Askofu mstaafu Magnus Mwalunyungu wa Jimbo la Tunduru-Masasi, Tanzania, amefariki
dunia Alfajiri ya Ijumaa tarehe 13 Februari 2015 katika Hospitali ya Tosamaganga,
iliyoko Jimbo Katoliki la Iringa. Taarifa zinabainisha kwamba, Marehemu Askofu Mwalunyungu
anatarajiwa kuzikwa kwenye Kanisa la Tosamaganga, Jimbo Katoliki la Iringa, Ijumaa,
tarehe 20 Februari 2015. Historia inaonesha kwamba, humu ndimo alimozikwa pia Askofu
Attilio Betramino, huyu alikuwa ni Askofu wa kwanza kabisa wa Jimbo Katoliki Iringa.
Marehemu Askofu Magnus Mwalunyungu alizaliwa kunako tarehe 25 Agosti 1930
huko Iringa. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, akapewa Daraja takatifu
la Upadre kunako tarehe 23 Agosti 1959. Kwa miaka mingi alikuwa ni Gombera wa Seminari
kuu ya Kipalapala, kiongozi ambaye lifahamu kwa kina na mapana historia ya Seminari
ya Kipalapala.
Kunako tarehe 30 Machi 1992, akateuliwa na Baba Mtakatifu Yohane
Paulo II kuwa Askofu wa Jimbo la Tunduru-Masasi na kuwekwa wakfu hapo tarehe 25 Juni
1992. Baada ya kuihudumia Familia ya Mungu Jimboni Tunduru-Masasi, kwa ari na moyo
mkuu, kunako tarehe 25 Agosti 2005 akang'atuka kutoka madarakani.
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.