2015-01-17 09:29:27

Tofauti si tija! Jengeni madaraja ya watu kukutana!


Kardinali Antonio Maria Veglio', Rais wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wahamiaji na wakimbizi katika maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi na Wahamiaji Duniani kwa Mwaka 2015 inayoadhimishwa na Mama Kanisa, Jumapili, tarehe 18 Januari 2015 anasema, ushirikishwaji wa watu katika jamii ni changamoto endelevu inayopaswa kufanyiwa kazi na Jumuiya ya Kimataifa kwa kujikita katika ushirikiano.

Tofauti kati ya watu ndani ya jamii zinapaswa kuwa ni daraja la watu kukutana ili kuendeleza majadiliano yaanayomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu. Ikumbukwe kwamba, maeneo ya kazi na shule ni sehemu murua kabisa zinazowakutanisha watu mbali mbali changamoto kubwa ni watu kufahamiana, kushirikiana na kusaidiana katika hija ya maisha ya kila siku, kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa utandawazi unaojali utu na heshima ya binadamu.

Kardinali Antonio Veglio' anasema, sera na mikakati inayoamriwa na Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuepuka tabia ya ubaguzi na kutowatambua watu katika utu na heshima yao, mambo amabayo wakati mwingi yamekuwa ni sababu ya chuki na kinzani zisizokuwa na mashiko. Watu wengi wanahama au kukimbia kutoka katika nchi zao ili kutafuta maisha bora zaidi na fursa za ajira. Lakini kwa bahati mbaya, sera nyingi zimekuwa zikiamsha hasira, chuki, vizuizi na hali ya watu kutothaminiana, mambo ambayo ni hatari kwa amani, utulivu na mfungamano wa kijamii.

Maeneo yaliyoko pembezoni mwa miji mikuu duniani, yanaonekana kusahauliwa na wanasiasa katika sera na mikakati yao; mambo ambayo yanachangiwa pia na athari za myumbo wa uchumi kimataifa pamoja na kumong'onyoka kwa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia; matokeo yake, maeneo haya yamekuwa ni chanzo cha chuki, kinzani na ubaguzi dhidi ya wahamiaji na wageni.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake katika Maadhimisho ya Siku ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani kwa Mwaka 2015 anasema Kanisa halina mipaka kwani ni Mama wa wote! Hii ni changamoto ya kuheshimu na kuthamini utu wa binadamu na haki zake msingi. Tofauti za kidini na kiimani kisiwe ni kisingizio cha vita na kinzani za kijamii zisizokuwa na mashiko. Watu wajifunze na kudumisha utamaduni wa majadiliano, kwa kuheshimiana, katika ukweli na uwazi, mambo msingi yanayotiliwa mkazo na Baba Mtakatifu Francisko.

Dhana ya uhamiaji imekuwa ni chanzo cha majanga na vifo kwa watu wengi anasema Kardinali Antonio Veglio'. Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwepo na udhaifu mkubwa katika kulinda na kudumisha haki msingi za binadamu kwa kisingizio cha usalama wa taifa. Kuna wahamiaji wengi wanaodhulumiwa na kunyonywa; kundi kubwa la watu linalotumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo! Haya ni mambo yanayopaswa kufanyiwa kazi mintarafu Sheria na Protokali za Kimataifa.

Kila mtu ana thamani mbele ya Mungu na jamii, changamoto ya kujenga na kudumisha mshikamano wa upendo na udugu; kila mtu akipewa haki zake msingi; ili kujenga na kuendeleza mafao ya wengi ndani ya jamii. Inasikitisha kuona kwamba, kuna baadhi ya wafanyakazi Serikali na katika Mashirika ya Misaada Kimataifa wanaojitajirisha kutokana na magumu ya wakimbizi na wahamiaji.

Kardinali Veglio' anasema kuna haja ya kuwa na mwelekeo mpya unaothamini na kujali wahamiaji na wakimbizi kuwa ni sehemu ya rasilimali watu, inayoweza kuchangia katika ustawi na maendeleo na nchi na kwamba, rasilimali hii si tishio kwa usalama wa taifa.

Vita inayoendelea Syria, Iraq na huko Mashariki ya Kati katika ujumla wake, imepelekea uwepo wa wimbi kubwa la wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta hifadhi na msaada kutoka kwa Jumuiya ya Kimataifa. Ni maeneo yanayopaswa kusaidiwa ili amani, usalama na utulivu viweze kurejea tena. Watu wanaotafuta hifadhi, wahakikishiwe usalama wa maisha yao; tabia ya kufumbia macho mahangaiko ya watu ni hatari sana!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.