2015-02-14 12:26:55

Tanzia!


Askofu mstaafu Magnus Mwalunyungu wa Jimbo la Tunduru-Masasi, Tanzania, amefariki dunia Alfajiri ya Ijumaa tarehe 13 Februari 2015 katika Hospitali ya Tosamaganga, iliyoko Jimbo Katoliki la Iringa. Taarifa zinabainisha kwamba, Marehemu Askofu Mwalunyungu anatarajiwa kuzikwa kwenye Kanisa la Tosamaganga, Jimbo Katoliki la Iringa, Ijumaa, tarehe 20 Februari 2015. Historia inaonesha kwamba, humu ndimo alimozikwa pia Askofu Attilio Betramino, huyu alikuwa ni Askofu wa kwanza kabisa wa Jimbo Katoliki Iringa.

Marehemu Askofu Magnus Mwalunyungu alizaliwa kunako tarehe 25 Agosti 1930 huko Iringa. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, akapewa Daraja takatifu la Upadre kunako tarehe 23 Agosti 1959. Kwa miaka mingi alikuwa ni Gombera wa Seminari kuu ya Kipalapala, kiongozi ambaye lifahamu kwa kina na mapana historia ya Seminari ya Kipalapala.

Kunako tarehe 30 Machi 1992, akateuliwa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo II kuwa Askofu wa Jimbo la Tunduru-Masasi na kuwekwa wakfu hapo tarehe 25 Juni 1992. Baada ya kuihudumia Familia ya Mungu Jimboni Tunduru-Masasi, kwa ari na moyo mkuu, kunako tarehe 25 Agosti 2005 akang'atuka kutoka madarakani.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.