2016-12-05 13:57:00

Kanisa nchini Marekani kuonesha mshikamano na Wahamiaji


Maaskofu wa Marekani wameiteuwa tarehe 12 Disemba, sikukuu ya Bikira Maria wa Guadalupe, kuwa ni siku ya kuonesha mshikamano kwa wakimbizi na wahamiaji, waliofika nchini humo katika harakati za kutafuta maisha bora. Lengo ni kuonesha dhahiri hali, hofu na mahitaji ya wakimbizi na wahamiaji nchini humo. Kardinali Daniel DiNardo, Askofu mkuu wa Galveston-Houston na Mwenyekiti wa Baraza la maaskofu Marekani anasema: wakati Kanisa linaelekea kusherehekea sikukuu ya Noeli, waamini wanakumbushwa kutambua kwamba Kristo Yesu hakuzaliwa katika hali ya ufahari nyumbani kwao, bali katika pango ugenini. Hivyo ni muhimu kuwajali wageni na wahitaji.

Siku hiyo itakuwa siku ya sala, na maadhimisho ya ibada mbali mbali za liturjia katika majimbo ya marekani. Katika mtandao pia kuna sala ya Rozari iitwayo Umoja katika tofauti, unity in diversity. Rozari hiyo ina sala zinazowahusu wakimbizi na wahamiaji. José Horacio Gomez, Askofu mkuu wa Los Angeles na Mwenyekiti msaidizi wa Baraza la maaskofu Marekani anasema: ni muhimu kujitafakari kwamba hali itakuwaje kwa wakimbizi, wahamiaji na wageni iwapo sera za wahamiaji zitabadilishwa dhidi yao. Lengo la Kanisa nchini Marekani ni kutetea haki msingi za wahamiaji, wakitambuliwa kuwa ni binadamu wenye kustahili heshima kwa utu wao na kusaidiwa.

Katika mshikamano huo, ambapo Kamati ya Baraza la maaskofu kwa ajili ya Kanisa la Amerika ya kusini inaadhimisha miaka 50 ya ukusanyaji wa misaada kwa ajili ya Amerika ya kusini, mwaka huu miradi 204 itapatiwa misaada ya jumla ya dola milioni 4. Miradi hii inahusu maandalizi ya walei, waseminari, watawa, shughuli za kitume, uchungaji kwa wafungwa na kwa vijana. Katika hiyo miradi, upo pia ule wa ujenzi wa makanisa ya Equador yaliyoharibiwa na tetemeko la ardhi mwezi Aprili mwaka huu 2016.

Eusebius L. Elizondo, Askofu msaidizi wa Seattle na Mwenyekiti wa kamati ya Baraza la maaskofu Marekani kwa ajili ya Kanisa Amerika ya kusini anasema kwamba: shughuli za kichungaji na elimu vinapaswa kupatikana kwa wote, lakini kwa walio wengi Amerika ya kusini hawapati huduma hizo kwa sababu za kigeografia au kiuchumi. Misaada hiyo inapeleka imani na matumaini kwa wale walio mbali na wenye kuhitaji. Ni misaada inayofanikishwa kwa ukarimu wa waamini wakatoliki nchini Marekani. Kwa miaka ya karibuni, misaada mingi ilielekezwa katika kuijenga upya Haiti baada ya tetemeko la mwaka 2010, na mingine nchini Ufilipini.

Na Padre Celestine Nyanda

Idhaa ya Kiswahili, Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.