Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema mkoa wa Mbeya unaweza kupaa kiuchumi
kama utazingatia fursa za kibiashara ilizonazo na kuwekeza zaidi kwenye viwanda vya
usindikaji mazao ya kilimo na mifugo. Ametoa kauli hiyo Jumatatu, Machi 2, 2015 wakati
akizungumza na viongozi mbalimbali wa mkoa wa Mbeya waliofika kusikiliza majumuisho
ya ziara yake ya siku saba kwenye mkoa huo. Mkutano huo ulifanyika kwenye ukumbi wa
Mkapa, jijini Mbeya.
“Nguvu kubwa mnayo katika biashara hasa kama mtajitahidi
kutumia vema fursa kubwa ya uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani kwenye mazao
ya kilimo na mifugo mliyonayo,”alisema. Waziri Mkuu alisema mkoa wa Mbeya katika msimu
wa 2013/2014 umeweza kuzalisha tani 4,159,907 za nafaka na kuuwezesha kuwa na ziada
ya chakula ya tani 3,347,680.
Hata hivyo, Waziri Mkuu alisema mkoa wa Mbeya
bado una fursa nzuri ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara na unaweza
kuiwezesha kama nchi kuuza chakula katika masoko ya Afrika na Afrika ya Mashariki
kama watajipanga vizuri.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu aliwapongeza viongozi
hao kwa kuuwezesha mkoa wa Mbeya kutoa mchango mkubwa katika Pato la Taifa. “Katika
taarifa ya mkoa, nimeelezwa kuwa mwaka 2013, mkoa huu ulichangia shilingi trilioni
3.951 na hivyo kushika nafasi ya tatu kati ya mikoa yote nchini ikitanguliwa na mikoa
ya Dar es Salaam na Mwanza.”
Alisema kutokana na ukuaji wa kasi wa idadi ya
watu ambao ni asilimia 2.7, mtu akichukua pato hilo la mkoa na kuligawanya kwa idadi
ya watu wa mkoa wa Mbeya anapata wastani wa pato la kila mwananchi kuwa ni sh. 1,420,427.
“Kipato hicho, ni sawa na shilingi 118,369 kwa mwezi au shilingi 3,946 kwa siku sawa
na Dola za Kimarekani (US $) 2.3,” alifafanua.
Waziri Mkuu alibainisha kwamba
mtu akichukua wastani wa pato la kila mwananchi kwa mwaka 2013 na kupanga kwa mikoa
yote, mkoa wa Mbeya unashuka na kushika nafasi ya sita kitaifa. Aliitaja mikoa inayowatangulia
kuwa ni Dar es Salaam sh. 1,990,043/-ambao ni wa kwa kwanza; wa pili ni Iringa (sh.
1,660,532/-); wa tatu ni Arusha (sh. 1,448,782/-); wa nne ni Kilimanjaro (sh. 1,444,882/-);
wa tano ni Ruvuma (sh. 1,438,392/-) na wa sita ni Mbeya (sh. 1,420,427/-).
“Nawashauri
muongeze juhudi za kuipita mikoa hiyo kwa kuwa mna fursa nyingi za kuongeza uzalishaji
hasa katika mazao ya kilimo cha kahawa, kakao, mpunga, mahindi, viazi, pamoja na mazao
ya maliasili kama vile mazao ya misitu, na uvuvi na uchimbaji madini,”.