Kumbe, majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Makanisa ni jitihada za kutaka kujenga na kudumisha umoja wa Kanisa kama Kristo mwenyewe alivyoliombea, liwe na umoja. (Rej. Yn. 17: 21) Ikumbukwe kwamba, asili ya Kanisa ni moja!

Askofu mkuu Ruzoka anakaza kusema,  Maaskofu Mahalia kwa kushirikiana na Khalifa wa Mtakatifu Petro wanapaswa kukoleza ari na mojo wa majadiliano ya kiekumene yanayojikita katika katika: ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake hata kiasi cha kumwaga damu yao; ushuhuda wa sala na maisha ya kiroho kwa kusali na kutafakari pamoja Neno la Mungu linalopaswa kuwa ni dira na mwongozo wa maisha ya Wakristo pamoja na kushikimana kwa dhati katika kuwahudumia maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Askofu mkuu Ruzoka anaendelea kufafanua kwamba, juhudi za majadiliano ya kiekumene zilianza tangu wakati wa maadhimisho ya Mtaguso wa Pili wa Lyon mnamo mwaka 1276; Mtaguso wa Florence wa Mwaka 1437, lakini maadhimisho yote haya hayakuweza kuzaa matunda ya umoja wa Kanisa. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, wakaamua kuivalia njuga changamoto ya majadiliano ya kiekumene; dhamana iliyoendelezwa kwa namna ya pekee na Mtakatifu Yohane XXIII, Mwenyeheri Paulo VI, Yohane Paulo II, Benedikto XVI na kwa sasa kasi ya majadiliano ya kiekumene imeongezeka zaidi chini ya uongozi wa Baba Mtakatifu Francisko.

Askofu mkuu Ruzoka anasema, kwa namna ya pekee kabisa, Jimbo kuu la Tabora lilihamasika kwa maneno ya Mtakatifu Yohane Paulo II wakati wa maadhimisho ya Jubilei kuu ya Miaka 2000 ya Ukristo aliyelitaka Kanisa kuwa ni chombo cha msamaha, haki, amani na upatanisho, ili kuponya dhambi na madonda ya utengano miongoni mwa Wakristo, ili kweli maadhimisho ya Millenia ya tatu ya Ukristo yaweze kuwa ni chachu ya msamaha, upatanisho na umoja wa Kanisa.

Hii ni changamoto pia iliyokuwa imefanyiwa kazi na Mababa wa Sinodi ya kwanza ya Afrika na hatimaye, Papa Yohane Paulo II akachapisha Wosia wa Kitume, Kanisa Barani Afrika, “Ecclesia in Africa” akiitaka Familia ya Mungu Barani Afrika kujikita katika Uenezaji wa Injili unaofumbatwa katika utamadunisho, majadiliano na mchakato wa maendeleo endelevu ya binadamu: kiroho na kimwili, daima Kanisa likiwa ni sauti ya wanyonge!

Jimbo kuu la Tabora linaendelea kutekeleza maazimio ya Sinodi ya kwanza ya Jimbo masuala mbali mbali yaliyobainishwa katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene. Hii ikiwa ni pamoja na kushiriki katika Juma la Sala kwa ajili ya Kuombea Umoja wa Wakristo, kuanzia tarehe 18 - 25 Januari, wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Kuongoka kwa Mtakatifu Paulo, Mwalimu na mtume wa mataifa. Lengo ni kuwajengea waamini uwezo ili kweli waweze kuwa ni mashuhuda na vyombo vya huruma ya Mungu sanjari na kuongeza ushirikiano na mshikamano katika medani mbali mbali za maisha.

Askofu mkuu Paul Ruzoka wa Jimbo kuu la Mwanza anakaza kusema, Jimbo kuu la Tabora limejiwekea pia utamaduni wa kusali pamoja na Wakristo wa Madhehebu mbali mbali wakati wa Jumatatu ya Pasaka na Siku kuu ya Noeli, ili kuweza kuimarisha imani, mwingiliano unaofumbatwa katika maisha ya ndoa na familia, ili familia ziweze kushiriki kikimailifu katika maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa kwa kufuata taratibu, kanuni na sheria zilizowekwa na Mama Kanisa. Hii pia ni dhamana ya kuimarisha ushiriki wa wazazi katika malezi na makuzi ya watoto wao kadiri kanuni msingi, maadili na mwanga wa Injili.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.