2015-04-16 15:27:00

Zingatieni majadiliano ya kidini, mafao ya wengi na teteeni maskini


Baba Mtakatifu Francisko mapema Alhamisi hii,  alikutana na kundi la Maaskofu wanaounda Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Kenya . Maaskofu hao wako katika hija yao ya kitume katika Kaburi la Mtakatifu Petro na  Kiti Kitakatifu,tangu siku ya Jumatatu ya wiki hii na wanaikamilisha Ijumaa hii tarehe 17 Aprili 2015.

Akiongoza Msafara huo, Kardinali John Njue, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Nairobi, kwa niaba ya  wenzake, alitoa hutoba fupi kwa Papa, kama ujumbe wao kwa Papa na kwa kanisa la Ulimwengu kwa ujumla,  juu ya hali ya Kanisa katika taifa lao la Kenya. Na wamerudia kuonyesha ushirikiano wao kupitia fursa mbalimbali zenye kuimarisha muungano wa Kanisa Katoliki la Kenya katika umoja na Halifa wa Mtume Petro. Aidha Kardinali  aliwasilisha salaam za matashi mema kwa  Papa kwa niaba ya Mapadre wote , watawa wake kwa waume na waamini walei wa Kenya.Papa kwa moyo wa upendo na wa kibaba aliwapokea kwa ukarimu wote na kuwahakikishia sala zake na ukaribu wake  kiroho. 

Papa Francisco katika hotuba yake kwa Maaskofu wa Kenya , amegusia sehemu mbalimbali za utendaji wa  Maaskofu, hasa akimtaka kila Askofu,  kupanda mbegu bora ya miito kwa waumini wao, wakianzia ndani ya  familia, kama shule ya kwanza ya malezi katika ubinadamu wote, na katika hitaji la vijana kutoa jibu katika miito ya kanisa. Kwa sababu hii, Papa Francisco anasema ni  muhimu kwamba , nia njema  za vijana wanaotaka kujiunga na seminari, hamu  na bidii yao,  inapaswa kusindikizwa na malezi thabiti yenye kutambua ubinadamu kwa kina , kiroho, kielimu, na huduma za kichungaji mbalimbali.  Wakati huohuo Papa ameonyesha kutambua changamoto zinazowakabili katika kuimarisha juhudi hizi ,ndani ya majimbo yao , na hivyo akahimiza yote mawili kuimarisha juhudi kama Askofu binafsi na pia katika ujumla wao ili kwamba, mbegu wanayoipanda katika moyo wa Kijana iweze kuchipua kikamilifu kwa wito wa  Bwana katika daraja la Upadre.

Kwa maoni hayo Papa alisisitiza kuwa , kila mmoja wao kama Askofu,  anaitwa kuwa mchungaji na kama  baba.  Na hivyo aliwataka wawe karibu na Mapadre wao.  Amesema , Mapadre wanahitaji  uongozi ulio wazi na thabiti lakini wakati huohuo pia kuongozwa na huruma na hekima. Kama Maaskofu, ni lazima daima kutazama mfano wa Yesu, ambaye  binafsi  aliwatumikia mitume, na alitumia muda mwingi kukaa pamoja na mitume kubarizi nao.  Vivyo hivyo wao Maaskofu, ni lazima wajitahidi kukaa na Mapadre wao,  kuwasikiliza, kujua matatizo yao na mahitaji yao. Na pia kuwapa msaada wa kiroho  unaohitajika katika  kuwadumisha kama  Mapadre katika uaminifu wa ahadi walizotoa na kuimarisha juhudi yao za kawaida  katika kuujenga ufalme wa Mungu kwa  Kenya.

Aidha Papa aliurejea  Mwaka huu wa Watawa, akisema , anawakumbatia, ndani ya moyo wake, wote walio yatolea maisha yao sadaka katika kulitumikia kanisa , watawa wake kwa waume, walio yakataa ya dunia kwa ajili ya ufalme wa Mungu , ambao huleta baraka nyingi kwa Kanisa na kwa  jamii ya Kenya.  Papa aliwaomba Maaskofu, wafikishe salaam zake za upendo  na matumaini yake kwao wote, kwamba katika mwaka huu wa Maisha yaliyowekwa wakfu, wanaweza kuushangilia kwa  shangwe na ushujaa wa kumweka kwa Kristo, kuwa ngao ya maisha yao. Na kwamba wanaitwa  na  Kanisa kuonyesha matumaini na  ushuhuda  wa manufaa kwa upya wa maisha, yaliyo ahidiwa na Kristo katika Injili. Katika suala hili, Papa anasema, Kanisa lazima hasa kwa wale walio katika nafasi za uongozi na mamlaka, kusisitiza  juu ya kanuni za maadili yenye kukuza manufaa ya umma na yenye kujenga ya jamii bora kwa ujumla. Katika kutimiza dhamira yake ya kitume, Kanisa lazima lichukue msimamo wake wa kinabii, kwa ajili ya utetezi kwa  walio maskini na wale wanaogandamizwa na madhulumu ya rushwa zote na matumizi mabaya ya madaraka. Askofu anatakiwa kuwa mfano bora katika kuwatetea wanyonge.

