2015-01-30 15:20:26

Mwaka wa Watawa Duniani


Nembo ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, utakaozinduliwa rasmi Jumapili ya kwanza ya kipidni cha Majilio kwa mwaka 2014 inaonesha kwa kina na mapana tunu msingi zinazofumbatwa katika maisha ya kitawa, mwendelezo wa kazi ya Roho Mtakatifu, ambaye daima analitajirisha Kanisa kwa karama na tunu mbali mbali zinazojidhihirisha katika mashauri ya Kiinjili. Kwa njia hii, Roho Mtakatifu analiwezesha Kanisa kuendelea kuonesha Fumbo la uwepo wa Kristo ulimwenguni. RealAudioMP3

Nembo hii inamwonesha njiwa, ambaye kimsingi ni alama ya amani, changamoto kwa watawa kuwa kweli ni vyombo vya upatanisho, haki na amani ndani ya Kristo. Njiwa kadiri ya Mapokeo ya Mama Kanisa anaonesha uwepo wa Roho Mtakatifu, chemchemi ya maisha na mwendelezo wa kipaji cha ugunduzi. Njiwa anawakumbusha walimwengu kuhusu kazi ya uumbaji iliyofanywa na Mwenyezi Mungu, mwaliko wa kulinda na kutunza mazingira, kazi ya uumbaji, kwa ajili ya mafao ya kizazi cha sasa na kile kijacho.

Roho Mtakatifu anaonesha maisha mapya ambayo kwa njia ya Maji na Roho Mtakatifu, waamini wanaifia dhambi na kuzaliwa upya katika Fumbo la Pasaka, kumbe, Roho Mtakatifu anawaweka walimwengu wote wakfu kwa Kristo.

Alama ya maji katika Nembo ya Mwaka wa Watawa Duniani ni mwaliko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutafakari kwa kina kuhusu zawadi ya uumbaji na dhamana ambayo mwanadamu amekabidhiwa na Mwenyezi Mungu. Watawa waliowekwa wakfu, wanatumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia; kwa kuwashirikisha karama za Mashirika yao, wale wote wanaowahudumia kiroho na kimwili.

Watawa wanakumbushwa kwamba, wao ni wahudumu wa karama mbali mbali katika maisha ya watu, hata kiasi cha kujisadaka kama ushuhuda makini wa imani tendaji kwa Kristo na Kanisa lake, kama ambavyo imejionesha katika historia ya Kanisa. Watawa wanaalikwa kukumbatia Msalaba, kielelezo cha upendo na hekima ya Mungu kwa binadamu. Kanisa ni chombo cha wokovu na huruma ya Mungu, linapenda kuganga na kuponya, wale wote wanaokimbilia huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao.

Nyota tatu ambazo zinajionesha katika Nembo hii ni kielelezo kwamba, Watawa wamewekwa wakfu katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, kumbe wanaalikwa kushuhudia kwa maneno, lakini zaidi kwa njia ya matendo yao, udugu unaofumbatwa katika huduma kwa Familia ya Mungu. Watawa wanasukumwa kuwaonjesha walimwengu upendo unaobubujika kutoka katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, kama alivyofanya Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa. Bikira Maria ni kielelezo na mfano wa kuigwa na Watawa katika maisha na utume wao, ni Mama, Msimamizi na Mwombezi wa Watawa wote.

Maisha ya kitawa kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko yanamwilishwa na watu kutoka katika kila kabila, lugha na jamaa, changamoto kwa Watawa hao kuonesha kweli ile karama ya Roho Mtakatifu inayotenda kazi ndani mwao, huku wakisukumwa kwenda pembezoni mwa jamii ili kuwatangazia Watu wa Mataifa Furaha ya Injili.

Kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni “Vita Consecrata in Ecclesia hodie. Evangelium, prophesia spes”, yaani “Maisha ya kuwekwa wakfu ndani ya Kanisa; Unabii na Matumaini”. Kauli mbiu hii inakazia kwa namna ya pekee kabisa utambulisho wa maisha ya kitawa, mwelekeo wake, mang’amuzi na uzoefu wao katika maisha na utume wa Kanisa ulimwenguni. Watawa ni kielelezo cha neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu ndani ya Kanisa, wanaoendelea kuhamasishwa na Mama Kanisa kuonesha udumifu katika hija yao kwa Watu wa Mataifa na tamaduni mbali mbali hadi utimilifu wa nyakati.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.