2015-05-15 08:15:00

Wakandarasi fanyeni kazi kwa weledi kwa kuzingatia kanuni na sheria!


Rais Mstaafu wa awamu ya tatu Mhe. Benjamin William Mkapa amewataka Wakandarasi kote nchini kufanya kazi zao kwa weledi na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia Sekta ujenzi ili miradi wanayoisimamia na kuitekeleza iweze kuwa na manufaa kwa taifa. Mhe.Mkapa ameyasema hayo Alhamisi tarehe 14 Mei 2015  Jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa mkutano wa mwaka wa Bodi ya Usajili wa Wakandarasi (CRB) uliowawajumuisha pia wadau wa sekta ya Ujenzi kutoka nchini Malawi na Kenya.

Amesema umakini katika usimamizi wa kazi za wakandarasi na uwepo wa wataalam waliobobea katika sekta ya ujenzi umechangia kwa kiasi kikubwa kasi maendeleo inayotokea sasa nchini Tanzania. Ameeleza kuwa sekta ya ujenzi ndiyo iliyolifikisha taifa hapa kutokana na mchango wake katika Pato la Taifa unaofikia asilimia 14.1 ikifuatiwa na sekta nyingine na kuongeza kuwa ili nchi iweze kuendelea lazima wakandarasi wazalendo wajengewe uwezo ili kuhakikisha kuwa fedha zinazotolewa katika sekta ya ujenzi zinabakia Tanzania na kuwanufaisha wazawa badala ya wageni.

Amesisitiza kuwa uchumi wa Tanzania lazima ubakie mikononi mwa watanzania wenyewe na kutoa wito kwa Serikali kuendelea kutoa kipaumbele kwa wakandarasi wa ndani ili wawe na uwezo wa kujiendeleza na kujitegemea kwa kutengeneza ajira nyingi zaidi na kuiwezesha Tanzania kuwa nchi ya kipato cha kati. Amewataka wakandarasi wa ndani kuendelea kufanya kazi zao kwa kuzingatia weledi, kuzingatia kanuni na taratibu zinazosimamia sekta hiyo ili taaluma yao iendelee kuheshimiwa ndani na nje ya nchi huku akisisitiza umuhimu wa wakandarasi hao na kuungana ili kujenga uwezo wa kushindana na makampuni mengine kutoka nje.

Kwa upande wake,  Waziri wa Ujenzi Mhe.John Magufuri akizungumza wakati wa mkutano huo amesema kuwa ili taifa liweze kupata maendeleo endelevu katika sekta ya ujenzi lazima wataalamu wanaohusika na sekta hiyo wafanye kazi zao kwa kuzingatia kanuni, miiko na sheria zilizowekwa. Amesema taaluma ya uhandisi nchini Tanzania imechangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha miundombinu ya barabara, madaraja, majengo, vivuko mbalimbali na miundombinu mingine muhimu ya kuwarahisishia wananchi huduma bora ya usafiri. Aidha, amesema uwepo wa sheria na 15 inayosimamis sekta hiyo hapa nchini na ongezeko la wakandarasi waliosajiliwa wanaofikia 15,062 kutoka ndani na nje ya nchi, wengi wao wakiwa watanzania linaonyesha maendeleo makubwa yaliyopigwa na sekta hiyo ikilinganishwa na miaka 15 iliyopita.

Amesema Serikali ya awamu ya nne chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete iko katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi ikiwemo miradi mikubwa ya barabara za mzunguko katika jiji la Dar es salaam Barabara, madaraja makubwa, reli na miradi mingine ambayo itaifungua nchi ya Tanzania kitaifa na kimataifa na kuimarisha sekta usafirishaij. Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutoa kipaumbele kwa Wakandarasi wazalendo kote nchini Ili waendelee kunufaika na zabuni mbalimbali zinazotangazwa kote nchini kwa asilimia 45 na kuongeza kuwa malengo yaliyopo ni kufikia ongezeko la asilimia 70 ili uchumi wa sekta ya ujenzi uendelee kubaki nchini Tanzania.

Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wakandarasi Dkt.Ambwene Mwakyusa amesema mkutano huo umeandaliwa na Bodi ya Wakandarasi Tanzania kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Sekta ya ujenzi Chini ya kauli Mbiu isemayo "Changamoto na Mustakabali wa Sekta ya Ujenzi katika Kutimiza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025". Amesema licha ya sekta ya ujenzi nchini Tanzania kuendelea kupata mafanikio nchini bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali za kihandisi zikiwemo za mazingira yanayosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi katika kuathiri ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo madaraja na barabara ambazo zimekua zikiathoriwa na mvua.

Amesema wakandarasi wanakabiriwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya ucheleweshwaji wa malipo yao na madeni makubwa wanayoidai Serikali kutokana na miradi waliyofanya katika maeneo mbalimbali nchini. Amefafanua kuwa mkutano huo wa mwaka umehudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya ujenzi kutoka ndani na nje ya Tanzania wakiwemo kutoka Kenya na Malawi pamoja na kampuni mbalimbali zipatazo 95 zinazojihusisha na ujenzi zilizoshiriki kuonesha namna zinavyotekeleza majukumu yao, kuonesha bidhaa wanazozalisha,vifaa vya ujenzi na mitambo mbalimbali inayotumika katika ujenzi hapa nchini.

Katika hatua nyingine Bodi ya Usajili wa Wakandarasi imewaapisha Wahandisi waliohudhuria mkutano huo ili kulinda weledi na ufanisi wa kazi zao na kuwakumbusha wahandisi hao kutumia utaalam wao katika kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viwango ,sheria na taratibu zilizowekwa. Aidha Bodi ya Usajili wa Wakandarasi imetoa zawadi mbalimbali ikiwemo vyeti kama motisha ya kutambua mchango wa makampuni na wakandarasi wazalendo waliofsnya vizuri katika sekta hiyo nchini Tanzania kwa kuzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo suala la uzingatiaji wa Afya na usalama mahali pa ujenzi,viwango vya ubora wa ujenzi na vifaa wanavyotumia katika miradi mbalimbali wanayotekeleza.


 








All the contents on this site are copyrighted ©.