2014-12-19 16:26:04

Amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu!


Amani inayopaswa kutawala katika mioyo ya watu ni zawadi kutoka kwa Roho Mtakatifu inayoambatana na: upendo, furaha, uvumilivu, utu wema, uaminifu, upole, kiasi, juu ya mambo kama hayo hakuna sheria anasema Mtakatifu Paulo na kwamba, kuna tofauti ya karama, changamoto na mwaliko kwa waamini kushirikiana na neema ya Roho Mtakatifu katika uhuru kamili. Amani kama zawadi kutoka kwa Roho Mtakatifu inajionesha katika utulivu wa moyo na hii ndiyo ambayo watu wengi wanayohitaji katika maisha yao.

Amani ya ndani ni kati ya mambo ambayo Mama Kanisa amependa kuyaendeleza katika historia ya maisha ya mwanadamu na tasaufi ya Kanisa, iliyokuzwa na kupanuliwa zaidi na Mtakatifu Agostino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa, kwani moyo wa mwanadamu hauwezi kutulia wala kupata amani ya kweli hadi pale utakapoungana na Muumba wake, kwa kutekeleza mapenzi yake na hatimaye, kupata amani ya milele.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Padre Raniero Cantalamessa, Mhubiri mkuu wa Nyumba ya Kipapa, kama sehemu ya maadhimisho ya Kipindi cha Majilio, mahubiri ambayo yametolewa Ijumaa tarehe 19 Desemba 2014 kwenye Kikanisa cha Mama wa Mkombozi, mjini Vatican. Anasema, njia ya amani ni kanuni msingi ya mang'amuzi katika maisha ya mwanadamu mintarafu mapenzi ya Mungu kwa kuhakikisha kwamba, mapambano ya maisha ya kiroho dhidi ya mapungufu ya kibinadamu yanakuzwa na kuendelezwa zaidi. Ni changamoto na mwaliko wa kubeba vyema Msalaba na kuanza kumfuasa Yesu katika njia ya Msalaba na kuishi kadiri ya mang'amuzi ya maisha ya kiroho.

Amani ya ndani ni sehemu ya mchakato wa nguvu inayooneshwa na mwamini kwa kushirikiana na Roho Mtakatifu, kwa kusikiliza kwa makini na kumwilisha Mafundisho ya Roho Mtakatifu katika uhalisia wa maisha, katika hali ya unyenyekevu. Mwamini anayetekeleza mambo haya katika maisha yake anaweza kuingia katika ufalme wa amani na utulivu wa ndani, daima akijitahidi kumfuasa Kristo.

Hii inatokana na ukweli kwamba, Mwenyezi Mungu yuko tayari kumlinda na kumtegemeza mtu ambaye anategemea na kumwaminia katika amani kamilifu; ndiyo changamoto inayotolewa na Yesu kwa wafuasi wake kutojitaabisha mno na kesho ambayo tayari iko mikononi mwa Mwenyezi Mungu. Hii ni changamoto kwa waamini kujenga matumaini yao kwa Mwenyezi Mungu ambaye ni mwamba salama.

Wakati huu, waamini wanapojiandaa kuadhimisha Siku kuu ya Noeli wanapaswa kutunza amani ndani mwao kwa kutambua kwamba, wanapendwa na Mwenyezi Mungu na zawadi ya kwanza ambayo mwanadamu amepewa katika Fumbo la Umwilisho ni amani duniani kwa watu wanaopendwa na Mwenyezi Mungu na hii ni zawadi kwa wote pasi na ubaguzi.

Je, ni nani anayeweza kuwatenga watu na upendo wa Mungu anauliza Mtakatifu Paulo, Je, ni dhiki, shida, adha, njaa, utupu, hatari au upanga? Haya ni mambo ambayo yanaleta shida na mahangaiko katika maisha ya mwanadamu, lakini hakuna kitu kinachoweza kuwatenga na upendo wa Mungu ulio katika Yesu Kristo. Licha ya maendeleo ya sayansi na teknolojia, mwanadamu bado anaendelea kubaki kuwa ni dhaifu kutokana na uwepo wa magonjwa yasiokuwa na tiba na vitendo vya kigaidi; yote haya yanapita, lakini mtu ambaye amejikabidhi mbele ya Mwenyezi Mungu hawezi kupungukiwa na chochote. Noeli iwe ni kipindi cha amani inayojikita kwa Mwenyezi Mungu, jirani na katika moyo wa mtu binafsi!.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.