Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake wa Kwaresima kwa mwaka huu, anawaalika
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kukabiliana kikamilifu na changamoto zinazojitokeza
katika ulimwengu wa utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu. Baba Mtakatifu
anawataka waamini kujifunga kibwebwe ili kupambana dhidi ya tabia ya uchoyo na ubinafsi,
inayoendelea kujitanua kiasi hata cha kupata mwelekeo wa kimataifa, kwa kuwabeza watu
wanaoteseka, uwepo wa ukosefu wa misingi ya haki na amani. Ni tabia inayotaka
kumwondoa Mwenyezi Mungu katika maisha ya watu na kusahau kwamba, Mungu ameupenda
ulimwengu kiasi hata cha kumtoa Mwanaye wa pekee kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu
kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba,
ni dhamana na jukumu la Kanisa kuhakikisha kwamba, linaacha malango wazi ya mawasiliano
kati ya Mwenyezi Mungu na binadamu, kwa njia ya mchakato wa utangazaji wa Habari Njema
ya Wokovu, Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa, Ushuhuda wa imani tendaji inayomwilishwa
katika matendo ya huruma. Hata pale ulimwengu unapotaka kujifungia na hatimaye kufunga
lile lango na mawasiliano kati ya Mungu na ulimwengu, Mwenyezi Mungu bado anaendelea
kuonesha jitihada za kumtafuta mwanadamu ili aweze kumwonjesha huruma na upendo wake
usiokuwa na kifani. Kwaresima anasema Baba Mtakatifu, ni kipindi cha mabadiliko,
toba na wongofu wa ndani, unaowawezesha Watu wa Mungu kushinda kishawishi cha utandawazi
usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu na badala yake, kujenga utandawazi wa
upendo, udugu na mshikamano wa dhati. Baba Mtakatifu anafafanua mambo mambo makuu
matatu yanayopaswa kufanyiwa kazi na Watu wa Mungu ili kuhakikisha kwamba, wanataabikiana
na kusumbukiana katika shida na mahangaiko yao, kwani kama kiungo kimoja kinateseka,
basi viungo vingine vyote vinateseka pamoja nacho. Huu ni wajibu ambao kwanza kabisa
unapaswa kutekelezwa na Kanisa la kiulimwengu, kwa kuonesha umoja wa watakatifu na
katika mambo matakatifu. Upendo wa Mungu ni silaha madhubuti dhidi ya utandawazi
usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu, ushuhuda wa upendo unaoneshwa na Mama
Kanisa kwanza kabisa katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Hapa waamini
wanakirimiwa neema na baraka ya kuwa ni Ekaristi, yaani Mkate uliomegwa kwa ajili
ya jirani zao na hivyo kuwa kweli ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa,
hapa ubinafsi na uchoyo havina nafasi tena! Hatua ya pili katika hija hii ya kipindi
cha Kwaresima ni changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika dhamana
na maisha ya Parokia na Jumuiya zake, kwa kuhakikisha kwamba, Kanisa linalosafiri
hapa duniani, linaunganika na lile Kanisa la Mbinguni, kwa kuungana pamoja katika
sala, huduma na mafao ya wengi, ili kuonesha utukufu wa Mungu. Waamini pia wanapaswa
kutambua dhamana na wito wao wa kimissionari, kwa kuvuka mipaka inayowahusianisha
na jamii inayowazunguka, tayari kwenda kuwatangazia maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa jamii, Habari Njema ya Wokovu. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko
kwamba, Parokia na Jumuiya za Kiparokia ndipo mahali muafaka ambapo Kanisa linaonesha
kwa namna ya pekee kabisa utambulisho wake, kwa kuwa ni visiwa vya huruma na upendo
wa Mungu kati ya watu wanaozungukwa na bahari kubwa ya utandawazi usiojali wala kuguswa
na mahangaiko ya watu. Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi
mema akisema “imarisheni mioyo yenu”. Ni jambo la kutisha kabisa kuona jisni ambavyo
mwanadamu hana nguvu ya kupambana na mateso pamoja na mahangaiko ya binadamu yanayoendelea
kujitokeza kila siku siku ya maisha; lakini wanaweza kuyashinda yote haya kwa njia
ya mshikamano wa sala za wengi. Kutokana na changamoto hii, Baba Mtakatifu anawaalika
kuungana na Kanisa zima, kwa ajili ya kumtolea Mwenyezi Mungu sala na maombi kwa musa
wa masaa 24, tukio litakalofanyika tarehe 13 na tarehe 14 Machi 2015. Licha yak
usali, waamini wanahamasishwa kuonesha ushuhuda wa upendo kwa njia ya matendo ya huruma
kama kielelezo makini cha ushiriki wao katika kuwashirikisha wengine upendo unaoguswa
na mahangaiko ya jirani. Baba Mtakatifu anasema kwamba, haiwezekani kwa mwamini kujiokoa
peke yake, kwani hiki ni kishawishi cha shetani. Hapa kunahitajika kama anavyosema
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI mchakato wa majiundo ya moyo unaotambua umaskini
wake na hivyo kujisadaka kwa ajili ya wengine. Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha
ujumbe wake wa Kwaresima kwa Mwaka 2015 kwa kumwomba Yesu Kristo ili aweze kuifanya
mioyo ya waamini kufanana na Moyo wake Mtakatifu, unaosheheni nguvu na huruma; moyo
unaokesha na kuonesha ukarimu, ili usije ukatumbukia katika utandawazi usiojali wala
kuguswa na mahangaiko ya watu. Kwa ujumbe huu, Baba Mtakatifu anawatakia waamini na
watu wote wenye mapenzi mema Kwaresima yenye mabadiliko na mafanikio makuu katika
maisha ya kiroho! Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya
Radio Vatican.