2015-01-30 15:28:00

Mwilisheni furaha ya Injili!


Baraza la Maaskofu Katoliki Croazia kwa kushirikisha na Shirikisho la Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, wameandika barua ya kichungaji kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, uliotangazwa na Baba Mtakatifu Francisko na kuzinduliwa rasmi Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio. RealAudioMP3

Mwaka wa Watawa utafungwa rasmi hapo tarehe 2 Februari 2016, Mama Kanisa atakapokuwa anaadhimisha Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni, sanjari na Siku ya Watawa Duniani, iliyoanzishwa na Mtakatifu Yohane Paulo II.

Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, watawa kwa namna ya pekee wanahamasishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba wanaishi na kumwilisha furaha ya Injili katika maisha yao, huku wakiendelea kuishi wito ambao ambao ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu na ustawi wa maisha ya binadamu.

Ni changamoto ya kuendelea kumwilisha karama za mashirika haya katika maisha na utume wa kwa Kanisa mahalia, kwani hii ni zawadi kubwa kutoka kwa Roho Mtakatifu kwa ajili ya Kanisa. Mwaka wa Watawa Duniani iwe ni fursa kwa watawa kusoma alama za nyakati na kusikiliza kwa makini sauti ya Roho Mtakatifu, ili kuepuka kinzani zinazoweza kujitokeza katika nadharia na uhalisia wa maisha; kwa kujifunga katika mitazamo yao na kusahau kile ambacho Roho Mtakatifu anawataka kutenda kwa wakati huu.

Maaskofu wanatambua kwamba, watawa wanakabiliwa na kinzani za ukosefu wa miito katika Mashirika yao, hali ambayo inakatisha tamaa kwa ajili ya uhai wa Mashirika haya kwa siku za usoni. Kinzani hizi ziwe ni changamoto ya kufanya tafakari ya kina kuhusu maisha na utume wao, tayari kukubali kufanya mabadiliko makubwa yatakayoleta mvuto na mguso kwa vijana wa kizazi kipya; maisha ambayo yanajikita katika ushuhuda wa mashauri ya Kiinjili.

Watawa waoneshe moyo wa toba na wongofu wa ndani, kama mtu binafsi na jumuiya, ili kweli waweze kukumbatia neema na baraka zinazotolewa na Kristo pamoja na Kanisa lake, wanapojitahidi kumfuasa kwa uaminifu na udumifu bila ya kumezwa na malimwengu.

Watawa wanahamasishwa kuendelea kumwamini na kumtumainia Mwenyezi Mungu katika maisha yao, ili kuishi na kutenda mintarafu mwanga wa imani, kama kielelezo makini cha uwepo endelevu wa Mungu kati ya watu wake. Watawa wawe ni mashahidi amini katika mapambano dhidi ya umaskini, ukosefu wa imani na migawanyiko kati ya watu.

Mwaka wa Watawa Duniani, uwe ni kikolezo cha thamani kubwa ya maisha ya kitawa nchini humo. Watawa waendelee kuwa ni watu wa sala na tafakari ya Neno la Mungu; watu wanaomwilisha imani katika huduma kwa Mungu na jirani. Baraza la Maaskofu Katoliki Croatia linasema kwamba, tarehe 14 Machi 2015 watawa nchini humo watafanya hija ya maisha ya kiroho, itakayowakutanisha kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Bistrica.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.