2015-03-03 15:03:10

Ekaristi Takatifu ni Fumbo la Umoja


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake, Jumatano tarehe 4 Machi 2015 anatarajiwa kukutana na kuzungumza na Maaskofu kutoka katika nchi 35 wanaohudhuria Kongamano la 38 unaohusu tasahufi ya maisha ya kiroho ya Chama cha Wafokolari linaloongozwa na kauli mbiu "Ekaristi Takatifu ni Fumbo la Umoja". Kongamano hili linaratibiwa na Kardinali Francis Xavier Kriengsak Kovithavanij, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Bangkok, Thailand.

Taarifa inaonesha kwamba, hili ni kundi la Maaskofu kutoka sehemu mbali mbaloi za dunia ambazo kwa miaka ya hivi karibuni zimetikiswa na kuguswa na madhulumu, nyanyaso na maonevu ya kidini. Ni nchi ambazo, vita bado inaendelea kuonesha makucha yake na kwamba, kuna umati mkubwa wa watu ambao wanaendelea kuteseka kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Lakini, pia ni Maaskofu ambao wanatoka katika nchi zenye matumaini na imani thabiti. Maaskofu katika Kongamano hili ambalo limeanza Jumanne tarehe 3 Machi linatarajiwa kufungwa rasmi hapo tarehe 6 Machi 2015.

Maaskofu wanashirikishana mang'amuzi, matumaini na mikakati mbali mbali ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Familia ya Mungu katika maeneo yao. Lengo ni kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene kama sehemu ya utekelezaji wa dhamana ya Uinjilishaji mpya, inayovaliwa njuga na Mama Kanisa kwa wakati huu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.