Papa amewataka Maaskofu kutokuwa na woga katika  hilo bali wasimame imara katika kutoa sauti ya kinabii! Na wahakikishe  hekima ya Kanisa, inatambulika hasa kupitia mafundisho yake ya kijamii, na katika kuyabeba  maisha ya watu wa kawaida wa Kenya. Papa alieleza na kuwahimiza Maaskofu kuimarisha viungo vyao katika huduma na ushirikiano walionao na taasisi za kidini katika taifa lao la Kenya, ili kupitia juhudi hizo , Jina la Mungu liweze kusifiwa na kutukuzwa kwa matendo ya huruma na upatanifu.  Papa ameeleza na kutoa shukurani zake za dhati kwa wafanyakazi  wote wanaotenda kwa unyenyekevu na ari  kubwa  katika  taasisi za Kanisa, kwa ajili ya huduma katika yote  mawili kiroho na kimwili, hasa kwa watu wahitaji zaidi.  Aidha ameonyesha kufurahishwa na jinsi Kanisa linavyo changia na kuendesha shughuli zake katika maisha ya kijamii  kwa manufaa ya wote, kupitia safu mbalimbali kama shule, taasisi, vyuo vikuu, zahanati, hospitali, nyumba kwa ajili ya wagonjwa na wazee, yatima na mashirika ya kijamii, ambamo Watawa hutoa mchango wao mkubwa kwa ustawi wa taifa zima. Na pia kwa ajili ya sifa ya  matendo endelevu  katika  maisha ya sala na ibada, mihadhara, nyumba za watawa na monesteri..

Aidha Papa analihimiza Kanisa nchini Kenya daima kuuishi ukweli wa utume wake,  kama chombo cha maridhiano, haki na amani. Katika uaminifu wa urithi mzima wa imani na mafundisho ya maadili ya Kanisa, waweze  kuimarisha dhamira yao ya kufanya kazi na viongozi wengine , Wakristo na wasio-Wakristo  katika usawa wa kukuza amani na haki katika nchi yao kwa njia ya mazungumzo, udugu na urafiki. Kwa njia hii watakuwa na uwezo wa kujenga  umoja zaidi na ujasiri wa  kukataa  vurugu zote, hasa zinazo fanywa kwa kutumia jina la Mungu. Hili litaweza kuwapatia dhamana thabiti  zaidi, kutoka kwa wananchi wote.  Kwa maoni hayo Papa amesema, yuko pamoja nao ,katika sala za kuwaombea wote waliouawa katika utendaji wa kigaidi  au uhasama wa kikabila au kidini katika nchi ya Kenya, na maeneo mengine ya bara la Afrika.  Na kwa namna ya kipekee aliwakumbuka kafara wa ugaidi katika Chuo Kikuu cha Garissa.  Wote amewaombea kupumzika kwa amani na wapendwa wao wapate faraja za Bwana na wote wanaofanya ukatili huo , waweze kuwa na hisia za ubinadamu nakuomba Huruma ya Mungu.

Papa pia, amewatia moyo Maaskofu kwa ajili ya huduma yao ya kichungaji kwa familia , hasa katika mtazamo kwamba, mwaka huu ambamo kutakuwa na  Sinodi ya kawaida ya Maaskofu,  kujadili suala ya maisha ya kichungaji kwa familia katika  maoni ya uinjilishaji mpya.  Papa ameonyesha imani yake kwa maaskofu kwamba, wataendelea  kusaidia familia kubaki imara katika maisha ya ndoa , licha ya wimbi la sasa la  ndoa kuvunjwa, ukafiri, madawa ya kulevya au vurugu. Amehimiza mafundisho thabiti yatolewa kwa wale wote wanaotaka kufunga ndoa , na pia kwa wale wanaopenda kujiunga katika maisha ya kitawa au Upadre. Papa anasema wote wanahitaji  kufundisha ukweli kuokoa  wa Injili ya Maisha.

Na hatimaye,  Papa ameomba  Jubilee ijao wa Huruma ya Mungu uwe ni wakati wa kutafuta msamaha kwa Bwana, wakati wa uponyaji, uongofu, na neema  kwa Kanisa la  zima nchini  Kenya, na Afrika kwa ujumla.  Na ameweka Maaskofu na Kanisa zima,  chini ya Maombezi ya Mama Bikira Maria, Mama wa Kanisa, na kwa upendo mkubwa  aliwapatia wote Baraka zake za Kitume. 








All the contents on this site are copyrighted ©.