2014-12-16 10:31:00

Uchu wa mali na madaraka kisiwe ni chanzo cha majanga na kinzani!


Kardinali John Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, ameiomba Serikali ya Nigeria chini ya uongozi wa Rais Goodluck Jonathan kuhakikisha kwamba, uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini humo, unakuwa huru na wa haki bila kutumia nguvu ya dolla kupita kiasi, jambo ambalo mara nyingi limekuwa ni sababu ya watu kutaka kulipizana kisasi.

Ni wajibu wa kila Chama cha kisiasa nchini Nigeria kutekeleza vyema wajibu wake kwa kuendesha kampeni zinazopania kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa badala ya kuendekeza udini na ukabila, chanzo kikuu cha majanga na maafa kwa wananchi wa Nigeria. Mchakato mzima wa upigaji kura, tangu wakati wa kampeni, siku yenyewe ya kupiga, zoezi la kuhesabu kura na hatimaye kutangaza washindi, hauna budi kusimamiwa vyema kwa kuzingatia misingi ya ukweli, uwazi na uwajibikaji.

Ikiwa kama wanasiasa watachakachua matokeo ya uchaguzi, kuna hatari kubwa kwamba, wananchi wakaamua kuchukua sheria mikononi mwao ili kutafuta haki ilipotea! Huu utakuwa ni mwanzo wa machafuko na umwagaji wa damu ya watu wasiokuwa na hatia. Serikali kuu ihakikishe kwamba, uchaguzi unakuwa huru na wa haki, ili kweli demokrasia iweze kuchukua mkondo wake.

Kardinali Onaiyekan anawataka wanasiasa kuachana na siasa za chuki na kampeni za kinyongo kwa kutishia usalama na maisha ya watu, ikiwa kama baadhi yao watashindwa kupata ridhaa ya kuongoza nchi, kwani asiyekubali kushindwa huyo si mshindani.

Kwa wale watakaoshinda na kupewa ridhaa ya kuongoza nchi, waoneshe shukrani kwa kutekeleza ahadi zao na wale watakaoshindwa, basi wajenge uvumilivu kwa kujipanga vyema zaidi katika chaguzi nyingine zijazo. Umefika wakati kwa wananchi wa Nigeria kuhakikisha kwamba, utawala wa sheria na demokrasia vinashika mkondo wake.

Uchu wa mali na madaraka ni chanzo cha majanga na maafa makubwa Barani Afrika. Wanasiasa wanapaswa kutambua kwamba, cheo ni dhamana wanayopewa na wananchi ili kuchochea mchakato wa maendeleo. Fedha isiwe ni kisingizio cha kuvunja misingi ya haki, amani, ustawi na maendeleo ya watu.









All the contents on this site are copyrighted ©.