2017-01-06 14:08:00

Mbiu ya Mwaka wa Bwana 2017


Siku kuu ya Tokeo la Bwana, yaani Epifania ni kati ya Sherehe kubwa zinazoadhimishwa na Mama Kanisa katika Liturujia ya Mwaka wa Kanisa. Mtoto Yesu aliyezaliwa na Bikira Maria anajifunua kwa mataifa kama Mwana wa Mungu, Masiha na Mwanga wa Mataifa. Mama Kanisa katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, anatangaza pia Fumbo la Pasaka, linaloonesha kwa namna ya pekee, utukufu wa Kristo kati ya watu wake hadi pale atakapokuja tena kuwahukumu wazima na wafu. Katika hija ya maisha ya kila siku, waamini wanajitahidi kumwilisha Fumbo la Ukombozi, kiini cha maadhimisho haya ni Liturujia ya Mwaka wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee, Siku kuu tatu zinazoonesha: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo kutoka katika wafu, yaani Siku kuu ya Pasaka ambayo kwa Mwaka huu itaadhimishwa hapo tarehe 16 Aprili 2017.

Kila Jumapili, Mama Kanisa anaadhimisha Pasaka ya Bwana na kuwawezesha waamini kuendelea kuadhimisha tukio hili kuu katika maisha na imani yao; kwani Kristo ameshinda dhambi na mauti. Siku kuu ya Pasaka ni chemchemi ya Siku kuu nyingine zote zinazoadhimishwa na Mama Kanisa. Kipindi cha Kwaresima kwa mwaka huu, kitaanza rasmi tarehe 1Machi 2017 kwa kupakwa majivu, mwaliko wa toba na wongofu wa ndani.

Mama Kanisa ataadhimisha Siku kuu ya Kupaa Bwana Mbinguni hapo tarehe 28 Mei 2017 na Pentekoste, Siku kuu ya kuzaliwa kwa Kanisa na Siku ya Waamini Walei itaadhimishwa hapo tarehe 4 Juni 2017. Jumapili ya kwanza ya Majilio ambayo kimsingi ni mwanzo wa Mwaka Mpya wa Kanisa, na maandalizi ya ujio wa Kristo itaadhimishwa hapo tarehe 3 Desemba 2017. Mama Kanisa anayeendelea kufanya hija yake hapa duniani anatangaza pia Pasaka ya Bwana, anapoadhimisha Siku kuu za Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa; Siku kuu za Mitume na Watakatifu mbali mbali; anapowakumbuka watoto wake waliotangulia katika usingizi wa amani, wakiwa na tumaini katika ufufuko wa wafu. Sifa na utukufu kwa Kristo aliyekuwepo, aliyepo na atakayekuja. Yeye ni Bwana wa Historia na nyakati zote ni zake. Amina.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.