2016-05-03 14:04:00

Sherehe ya Kupaa Bwana Mbinguni!


Amepaa mbinguni na ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Nasi tumekabidhiwa jukumu la kuendeleza utume na kutangaza ufalme wa Mungu. Tunaongozwa na vifungu vya Maandiko Matakatifu kama ifuatavyo! Ingekuwa vyema kuvipitia vifungu hivi kabla ya kuzama katika tafakari hii, ili uweze kuwa na dira na mwongozo kamili!

I. Mdo 1,1-11

II. Efe. 1,17-23

III. Mt. 28,16-20

Leo tunaadhimisha sherehe ya kanisa, siku 40 baada ya sherehe ya Pasaka - kupaa mbinguni Bwana wetu Yesu Kristo. Mhubiri mmoja asema hakuna awezaye kukaa peke yake mwanamke/mwanamme – kila mmoja anamhitaji mwingine, mwalimu ahitaji wanafunzi n.k. Hivi pia kwa mkristo, leo hii yupo Roho Mtakatifu na akiwepo utamu wa maisha ya kikristo huongezeka. Katika Mt. 1: 23 tunaambiwa kuwa Mungu yu pamoja nasi. Leo tunasikia tamko hilo la Yesu.

Leo Yesu asema nipo pamoja nanyi. Ikumbukwe kuwa sikukuu ya kupaa siyo kumbukumbu ya Kristo kuondoka kati yetu bali ni adhimisho la kumbukumbu ya uwepo wa Kristo kati yetu. Kivipi? Uwepo huu unaoneshwa na kazi zifanywazo na watu wa Mungu - wale ambao daima wanamtii Roho Mtakatifu. Tunaposoma habari ya Kupaa Bwana - katika Yoh. 3:13 - wala hakuna mtu aliyepaa mbinguni ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni yaani Mwana wa Adamu. Katika Efe. 4:10 - naye aliyeshuka ndiye yeye aliyepaa juu sana kupita mbingu zote ili avijaze vitu vyote. Ebr. 4:14 – basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia mbinguni Yesu, mwana wa Mungu, tuyashike tena maungamo yetu.

Padre Raniero Cantalamesa anasema mbingu ikieleweka kama mahali pa pumziko, pa utimilifu wa milele ilifanyika mara tu alipofufuka na kupaa. Mbingu yetu ya kweli ni Kristo mfufuka tunayetumaini kukutana naye na pamoja naye tutakuwa mwili mmoja naye baada ya ufufuko wetu. Na tukisoma habari ya ufufuko na kupaa – katika Yoh. 20:17 - Yesu akamwambia (Mariamu) usinishike kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba, lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie ninapaa kwenda kwa Baba yangu, naye ni baba yenu, kwa Mungu wangu, naye ni Mungu wenu. Na katika Lk. 24:51 - ikawa katika kuwabariki alijitenga nao akachukuliwa juu mbinguni.

Kadiri ya Wainjili Mathayo na Marko - Yesu alipaa mbinguni mwili na roho na tena hilo limetokea siku ile ile ya ufufuko wake, mara moja na hivyo tu. Katika Luka na Kitabu cha Matendo ya Mitume – Yesu alipaa akiwa Yerusalemu na hii ilifanyika siku 40 baada ya ufufuko na muda huo amewatokea mitume mara kadhaa. Lakini lengo la waandishi siyo uhakika katika mandishi bali katika ujumbe wa tukio hilo kuu. Adhimisho la Sikuku hii ya leo laonesha tu mwisho wa muda/wakati ambao Yesu bado alihusiana kwa macho na wanafunzi wake.

Tunachoambiwa ni kuwa atakuja tena siku ya mwisho– Yoh. 21:22 Yesu akamwambia ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? Wewe unifuate mimi? Hakika masomo yetu ya leo, liturjia yetu ya leo yahimiza ufuasi katika ukweli, kwamba maana halisi ya maisha ya kikristo ipo katika Kristo mwenyewe. Mitume wanahimizwa wakaze mwendo na kuongoa wengi, wakibatiza na kufundisha. Nguvu yao ni Kristo na wao wenyewe. Kinachotokea ni kuwa Yesu aliye na nguvu ya Baba anatoa uwezo huo huo kwa wafuasi wake.

Ufuasi ni mchakato ambao kila mwamini anaelimishwa na kuingizwa katika njia mpya, ni mchakato wa uinjilishaji. Huu ndio mwito uliotolewa na jukumu kuu walilopewa wafuasi wakati wa kupaa Bwana nao wakafanye aliyofanya Bwana, kuendeleza utume wake Bwana. Huu ni wosia wakati wa Kupaa. Katika tukio la kupaa kwake Bwana, hupatikana nguvu kwao wote wamfuatao. Yeye atamani kubaki na watu wake ndio maana asema mimi nipo kati yenu. Hatuachi peke yetu. Yote asemayo yatuachia furaha na amani na maneno hayo bado yanabaki kati yetu. Hata leo tunahitaji uongozi wake Kristo.

Sikukuu ya Kupaa Bwana ni sikukuu ambayo sote tunaitwa kutambua kuwa yule Kristo tumwaminiye amepaa mbinguni na ameketi mkono wa kuume wa Mungu Baba, ametukuzwa na ana mamlaka yote na atakuja tena na ukuu na enzi. Katika tendo hili la kupaa, Yesu alitoa tamko la utume - tena wafanye kwa uaminifu mpaka atakapokuja. Aliwahakikishia mema ya Mungu katika utumishi wao. (Mdo 1,8 -Mt 28,19-20 -Mk 16,15-18). Hili tamko la utume ni lipi? Ushuhuda katika kueneza habari njema mpaka miisho ya dunia katika mataifa yote na kutangaza kwa kila kiumbe hii habari njema ya ufalme wake bila kuwa na mipaka ya utaifa au ukabila.  Huu ndio ujumbe tena unaowekwa mbele yetu tunaposherehekea sikukuu ya kupaa Bwana. Ujumbe huo ni wa Bwana, ndiyo maana anatuahidia Roho Mtakatifu. Peke yetu tutashindwa.

Sherehe hii yathibitisha ukamilifu wa huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka kwa waja wake, changamoto ya kushuhudia huruma na upendo katika maisha ya kila siku, husana mwaka huu, Kanisa linapoadhimisha Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu. Mwana wa Mungu amekamilisha utume wake hapa duniani. Ametufundisha juu ya ufalme wake, ametuaminisha sisi watu wake tuendeleze hilo jukumu, anatutuma sisi tuende sasa ulimwenguni lakini pamoja na Roho wake ili kuwa kweli ni mashuhuda na vyombo vya huruma na upendo wa Mungu. Hakika ni uaminifu mkubwa. Hiyo ndiyo changamoto iliyopo mbele yetu leo  nasi twende tukahubiri hiyo Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wenye mashiko na mvuto!

Tumsifu Yesu Kristo.

Na Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.