2016-12-12 14:18:00

Ujumbe wa Papa Francisko wa Siku ya 50 ya Kuombea Amani Duniani 2017


Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe Mosi, Januari, Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Mungu anaadhimisha Siku ya Kuombea Amani Duniani. Maadhimisho ya Siku ya 50 kwa Mwaka 2017 yanaongozwa na kauli mbiu “Kutotumia nguvu: mtindo wa siasa ya amani”. Baba Mtakatifu Francisko anaelezea kuhusu vita, kinzani na mipasuko ya kijamii duniani; umuhimu wa kutangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu; Wajumbe na mashuhuda wa amani duniani; umuhimu wa kuzamisha mizizi katika siasa za kutotumia nguvu, mwishoni, Baba Mtakatifu anatoa mwaliko kwa familia ya Mungu duniani pamoja na kuhitimisha ujumbe wake!

Mwanzo mwa Mwaka mpya wa 2017 Baba Mtakatifu anapenda kuwatakia watu wote heri, baraka na amani kwa kutambua kwamba, wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Utu na heshima ya watu wanaoishi katika maeneo ya vita unapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa, kwa kushinda kishawishi cha kutumia siasa ya vita. Miaka 50 iliyopita, Mwenyeheri Paulo VI alituma ujumbe wa amani kwa familia ya Mungu duniani kwa kuonesha kwamba, amani ni chachu ya maendeleo ya watu na kwamba, kinzani, misigano na utaifa usiokuwa na mashiko ni mambo yaliyokuwa yanatishia amani. Kumbe, vita, migogoro na kinzani mbali mbali zinaweza kupatiwa ufumbuzi kwa kujikita katika: sheria, haki, usawa, upendo; ukweli na uhuru, tunu ambazo zinaonesha umuhimu wa pekee hata katika ulimwengu mamboleo.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko anapenda kukazia kutotumia nguvu kuwa ndio unaopaswa kuwa ni mtindo wa maisha ya kisiasa ili kujenga na kudumisha amani duniani na anamwomba Mwenyezi Mungu awasaidie watu kuchota tunu hizi msingi kutoka katika undani wa maisha yao. Upendo na amani ziwe ni tunu ambazo zitasaidia kujenga na kudumisha mahusiano ya binafsi, kijamii na kimataifa. Huu ni mwaliko wa kuondokana na utamaduni wa kulipizana kisasi na kwamba, wahanga wanaweza kuwa ni wadau wa mchakato wa kutotumia nguvu kwa ajili ya ujenzi wa amani katika medani mbali mbali za maisha, ili kweli maamuzi, mahusiano, matendo na nguvu zote za kisiasa ziweze kujielekeza huko.

Baba Mtakatifu anakaza kusema, Karne ya 20 iligubikwa na vita kuu ya dunia, vitisho vya mashambulizi ya silaha za kinyuklia, kinzani na migogoro inayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia kana kwamba, ni Vita ya Tatu ya Dunia. Vyombo vya mawasiliano ya jamii vinaendelea kuonesha jinsi ambavyo dunia imesambaratika kutokana na kinzani na mipasuko ya kijamii inayoendelea kusababisha mateso na mahangaiko ya watu wengi. Vita, ugaidi, vitendo vya kihalifu na mashambulizi ya silaha ni mambo ambayo hayawezi kutabirika. Wakimbizi na wahamiaji wananyanyaswa na kudhulumiwa; kuna wahanga wa biashara haramu ya binadamu pamoja na uharibifu wa mazingira.

Baba Mtakatifu Francisko anauliza, Je, lengo na uharibifu wote huu ni nini? Bila shaka ni kwa ajili ya mafao ya “Mabwana wa vita”. Vita kamwe haitaweza kuwa ni suluhu ya ulimwengu uliomeguka vipande vipande kwani matokeo yake ni: uhamiaji wa nguvu, mateso na mahangaiko na kiasi kikubwa cha rasilimali kinaelekezwa kwenye masuala ya kivita na kuondolewa katika: huduma za afya, elimu, ustawi na maendeleo ya watu wengi duniani. Na mbaya zaidi vita inapelekea vifo vya watu: kiroho na kimwili, kwa wengi na kama si kwa watu wote.

