2016-11-15 07:21:00

Endeleeni kuwa ni vyombo na mashuhuda wa huruma ya Mungu!


Ndugu yangu msikilizaji wa Radio Vatican, katika Maandiko Matakatifu Yesu anatuambia, tufanyapo sherehe  au karamu,  yatupasa kuwaalika; maaskini , vilema, na hata wasiojiweza (Lk 14:13) kwa mtazamo huu kila mkristo anapaswa kutambua utume wake katika kuwajali maskini na wasiojiweza. Yesu ameshatuonyesha njia, hasa pale alipoanza utume wake kwa maneno haya: Roho wa Bwana yuu juu yangu, kwani amenipaka mafuta  kuwahubiria maskini Habari Njema,  wafungwa kufunguliwa kwao, kuwatangazia vipofu kuwa wanaweza kuona tena, kuwaweka huru wanaonewa na kutangaza mwaka wa bwana uliokubalika (Lk 18:19). Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu, yametuwezesha kuwaona na kuwajali maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kwa kutambua kwamba, maskini ni lengo, amana na utajiri wa Kanisa kama anavyokaza kusema Baba Mtakatifu Francisko.

Mtakatifu Francisko wa Assisi aliwahi kusema   ‘Lengo  la kuishi kwangu  ni kuishi kama Yesu  anavyoishi na kuhubiri kama Yesu anavyohubiri” matamanio haya  yanatakiwa yatutafakarishe sana,  tena tutafakari tukitambua kuwa Yesu ameshatupa njia, namana ya kuishi na namna kuhubiri. Hivyo kwa mifano na matedo ya Yesu tuwafikie sasa wale wote wanaoteseka , labda kwa njaa, vita, kukosa haki, kukosa elimu bora zaidi, wagonjwa, vilema, waliokataliwa na waliokosa matumaini.  Kwani ni katika kuwafikia watu hawa na kuwatangazia Habari Njema watapata kushiba  furaha nafsini mwao  na watapata uponyaji wa kimungu nafsini mwao. Kwa maneno mengine, tunasukumwa na Mama Kanisa kuendelea kumwilisha imani katika matendo ya huruma: kiroho na kimwili kama ushuhuda wa imani yetu kwa Kristo na Kanisa lake! Ikumbukwe kwamba, imani bila matendo, hiyo imekuwa na wala haina mvuto wala mashiko kwa watu!

Baba  Mtakatifu Francisko,  katika Waraka wake wa kitume Furaha ya Injili  anatuambia, kila mkristo na kila jamii inaitwa kuwa dhana ya kimungu  katika kuwahudumia na kuwasaidia maskini , na zaidi kuhakikisha kuwa wanakuwa sehemu ya jamii. Pia anaendelea kusema  kazi ya upendo ielekeayo kwa jirani zetu ni mojawapo ya ukamilifu  wa maonyesho  ya ndani ya neema ya kiroho. Wakati huu pia, tukumbuke, ndiyo wakati uliokubalika ambapo Kanisa linaadhimisha  Mwaka Mtakatifu wa Jubilee ya huruma ya Mungu, hivyo, tujitahidi zaidi na zaidi  kuwasogelea na kuwasaidia  maskini na wasiojiweza, na kwa kufanya hivyo  tutajiongezea neema. Hakima ya  biblia inatuambua;  yeyote aliyemkarimu kwa maskini  anaelekea kwa Bwana  na Bwana atayazawadia matendo yake c( Methali  19:17).

Ndugu zangu, tuadhimishapo mwaka mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu,  tumtembelee Yesu katika  maskini, wasiojiweza, wenye njaa, wanyonge,wagonjwa  wahanga wa matetemeko, vita na majanga mengine ya maisha. Kwani kwa kufanya hivi ndiko kumtembelea Yesu kama mwenyewe alivyosema,; Maana nilikuwa na njaa nanyi mkanipa chakula; nilikuwa na kiu nanyi mkanipa maji; nilikuwa mgeni nanyi mkanikaribisha; nilikuwa uchi nanyi  mkanivika, nilikuwa mgonjwa nanyi mkaja kunitazama,  nilikuwa gerezani nanyi mkaja kunitembelea.(Mt 25 :35-36).

Huu ni wito wa kuwajali wengine katika Kristo na pia ni habari njema kwa watu wote. Ni mwaliko wa kuambata na Yesu pia katika Neno na Sakramenti zake, ili kuonja upendo unaobubujika kutoka katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na toba, msamaha na maondoleo ya dhambi yanayobubujika kutoka kwa Kristo chakula cha uzima na Uso wa huruma na upendo wa Mungu kwa binadamu. Neema na baraka za Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu ziendelee kutuambata na kutusindikiza katika maisha, ili kweli tuweze kuwa ni vyombo na mashuhuda wa huruma na upendo wa Mungu kwa watu wa nyakati hizi!

Na Padre Agapito Amani, O.S.S.

Shirika la Mapadre wa Kazi ya Roho Mtakatifu.

Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.