2015-02-18 08:49:39

Upendo


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake wa Kwaresima kwa mwaka huu, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kukabiliana kikamilifu na changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu. RealAudioMP3
Baba Mtakatifu anawataka waamini kujifunga kibwebwe ili kupambana dhidi ya tabia ya uchoyo na ubinafsi, inayoendelea kujitanua kiasi hata cha kupata mwelekeo wa kimataifa, kwa kuwabeza watu wanaoteseka, uwepo wa ukosefu wa misingi ya haki na amani.
Ni tabia inayotaka kumwondoa Mwenyezi Mungu katika maisha ya watu na kusahau kwamba, Mungu ameupenda ulimwengu kiasi hata cha kumtoa Mwanaye wa pekee kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, ni dhamana na jukumu la Kanisa kuhakikisha kwamba, linaacha malango wazi ya mawasiliano kati ya Mwenyezi Mungu na binadamu, kwa njia ya mchakato wa utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu, Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa, Ushuhuda wa imani tendaji inayomwilishwa katika matendo ya huruma. Hata pale ulimwengu unapotaka kujifungia na hatimaye kufunga lile lango na mawasiliano kati ya Mungu na ulimwengu, Mwenyezi Mungu bado anaendelea kuonesha jitihada za kumtafuta mwanadamu ili aweze kumwonjesha huruma na upendo wake usiokuwa na kifani.
Kwaresima anasema Baba Mtakatifu, ni kipindi cha mabadiliko, toba na wongofu wa ndani, unaowawezesha Watu wa Mungu kushinda kishawishi cha utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu na badala yake, kujenga utandawazi wa upendo, udugu na mshikamano wa dhati.
Baba Mtakatifu anafafanua mambo mambo makuu matatu yanayopaswa kufanyiwa kazi na Watu wa Mungu ili kuhakikisha kwamba, wanataabikiana na kusumbukiana katika shida na mahangaiko yao, kwani kama kiungo kimoja kinateseka, basi viungo vingine vyote vinateseka pamoja nacho. Huu ni wajibu ambao kwanza kabisa unapaswa kutekelezwa na Kanisa la kiulimwengu, kwa kuonesha umoja wa watakatifu na katika mambo matakatifu.
Upendo wa Mungu ni silaha madhubuti dhidi ya utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu, ushuhuda wa upendo unaoneshwa na Mama Kanisa kwanza kabisa katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Hapa waamini wanakirimiwa neema na baraka ya kuwa ni Ekaristi, yaani Mkate uliomegwa kwa ajili ya jirani zao na hivyo kuwa kweli ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa, hapa ubinafsi na uchoyo havina nafasi tena!
Hatua ya pili katika hija hii ya kipindi cha Kwaresima ni changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika dhamana na maisha ya Parokia na Jumuiya zake, kwa kuhakikisha kwamba, Kanisa linalosafiri hapa duniani, linaunganika na lile Kanisa la Mbinguni, kwa kuungana pamoja katika sala, huduma na mafao ya wengi, ili kuonesha utukufu wa Mungu. Waamini pia wanapaswa kutambua dhamana na wito wao wa kimissionari, kwa kuvuka mipaka inayowahusianisha na jamii inayowazunguka, tayari kwenda kuwatangazia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, Habari Njema ya Wokovu.
Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, Parokia na Jumuiya za Kiparokia ndipo mahali muafaka ambapo Kanisa linaonesha kwa namna ya pekee kabisa utambulisho wake, kwa kuwa ni visiwa vya huruma na upendo wa Mungu kati ya watu wanaozungukwa na bahari kubwa ya utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu.
Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema akisema “imarisheni mioyo yenu”. Ni jambo la kutisha kabisa kuona jisni ambavyo mwanadamu hana nguvu ya kupambana na mateso pamoja na mahangaiko ya binadamu yanayoendelea kujitokeza kila siku siku ya maisha; lakini wanaweza kuyashinda yote haya kwa njia ya mshikamano wa sala za wengi. Kutokana na changamoto hii, Baba Mtakatifu anawaalika kuungana na Kanisa zima, kwa ajili ya kumtolea Mwenyezi Mungu sala na maombi kwa musa wa masaa 24, tukio litakalofanyika tarehe 13 na tarehe 14 Machi 2015.
Licha yak usali, waamini wanahamasishwa kuonesha ushuhuda wa upendo kwa njia ya matendo ya huruma kama kielelezo makini cha ushiriki wao katika kuwashirikisha wengine upendo unaoguswa na mahangaiko ya jirani. Baba Mtakatifu anasema kwamba, haiwezekani kwa mwamini kujiokoa peke yake, kwani hiki ni kishawishi cha shetani. Hapa kunahitajika kama anavyosema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI mchakato wa majiundo ya moyo unaotambua umaskini wake na hivyo kujisadaka kwa ajili ya wengine.
Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha ujumbe wake wa Kwaresima kwa Mwaka 2015 kwa kumwomba Yesu Kristo ili aweze kuifanya mioyo ya waamini kufanana na Moyo wake Mtakatifu, unaosheheni nguvu na huruma; moyo unaokesha na kuonesha ukarimu, ili usije ukatumbukia katika utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu. Kwa ujumbe huu, Baba Mtakatifu anawatakia waamini na watu wote wenye mapenzi mema Kwaresima yenye mabadiliko na mafanikio makuu katika maisha ya kiroho!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.