2016-01-30 11:57:00

Shuhudieni utajiri unaofumbatwa katika Ekaristi Takatifu!


Askofu Cletus Chandrasiri Perera, mwakilishi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Sri Lanka anasema, maadhimisho ya Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa Jimbo kuu la Cebu, Ufilippini ni fursa ya kuadhimisha, kuabudu, kutafakari na kuzama katika katekesi za kina zinazotolewa wakati huu wa kongamano, ili kuwawezesha waamini kuonja na hatimaye, kushuhudia utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Fumbo la Ekaristi Takatifu, kiini na kilele cha maisha na utume wa Kanisa.

Waamini wanapaswa kutambua umuhimu wa Fumbo la Ekaristi katika maisha yao, tayari kulipatia kipaumbele cha kwanza katika maisha yao ya kila siku, ili kuweza kuipokea na kuimwilisha katika uhalisia wa maisha yao, ili kushuhudia huruma, upendo na furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Wakati huu, Kanisa Katoliki linaungana kwa pamoja kusali, kutafakari na kumwabudu Yesu Kristo ambaye daima yuko kati kati ya watu wake kwa njia ya Neno na Sakramenti, lakini zaidi kwa njia ya maskini, ambao kimsingi ni kiini cha Habari Njema ya Wokovu.

Maadhimisho ya Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu kimataifa yanajikita katika Ibada ya Misa takatifu,Sala, Katekesi, Tafakari, Ibada ya Kuabudu na Maandamano la Ekaristi Takatifu ushuhuda wa imani ya Kanisa katika Fumbo la Ekaristi Takatifu, kielelezo cha uwepo endelevu wa Kristo kati ya waja wake pamoja na mikutano mbali mbali ya kiimani. Inafurahisha kuona kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ameridhia maadhimisho ya Kongamano hili yafanyike nchini Ufilippini, nchi ambayo ina idadi kubwa ya waamini wa Kanisa Katoliki, watu ambao wako moto moto katika ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, ikilinganishwa na nchi nyingine kutoka Barani Asia.

Maadhimisho haya ni mkusanyiko wa waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaoshuhudia umoja na utofauti wao katika imani na upendo. Wote hawa wanaungana kwa pamoja ili kumwomba Kristo Yesu awaongoze na kuwaimarisha katika imani inayoshuhudiwa katika matendo ya huruma: kiroho na kimwili. Ekaristi takatifu ni kiini na hitimisho la maisha na utume wa Kanisa, kama ambavyo wanakaza kusema Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Maadhimisho haya ni wakati muafaka kwa Wakristo kutoka Sri Lanka waliohamia nchini Ufilippini kuweza kukutana na kusali kwa pamoja, ili kushuhudia imani yao katika Fumbo la Ekaristi Takatifu anasema Askofu Cletus Chadrasiri Perera, mwakilishi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Sri Lanka kwenye maadhimisho ya Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa linaloendelea huko Jimbo kuu la Cebu, Ufilippini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.