2015-01-26 10:04:17

Uzito wa malezi


Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la Nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo! Karibu kwa mara nyingine tena katika Kipindi chetu cha Kanisa la Nyumbani, tuendelee kuchota na kuneemeka kutoka katika Hazina ya mafundisho ya Mtaguso Mkuu wa II wa Vatican. 00:12:44:38 RealAudioMP3

Kwa wakati huu, kukukumbusha mpendwa msikilizaji, tunapitia hati zote za mtaguso wa pili wa Vatikani, moja baada ya nyingine. Lengo letu: tunataka Mafundisho ya Mama Kanisa kwa njia ya Mtaguso wa II wa Vatican, yajulikane kwetu sote, ili maisha yetu ya imani, ya kiutume na ya kijamii kwa ujumla, viwe na mkong’osio unaokubalika.

Leo tunaitupia jicho hati ile inayohusu malezi ya mwanadamu katika ujumla wake. Hati hii ambayo ni Tamko kati ya matamko matatu ya mababa wa Mtaguso Mkuu wa II wa Vaticani, kwa lugha ya Kilatini inajulikana kwa jina la Gravissimum Educationis, ikiwa na maana, Uzito wa Malezi. Mwangwi wa jumla tunaoupata katika hati hii ni kwamba Jamii nzima ya mwanadamu inahusika sawia katika suala la malezi.

Lengo la hati hii ni kumwalika zaidi mwanadamu kuongeza juhudi katika kuelewa umuhimu wa malezi kwa watoto, kwa vijana na watu wazima pia, ili kuweza kuwaunda watu kiroho na kimwili, wanaoweza kuyamudu malimwengu na kuyaratibisha sawia mahusiano yao kijamii. Sote tunaalikwa sana kutekeleza mipango ya malezi kwa mbinu sahihi zenye kuleta mafanikio mema, kwa ajili ya sasa na kesho iliyo bora zaidi.

daima linataka kuchangia juhudi hizo kufuatana na wake kwa watu wote, kwanza kabisa kama Mama na Mwalimu wa watu wote na kwa nyakati zote, na pili, kama Sakramenti ya jumla ya ukombozi kwa ajili ya kumkomboa mwadadamu kiroho na kimwili.

Gravissimum Educationis, inasisitiza ya kila mtu kupata malezi ya kumfaa. Huu kwanza ni wajibu wa wazazi katika familia na wote wanaoshika dhamana ya malezi katika maisha-jamii; zikiwemo taasisi za elimu kwa ngazi zote, kuhakikisha kwamba jitihada makini zinakuwepo za kumlea mwanadamu, kimwili, kiroho, kiakili na kiutashi, ili kumwandaa awe raia mwema na zawadi kwa jamii atakayoishi nayo mahali popote.

Gravissimum Educationis, inasema kwa msisitizo mkubwa kwamba, wazazi ndio walezi wakuu kwa watoto wao. Wasipoutimiza wajibu huo mkubwa, sio rahisi kwa taasisi nyingine kurekebisha aina hiyo ya mtu anayefanana na samaki mkavu, ambaye hakukunjwa akingali mbichi. Ndipo hapo, tunasema kwamba; kuwa na watoto tu haitoshi! Suala la msingi, ni watoto wa aina gani. Kama wazazi na jamii nzima tunahitaji watoto bora, basi, na tujifunge kibwebwe katika kuwalea vema.

Gravissimum Educationis, inaalika msaada kwa Kanisa na jamii kwa ujumla kuzisaidia familia katika suala la malezi ya watoto, na sio familia tu, bali kuchangia katika suala la malezi ya mwanadamu kwa ngazi zote kiroho na kimwili. Na Kanisa linatekeleza wajibu huo kwa njia mbali mbali zinazoonekana wazi, zikiwemo taasisi za elimu kwa viwango mbalimbali, warsha, makongamano, mafundisho jamii ya Kanisa, Mafundisho Mbalimbali ya Kanisa yenye lengo la kumkomboa mwanadamu, na pia kwa njia ya utendaji unaoonekana katika huduma za jamii. Ni jukumu la kila mwamini na watu wote, kutumia fursa hizo zinazotolewa na Kanisa katika kujiunda.

