Marekani na Cuba wafungua ukurasa mpya wa uhusiano wa kidiplomasia
Baba Mtakatifu Francisko amepokea kwa moyo mkunjufu na furaha taarifa kwamba, Serikali
ya Marekani na Cuba ambazo kwa miaka mingi zimekuwa ziliangaliana kwa "jicho la makengeza"
hatimaye, zimekubali kurudisha tena mahusiano ya kidiplomasia kwa ajili ya mafao ya
pande hizi mbili.
Katika miezi ya hivi karibuni, Baba Mtakatifu Francisko
aliwaandikia barua Rais Barack Obama wa Marekani pamoja na Rais RaĆ¹l Castro wa Cuba,
akiwasihi kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro wa kibinadamu baina ya nchi hizi
mbili tayari kuanza ukurasa mpya wa mahusiano ya kidiplomasia. Mwezi Oktoba, wawakilishi
wa nchi hizi mbili walikuwa mjini Vatican ili kujadili kwa pamoja masuala nyeti na
matokeo yake, pande hizi mbili zikawa zimeridhika na maamuzi yaliyokuwa yamefikiwa.
Vatican inasema, itaendelea kuunga mkono mchakato wa mahusiano mapya ya kidiplomasia
kati ya Marekani na Cuba kwa ajili ya mafao ya pande hizi mbili!