2016-12-05 07:31:00

Huruma na amani katika maisha ya mwanadamu!


Huruma na amani, huu ni mwaliko  wa baba Mtakatifu Francisko,  kwa watu wote wenye mapenzi mema, ili  kupata  kutualika  kuishi  huruma  na amani, na mwaliko huu unakuja tu  mara baada ya hitimisho la mwaka wa huruma ya Mungu. Mwaliko huu  wa baba mtakatifu  umeletwa  kwetu  na barua yake ya kitume  ijulikanayo “Misericordia et misera” yaani  "Huruma na amani". Neno huruma na amani  kama  ilivyotumiwa na  Baba Mtakatifu, ni neno  lilokwisha tumiwa  tena  na Mtakatifu Agustino  alipokuwa akioanisha  maneno ya Yesu  alipokutana na Yule mwanamke  mzinzi ( Yn 8:11). Na hapa  Baba mtakatifu anatuambia tendo la Yesu kumsamehe yule mwanamke mzinzi ni jambo la upendo  wa Mungu,  katika kuwafikia  hata wadhambi  na wenye kutubu, na hii  ni huruma katika uhalisia wake, anasema baba Mtakatifu.

Baba Mtakatifu  katika waraka huu wa kitume  anaendelea kunukuu   kifungu cha Injili chenye kumsamehe yule mwanamke mzinzi, kwani kifungu hiki   kinasimama kama alama  ya huruma ya Mungu katika msamaha.   Jambo ambalo  lilionekana sana  katika maadhimisho ya  mwaka mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu,  ambapo maadhimisho yake  yataendelea  kutuweka wapya na wenye upendo katika jamii  zetu  na hivyo kutuwezesha  kutembea  katika upendo  na msamaha , kama yule mwanamke  alivyoambiwa na Yesu,  nenda na kuanzia sasa usitende dhambi tena.

Baba Mtakatifu katika waraka wake huu wa kitume,  Huruma na amani  anaelezea pia na kusisistizia  umuhimu wa msamaha, na anasema  kila  Injili  imejaa msamaha  kama alama ya upendo  na huruma  ya Mungu kwa mwanadamu.  Ni katika  utajiri huu  wa huruma ya Kimungu, Yesu anaalikwa  kwenye chakula katika nyumba ya mfarisayo  na hapo anajitokeza mwanamke  ambaye kila mmoja alimfahamu kuwa ni mzinzi, ambapo mwanamke huyu anamkaribia Yesu na anaosha miguu ya Yesu  kwa machozi yake na kukausha miguu ya Yesu kwa nywele zake, na ndipo Yesu kwa kuwaangalia  wale Mafarisayo, akamwambie Yule mwanamke, dhambi zako zimesamehewa.

Msamaha huu haukuishia hapa tu, bali Baba Mtakatifu anaendelea kusema , msamaha wa Yesu uliendelea hadi nyakati za mwisho pale Msalabani,  Yesu alipotamka maneno  haya ya msamaha,  baba uwasamehe kwani hawajui watendalo. Na msamaha huu unaendelea hadi sasa.  Sasa ni  sisi kuupokea, kuuishi na kumshukuru Mungu daima. Baba Mtakatifu anatuambia huruma ya Mungu haina mwisho,  wala haina mipaka, anasema huruma hii ipo kizazi hata kizazi na inaendelea kuwepo daima hasa kwa wale wanaomtumainia  Mungu kama muumba wao bila kuchoka.

Baba Mtakatifu pia anatuelekeza  kujifunza  furaha  itokanayo na msamaha , kwani furaha hii ni chanzo  cha upendo wa Mungu  na upendo huu unatusaidia  kuondokana  na ubaguzi,  pamoja na uchoyo  na hivyo kutufanya kuwa  vyombo vya huruma ya Mungu. Anatuasa  kuwa ili kupata furaha  nafsini mwetu  yatupasa kuondokana na  utamaduni  uliokandamizwa na  teknolojia , uchungu na upweke, na badala yake yafaa kujipa  matumaini na furaha ya kweli, na hii  ni furaha itokanayo na moyo wenye huruma na hapa ndipo tutakapopata kuungana na maneno ya matakatifu Paulo yasemayo;  siku zote,  tena nasema siku zote  furahini  katika Bwana. Ndugu yangu msikilizaji, Mwaka  Mtakatifu wa Jubilee ya huruma ya Mungu , umeeisha na huu ukiwa ni mwaliko  wa kutufanya tuangalie  mbele katika  furaha, katika uaminifu na katika mwonekano mpya  na huku tukijichotea  utajiri  wa huruma na amani.

Kutoka katika Studio za Radio Vatican ni mimi Pd. Agapiti Amani, ALCP.OSS.








All the contents on this site are copyrighted ©.