2015-03-03 09:57:07

Uongozi bora Barani Afrika!


Rais Hifikepunye Pohamba wa Namibia aliyemaliza muda wake ndiye mshindi wa tuzo ya Mo Ibrahim kutokana na uongozi makini kwa wananchi wake. Tuzo hii inaambatana na kitita cha Dolla za Kimarekani Millioni 5. Zawadi hii inatolewa kwa viongozi wa Bara la Afrika ambao wameonesha uongozi bora pamoja na kuboresha hali ya maisha ya wananchi wao wakati walipokuwa madarakani na muda wao ulipowadia wakaachia ngazi na kuendelea na maisha kama kawaida pasi ya kung'angania kwenye madaraka kwa kutaka kupindisha Katiba ya nchi!

Rais Pohamba alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuongoza Namibia kunako mwaka 2004, akapewa tena dhamana hii kunako mwaka 2009 na hivi karibuni, aling'atuka kutoka madarakani na kwa sasa Rais mteule Hage Geingob anatarajiwa kusimikwa rasmi ili kuendeleza mchakato wa uongozi kwa watu wake. Rais Pohamba mwenye umri wa miaka 80 aliteuliwa na Jopo la viongozi wa Afrika kunako mwaka 2014 katika sherehe zilizofanyika Jijini Nairobi.

Tuzo hii ilianzishwa na Bwana Mo Ibrahim kutoka Sudan ili kuwahamasisha viongozi wa Bara la Afrika kuwaongoza watu wao kwa hekima na busara na hatimaye, kung'atuka kutoka madarakani kwa amani na utulivu, huku wakijivunia mafanikio yaliyopatikana chini ya uongozi wao bila ya kung'ang'ania madarakani kana kwamba, hakuna mtu mwingine yeyote nchini mwao anayeweza kusukuma mbele Jahazi la maendeleo ya watu. Itakumbukwa kwamba, kunako mwaka 2007, tuzo hii ilinyakuliwa na Rais mstaafu Joaquim Chisano wa Msumbiji.

Dr. Salim Ahmed Salim kutoka Tanzania aliyewahi kuwa Katibu mkuu wa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika, OAU ndiye Mwenyekiti wa Jopo la majaji wa tuzo ya Mo Ibrahim.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican







All the contents on this site are copyrighted ©.