Ndani ya Gravissimum Educationis, Waalimu nao mashuleni wamepewa rai ya kuipokea kazi ya ualimu kama wito, na sio tu kama kitafutia fedha. Mwalimu wa ngazi yoyote ile, ana nafasi kubwa sana ya kujenga au kubomoa jamii. Mwalimu aliye makini katika kufikiri, kusema na kutenda, naye pia atatoa watu makini wenye kufikiri sawasawa, kusema kwa ufasaha na kutenda kwa ufanisi. Mwalimu mpigamiayo, mzembe na msinziaji katika fikra, daima atatoa watu wazembe katika jamii, waliojaa uvivu na kila aina ya uzembe kazini, ruhusa nyingi na malalamiko tele.

Mwalimu ni Kioo cha jamii. Mwalimu anafundisha darasani na nje ya darasa pia. Daima mwalimu aunganishe taaluma yake, uadilifu wake na maisha yake halisia katika jamii. Na hiyo ndio maana ya wito. Wito una mmyambuliko unganifu. Na kwa njia hiyo, mwalimu darasani, hawi tu ni msimulizi wa mambo ya vitabuni na ya zamani, bali ni mwalimu pia wa mtu-mkamilifu kwa nyakati zote na mahali pote.

Hati hii, Gravissimum Educationis, maana yake Uzito wa Malezi, inawalika wazazi nao kushirikiana na juhudi za waalimu pia katika kuwalea watoto. Wazazi, wasiwatupie au kuwazilia waalimu watoto wao, na hasa watoto wakorofi na watundu nyumbani. Hutokea mazingira fulani, wazazi huwapeleka watoto shuleni kwa sababu ni wasumbufu na waharibifu nyumbani, na hivyo kuondoa kero nyumbani, furushi la kero linapelekwa mbali sana katika shule ya bweni.

Na huko uzito wote unaachwa mikononi mwa waalimu au walezi bila kuwapa ushirikiano. Huko ni kukwepa wajibu na madhara yake ni kuzidi kuongeza ukuta wa mgawanyiko kati ya watoto na wazazi. Pawepo na ushirikiano, Gravissimum Educationis, inaelekeza. Na hati hii, inaongeza kusema, ni juu ya wazazi kuchagua kwa aina ya shule inayohakikisha watoto wao wanalelewa katika misingi sahihi ya utu na uadilifu kiroho na kimwili.

Na pia hati hii inasisitiza kwamba waamini wote wana haki ya kupata , hasa vijana wawapo mashuleni na nje ya shule, kwani wao ndio hazina na nguvu kazi-hai ya Kanisa na la Kanisa la leo na Kesho. Gravissimum Educations, inakaza kusema, Serikali haina haki ya kulazimisha watu wote kupata malezi ya aina moja, bali inapaswa kusaidia shule za watu binafsi na za kidini katika mchango wao kwa malezi ya watu.

Kwa jicho karimu la kichungaji, tukiangaziwa na Gravissimum Educationis, yaani Uzito wa Malezi, tunapenda kuangalisha kwamba, kikwepwe kishawishi cha nyakati zetu cha kubiasharisha elimu. Wapo watu binafsi wanaoanzisha shule kwa sababu wana fedha na wanapenda kujipatia fedha zaidi. Au hawana lengo la kutoa elimu sahihi, baliwana lengo la kupenyeza ajenda zao za siri. Hiyo ni hatari kwa Kanisa na Taifa.

Na pia, kuna kishawishi cha fasheni kwa baadhi ya wazazi na walezi, kupenda kupeleka watoto kwenye shule za gharama kubwa mno, bila kujali wanapata huko elimu ya namna gani. Ila mzazi anajisikia tu fahari kwamba ‘watoto wangu wanasoma shule za gharama, kuliko wote, tena mbali’. Hizo ni sifa na fahari zisizo na mshikio. Fasheni hizo ni hatari nazo kwa makuzi ya watoto wetu kiroho na kimwili. Tupeleke watoto shule, ambako tunauhakika watapata malezi bora ya kitaaluma, kumaadili, kiroho na kijamii.

Hati yetu, Gravissimum Educationis yaani, Uzito wa Malezi inatutakia sote uwajibikaji makini katika malezi ili tuunde kizazi cha sasa kilicho bora na kuijenga vyema yamii ya kesho. Kesho iliyo njema, ipo mikononi mwako na mwangu!

Kutoka katika Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.