2015-11-13 06:44:00

Tafakari ya Neno la Mungu Jumapili ya 33 ya Kipindi cha Mwaka B wa Kanisa


Karibu katika tafakari ya Liturujia ya Neno la Mungu, leo tukiwa Dominika ya 33 ya mwaka B wa Kanisa. Masomo yanatualika kutafakari juu ya siku ya mwisho, siku ya hukumu na hivi mwaliko ni kujiandaa mapema, yaani kukaa tayari. Fundisho la Bwana lisemalo anayetaka kunifuata ajikane nafsi yake mwenyewe, abebe msalaba wake anifuate kila siku, laweza kutusaidia kuelewa kuwa, wajibu wa kuokoka ni wa kila siku. Lazima kutimiza mapenzi ya Mungu kila siku ya maisha yetu.

Katika somo la kwanza tunaambiwa juu ya siku ya mwisho yaani siku ya hukumu, siku ya mavuno, siku ambayo kila mmoja wetu atapata dhawabu ya kazi yake ya kumtumikia Mungu na kutimiza mapenzi yake. Nabii Danieli anatangaza hali halisi itakavyokuwa siku ile ya mwisho, yaani kutakuwa na taabu ambayo haijawahi kupata kuonekana lakini kwa wale wote ambao majina yao yatakuwa kwenye kitabu cha mbinguni basi hawa watapata matunda mema ya jasho la kazi yao hapa duniani. Kinyume na hapo ni mateso kwa wale waliojibidiisha katika kuliishi giza la mwovu na ndiyo kukosa uzima wa milele! Mambo haya yanatisha lakini basi yanapoletwa kwetu yanatupa changamoto na tumaini kuwa jasho letu tunalolitoa kwa ajili ya mapendo hapa duniani litazaa matunda hapo baadaye. Ndugu zangu tukumbuke katika kuishi Imani yetu kuna mateso na madhulumu mbalimbali na hivi yatupasa kuyavumilia kwa ajili ya uzima wa milele.

Katika somo la pili tunaendelea kusikia juu ya Kuhani Mkuu Yesu Kristo aliye mkono wa kuume wa Mungu mbinguni. Yuko huko akingojea hata wapinzani wake wawekwe chini ya miguu yake. Harudii tena sadaka yake maana mara moja yatosha kwa ondoleo la dhambi. Kazi yetu ndugu zangu wapendwa ni kushiriki ukuhani wa Agano Jipya kwa upendo na unyenyekevu, yaani Misa Takatifu, kilicho kile cha hazina zote takatifu, yapaswa kuadhimishwa kwa uchaji na nguvu. Tunapaswa kusikiliza mafundisho yake kwa njia ya Neno lake na kujenga tabia ya makusudi katika mambo ya ibada takatifu kwa sifa na utukufu wake.

Mpendwa msikilizaji, Mwinjili Marko katika sura yake ya 13 anakazia ujumbe uleule wa Nabii Danieli, anatangaza hali itakavyokuwa nyakati za mwisho. Kutakuwa na giza, nyota za mbinguni kuanguka na mambo kama hayo. Haya yote ni viashilio tu na hivi siku wala saa hatujui! Kumbe, katika hali kama hiyo mwaliko ni kujitayarisha mapema katika maisha ya kila siku kwa kushiriki hazina zote za kiroho kadiri Mama Kanisa anavyoziratibisha daima. Tulilo nalo kwa hakika ni kwamba Mwana wa Adamu atakuja kuwahukumu wazima na wafu, na yakwamba kuna siku ya mwisho ni hakika, ila ni lini, Baba wa Mbinguni pekee ajua ukweli huo! Pamoja na hilo pia tuna uhakika kwamba waliotenda vema, yaani walioshiriki mateso na msalaba wa Kristo watafutwa machozi yao kwa kitambaa cha mwanga mtakatifu toka mbinguni.

Mpendwa unayenisikiliza, yafaa pia kuwa makini, wakati Injili inaandikwa Marko analenga na kukabili matatizo yaliyokuwepo wakati huo na anayalinganisha na mwisho wa dunia, kumbe umakini katika tafsiri ya Neno la Mungu ni muhimu, maana kuna watu wamejiimarisha katika kutumia maneno haya kutishia watu kwamba mwisho wa dunia uko tayari! Tafadhali ajuaye siku na saa ni Mungu peke yake! Kwamba matatizo yanayozungumzwa katika Injili yako hivi leo katikati yetu si kigezo cha kuweka Neno la Mungu katika mlengo huo wa vitisho! Neno la Mungu ni kwa ajili ya kutupatia faraja tunapoendelea kukabiliana na msalaba wa Bwana katika safari ya kwenda mbinguni. Ninakutakia heri na neema za Kristo mfufuka siku zote za maisha yako tunapoelekea kumaliza mwaka B wa Kanisa.

 

Tumsifu Yesu Kristo na Maria. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.