2015-01-30 07:52:06

Barua ya wazi kwa Rais Barack Obama!


Viongozi wa kidini nchini Marekani wamemwandikia barua ya wazi Rais Barack Obama wa Marekani, kumtaka kuvalia njuga tatizo la ukosefu wa haki na amani huko Mashariki ya Kati pamoja na kuhakikisha kwamba, kinzani za kivita kati ya Israeli na Palestina zinafikia ukomo, ili watu waanze tena mchakato wa upatanisho, ujenzi wa amani na maendeleo. Kuchelewa kupata ufumbuzi wa kudumu wa migogoro hii, kutaendelea kusababisha maafa na majanga makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia.

Viongozi wa kidini wanasema, suluhu ya kivita haina mashiko, bali jambo la msingi ni kuwawezesha wahusika wa pande hizi mbili kuketi kwa pamoja na kuanza mchakato wa majadiliano, kwani historia inaonesha kwamba, vita imeendelea kuwa ni mama wa vita duniani. Viongozi wa Israeli na Palestina hawana budi kutambuana kama mataifa mawili yanayojitegemea na kwamba, yanapaswa kushirikiana kwa dhati.

Viongozi wa kidini wanasema, kuna mambo makuu matatu yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mchakato wa majadiliano kati ya wadau wakuu kwenye mgogoro wa kivita kati ya Israeli na Palestina: amani, usalama na pande hizi mbili kutambuana kama mataifa mawili huru kabisa. Hapa kuna haja ya kuhakikisha kwamba, matatizo na changamoto zinazoendelea kujitokeza zinapatia ufumbuzi wa kudumu, lengo ni kusaidia wananchi wa mataifa mawili kuishi kwa amani na utulivu. Hapa Serikali ya Marekani na Jumuiya ya Kimataifa vinaweza kutoa mchango wa hali ya juu ili kufikia malengo ya amani na utulivu huko Mashariki ya Kati.

Viongozi wa kidini wanahitimisha barua yao ya wazi kwa Rais Barack Obama wa Marekani, kwa kusema kwamba, mchakato wa amani hauna budi kusindikizwa na juhudi za makusudi kutoka kwa viongozi wa kidini kwa kushirikiana na Jumuiya za waamini. Viongozi wanashauri kupewa nafasi katika majadiliano haya, kwani hata wao wanagusa na mateso na mahangaiko ya wananchi wengi huko Mashariki ya Kati.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.