Baba Mtakatifu anaendelea kukaza kwa kusema, Yesu Kristo ni kiini cha Habari Njema ya Wokovu anayekazia amani inayobubujika kutoka katika sakafu ya moyo wa mwanadamu,  kwa kuonesha upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka, upendo unafumbatwa katika msamaha kwa kutoa na kupokea, kwa kuwasamehe hata wale waliowakosea bila kulipiza kisasi. Habari Njema inawarejeshea wadhambi maisha mapya, inawataka Mitume kurejesha panga zao alani mwake na kuendelea na Njia ya Msalaba pale ambapo amani itavunjilia mbali uadui; kwa kuiachia Habari Njema ya Wokovu ifanye kazi yake, ili huruma ya Mungu igange na kuponya majeraha ya vita, ili hatimaye, waweze kugeuka na kuwa ni vyombo na mashuhuda wa upatanisho na amani inayobubujika kutoka katika sakafu ya maisha ya watu!

Wafuasi wa Kristo wanapaswa kushuhudia upendo na wema unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, kutokubali kutumia nguvu ni njia ya kuonesha utu unaodhihirisha upendo na nguvu ya Mungu ambayo inapambana na ubaya kwa kutumia upendo na ukweli. Upendo kwa adui ni kielelezo cha mageuzi katika maisha ya Kikristo; kwa kujibu ubaya kwa wema na wala si kujisalimisha, ili kuvunjilia mbali mnyororo wa ukosefu wa haki msingi! Mama Theresa wa Calcutta anasema familia ya binadamu inahitaji kukaa pamoja na watu kupendana ili kujenga na kudumisha amani na wala si silaha za mahangamizi, kwani biashara ya silaha inaendelea kuwatajirisha wahusika wakati ambapo kuna mashuhuda wa amani wanaendelea kuwasaidia jirani zao. Hawa ni watu wanaosimama kidete: kushuhudia kulinda, kutetea na kudumisha uhai wa binadamu; wanaendeleza moyo wa ukarimu na mapendo; wanaohudumia kwa huruma na upendo; kwa kutambua utu na heshima ya binadamu.

Viongozi wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa wanasutwa na maneno ya Mtakatifu Theresa wa Calcutta kwa kujitambua kuwa ni wahalifu pamoja na ongezeko la umaskini duniani kwani wao pia wamechangia hali hii. Hii ni changamoto ya kuwahudumia wahanga kwa ukarimu, moyo wa majitoleo, kwa kugusa na kuganga madonda yao; kwa kuponya maisha yaliyotikiswa na kusambaratishwa na vita! Duniani kuna mashuhuda na wajenzi wa amani kama vile Mahatma Gandhi na Khan Abdul Ghaffar waliojisadaka kupigania uhuru wa India pasi na kumwaga damu; Martin Luther Mdogo aliyepambana na ubaguzi wa rangi kwa njia ya amani: Hawa ni watu ambao kamwe hawataweza kusahaulika duniani!

Kuna mifano ya wanawake kama Leymah Gbowee na wanawake kutoka Liberia waliosimama kidete kupinga vita kwa njia ya sala pamoja na kuchochea majadiliano yaliyopelekea kuhitimishwa kwa vita ya pili ya wenyewe kwa wenyewe nchini Liberia. Kuna viongozi kama Mtakatifu Yohane Paulo II waliosimama kidete hadi kuta za utawala wa Kikomunisti zikaanguka chali! Ni kiongozi aliyewataka watu kusimamia na kuwa ni mashuhuda wa ukweli na haki kwa kupambana bila kumwaga damu sanjari na kupinga mapambano ya makundi ya kijamii na vita vya kimataifa. Kanisa daima limesimama kidete kutangaza na kushuhudia Injili ya amani kwa kuwataka wahusika kuwa ni wajenzi wa amani ya kudumu!

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kufafanua kwamba, huduma kwa wahanga wa ukosefu wa haki msingi za binadamu ni utajiri na amana ya dini zote duniani na wala si kwa Kanisa Katoliki peke yake kwani hii ni dira inayowaelekeza watu katika  njia ya maisha. Ikumbukwe kuwa, hakuna dini ambayo ni ya kigaidi na kwamba, vita ni kufuru ya Jina la Mungu na kwamba, haiwezekani kutumia jina la Mungu kuhalalisha vita vitakatifu kwani hakuna vita vitakatifu, isipokuwa amani peke yake ndiyo takatifu.

Familia inapaswa kuwa ni mahali muafaka pa kukuza na kudumisha siasa ya kutotumia nguvu kwa kuambata furaha ya upendo. Kwani, familia ni mahali pa kujisadaka na kuhudumiana kama ndugu pamoja na kuvuka kinzani na migogoro si kwa kutumia jazba, nguvu au mkong’oto; bali kwa njia ya majadiliano, heshima na kwa kutafuta mafao ya jirani, huruma na msamaha! Furaha ya upendo ndani ya familia inapaswa kushamiri na kuambata jamii nzima, kwa kujikita katika kanuni maadili na udugu ili kuondokana na mantiki ya woga na wasi wasi; kinzani na vita. Hapa kinachotakiwa ni kudumisha mchakato wa uwajibikaji, heshima na majadiliano katika ukweli na uwazi. Baba Mtakatifu anaiomba Jumuiya ya Kimataifa kuzuia na hatimaye kupiga rufuku kabisa utengenezaji na utumiaji wa silaha za kinyuklia. Ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa itaaminiana na kuthaminiana mintarafu kanuni maadili hakuna sababu ya kuwa na hofu ya mashambulizi ya kinyuklia. Kuna haja pia ya kuondokana na mashambulizi dhidi ya wanawake majumbani pamoja na watoto ili kujenga na kudumisha amani.

Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu, ulikuwa ni mwaliko kwa waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuchunguza dhamiri zao, ili kuruhusu huruma ya Mungu iweze kupenya nyoyoni mwao. Ni mwaliko wa kujenga utamaduni wa kuwashirikisha wengine badala ya kujikita kwenye utandawazi unaowatenga wengine, kwa kuwaonesha upendo, ukarimu, tabasamu pamoja na kutekeleza matendo madogo madogo yanayopandikiza mbegu ya amani na urafiki, ili kuvunjilia mbali mnyororo wa vita, unyonyaji na ubinafsi.

Baba Mtakatifu anatumia maadhimisho ya Siku ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2017 kuwaalika viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kujikita katika kanuni maadili na Heri za Mlimani, muhtasari wa mafundisho makuu ya Yesu katika kupambana na matumizi ya nguvu. Watu wenye heri ni wale wenye: rehema, wapole, wenye njaa na kiu ya haki; wenye moyo safi na wapatanishi. Hii ni changamoto kubwa kwa viongozi wa kisiasa, kidini na kijamii ili kujenga jamii kwa mtindo wa ushuhuda wa amani; huruma kwa kukataa utandawazi usiojali mahangaiko ya watu; unaharibu mazingira nyumba ya wote pamoja na uchu wa mali na madaraka kwa gharama yoyote ile.

Ili kuweza kujikita katika ujenzi wa mfumo mpya kuna haja ya kuambata mshikamano, kwa kuandika historia mpya pamoja na kujenga urafiki wa kijamii, ili kuonesha kwamba, umoja una nguvu zaidi kuliko hata vita na kinzani; kwani, ulimwengu wote kimsingi umeshikamana. Hapa Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kupambana na changamoto hizi  kwa kuungana ili kuanza mchakato mpya wa maisha kwa kuheshimu na kuenzi tofauti zinazojitokeza.

Baba Mtakatifu anapenda kuihakikishia Jumuiya ya Kimataifa kwamba, Kanisa Katoliki litaendelea kuunga mkono mchakato wa ujenzi wa amani duniani. Tarehe Mosi, Januari 2017, Baraza Jipya la Kipapa la Huduma ya Maendeleo Endelevu linazinduliwa rasmi, ili kulisaidia Kanisa kukuza na kudumisha haki, amani na utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote; kwa kuwahudumia wakimbizi, wahitaji, wagonjwa, waliotengwa na jamii; wahanga wa vita na majanga asilia; wafungwa na wasiokuwa na fursa za ajira pamoja na waathirika wa utumwa mamboleo na mateso; mambo yanayodhalilisha utu na heshima ya binadamu! Vitendo vyote vyenye mwelekeo huu vinapania kujenga ulimwengu usiokuwa na vita, hatua muhimu katika haki na amani.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, alitia mkwaju ujumbe huu wa Siku ya 50 ya Kuombea Amani Duniani hapo tarehe 8 Desemba 2016 wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, na Malkia wa amani. Kuzaliwa kwa mwanaye wa pekee, Malaika walikuwa wanamtukuza Mungu na kuitakia dunia amani kwa watu wote wenye mapenzi mema. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwomba Bikira Maria ili aweze kuwaongoza katika mchakato wa kutafuta amani duniani. Kila mtu anatamani amani na kuna mamillioni ya watu wanaoshiriki mchakato wa ujenzi wa amani kwa matendo yao ya kila siku na kwamba, kuna watu wanaojitahidi kufa na kupona ili kujenga amani.

Mwaka 2017, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanahimizwa kujenga amani kwa njia ya sala na maneno yanayomwilishwa katika matendo yanayobubujika kutoka katika sakafu ya nyoyo za watu. Lengo ni kujenga Jumuiya isiyokuwa na vita na inayojitaabisha kutunza mazingira, nyumba ya wote. Hakuna jambo lisilowezekana ikiwa kama watu watamkimbilia Mwenyezi Mungu kwa njia ya amani. Watu wote wanaweza kuwa ni wajenzi wa amani!

Ujumbe huu umehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.