2015-07-25 11:20:00

Tanzia: tunaskitika kutangaza kifo cha Kardinali William Wakefield Baum


Kardinali Donald Wuerl wa Jimbo Kuu la Washington, kwa huzuni  ametangaza  kifo  cha Kardinali William Wakefield Baum, kilichotokea siku ya Ijumaa 24 Julai 2015 huko Washington

Akitangaza kifo hiki, Kardinali Wuerl, amekiri huzuni yake kubwa ya kuondokewa na mchungaji huyu shupavu katika utumishi wa Kanisa, lakini pia akasema, anamshukuru Mungu kwa  huduma yake, hasa kama Askofu Mkuu wa Jimbo la  Washington,  alilolitumikia kwa kipindi kirefu. Na kwamba , wema, fadhila na kujitolea kwake katika  kuhudumia wito wake kwa Mungu kamwe hazitafuta katika mioyo ya watu. Daima alikuwa ni mtu aliyejazwa na furaha ya kipadre katika kuiishi ahadi yake ya kumtumikia Bwana aliyemwita, katika kazi hiyo, aliyoifanya kwa uaminifu kwa miaka  64 ya maisha yake ya Kipadre. Pia atakumbukwa, mpaka sasa kuwa Kardinali aliyetumikia kwa miaka mingi kuliko Makardinali wote , katika historia ya Baraza la Maaskofu Katoliki la Marekani.

Kardinali  Donald Wuerl wa Washington, ameungana na familia ya Marehemu, marafiki na waamini wote wa jimbo la Washington, kuomba kwa ajili yake,  huruma  ya Mungu, na pia kumtolea Mungu shukurani ,   kwa ukarimu na utulivu wa Marehemu Baum ambaye huduma yake iliweza kugusa mioyo ya wengi katika kipindi chote cha utumishi wake wa  miaka mingi.

Marehemu alizaliwa katika mji wa Dallas (USA), Novemba 21, 1926. Wazazi wake walihamia akiwa bado mtoto,  Kansas City, Missouri, ambako alipata elimu ya msingi katika shule ya Parokia ya Mtakatifu  Petro McKay.

Mwaka 1939 aliingia seminari madogo ya Mtakatifu John ya Kansas City, aliendelea masomo yake katika falsafa na teolojia katika Seminari Kenrick, St Louis na kupadrishwa  Mei 12, 1951.

Baada ya Upadrisho kwa miaka kadhaa alifanya utume wake kama Paroko msaidizi katika Parokia ya Parokia ya Mtakatifu Aloysius  ya Jiji la  Kansas , pia akiwa mwalimu wa  theolojia na historia ya kanisa katika Chuo cha Mtakatifu Theresa. Mwaka 1956 yeye alitumwa na askofu wake Roma, kwa ajili ya kujiendeleza zaidi kielimu hadi kujipatia shahada ya uzamivu  katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Angelicum  mwaka 1958.

Baada ya masomo alirudi Marekani ambako aliendelea na utume jimboni mwake, Kansas City. Na kutokana na mapenzi yake katika kujenga umoja wa Wakristo,aliingia kama mtaalam mshauri katika  kazi ya Mtaguso Mkuu wa II. Pia alishiriki katika mikutano kadhaa  kama Mjumbe wa Tume ya Pamoja ya mikutano ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni na  Kanisa Katoliki kuwa Katibu Mtendaji tangu  1964-1967 wa Kamati ya Kiekuemeni ya  Mambo ya Ndani ya Mkutano wa Kitaifa wa Maaskofu Katoliki ya Marekani(NCCB)  . Katika kipindi hicho, pia jimboni mwake alikuwa Paroko wa Kanisa la Mtakatifu James.

Februari 18, 1970  Papa Paul VI alimteua kuwa  Askofu wa Springfield-Cape Girardeau; naaliwekwa wakfu wa Askofu Aprili 6 ya mwaka huo.   Machi 5, 1973, aliteuliwa Askofu Mkuu wa Washington. Wakati huo huo alikuwa pia Rais wa Tume ya Kiekumeni kwa Mambo ya Ndani ya Baraza la Maaskofu Katoliki la Marekani.
Papa Yohana Paulo II, alimteua  kujaza nafasi ya Mkuu wa Taasisi ya Kipapa kwa ajili ya  Elimu Katoliki tangu Januari  15 1980 hadi  6 Aprili 1990 alipoteuliwa kuwa Mkuu wa Mahakama ya Kitume ya Kitubio, kazi aliyo ifanya  hadi Novemba 22, 2001. Na alitangazwa katika orodha ya Makardinali katika kikao cha Makardinali cha a Mei 24, 1976, na kuwa Askofu wa Jina wa Parokia ya  S. Croce, iliyoko mtaa wa Flaminia, jiji Roma.

Kwa kifo cha Kardinali William Wakefield Baum, idadi ya Makardinali Imebaki 220, ambao wenye haki ya kupiga kura ni 120 na wasiokuwa na haki ya kupiga kura imebaki 100.

Sasa  tumwombee apate nafasi katika nyumba ya Baba yetu Mbinguni, apumzike kwa amani. 








All the contents on this site are copyrighted ©.