2015-03-03 11:19:16

Miaka 50 ya Uaskofu si haba!


Hivi karibuni, Askofu mkuu mstaafu James Odongo wa Jimbo kuu la Tororo, Uganda aliadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu alipowekwa wakfu kuwa Askofu, sherehe ambazo zimehudhuriwa na umati mkubwa wa Familia ya Mungu nchini Uganda. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu mstaafu Odongo ni Askofu wa nne mzalendo kutoka Uganda kupewa dhamana ya kuliongoza Kanisa kama Askofu.

Askofu mkuu mstaafu Odongo ni matunda ya maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, kumbe katika maisha na utume wake, alipenda kuhakikisha kwamba, waamini walei wanapewa nafasi kubwa zaidi katika maisha na utume wa Kanisa. Ni kati ya Mababa wa Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo, shule ya Neno la Mungu, maisha ya Kisakramenti na matendo ya huruma. Ni Kiongozi wa Kanisa ambaye ameyakita maisha yake katika: Fumbo la Ekaristi, Neno la Mungu na Ibada kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa.

Katika maisha yake, amejitahidi kuwa kweli ni Baba mwenye huruma na mapendo, aliyetaka kuhakikisha kwamba, waamini wa Jimbo Kuu la Tororo wanajenga na kudumisha mshikamano wa udugu na upendo ili kuondokana na ukabila usiokuwa na mvuto wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya watu.

Askofu mkuu mstaafu anasema, enzi ya ujana wake alikuwa ni moto wa kuotea mbali si tu katika ujenzi wa Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo miongoni mwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana, bali pia alikuwa anatandaza kabumbu ile mbaya! Makali yake anasema, hata Kardinali Francis Arinze anayatambua. Ni kiongozi ambaye alitoa kipaumbele cha kwanza kwa maendeleo na ustawi wa Familia ya Mungu AMECEA na leo hii, Kanisa linafurahia matunda ya mchango wake!







All the contents on this site are copyrighted ©.