2014-11-28 12:03:05

Barua ya Papa Francisko katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani 2014 - 2016


Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, uliotishwa na Baba Mtakatifu Francisko yanazinduliwa rasmi katika maadhimisho ya Jumapili ya Kwanza ya Kipindi cha Majilio, tarehe 30 Novemba 2014 sanjari na Jubilee ya miaka 50 ya Waraka wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, Fumbo la Kanisa, "Lumen Gentium" inavyojulikana na wengi kama Mwanga wa Mataifa, hati ambayo imefafanua kwa kina na mapana nafasi ya Watawa ndani ya Kanisa. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho haya amewaandikia Watawa Barua ya Kichungaji inaobainisha Malengo ya Mwaka wa Watawa; Matarajio na Mwelekeo wa Mwaka wa Watawa utakaohitimishwa hapo tarehe 2 Februari 2016, Siku kuu ya Kutolewa Yesu Hekaluni, sanjari na Siku ya Watawa Duniani, kama ilivyoelekezwa na Mtakatifu Yohane Paulo II katika Waraka wake wa kichungaji kuhusiana na Maisha ya Kitawa.

Katika lengo la kwanza, Baba Mtakatifu anatawaka watawa kuthamini uzoefu watakaoupata katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, kwa kuangalia maisha yaliyopita kwa moyo wa shukrani. Mwaka wa Watawa Duniani, iwe ni fursa kwa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kuangalia kwa kina na mapana historia na maendeleo ya Shirika, kwani simulizi la historia ya Mashirika haya ni sehemu ya mchakato wa kutaka kupyaisha utambulisho wao ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano kati ya wanashirika, kwa kutambua na kuthamini asili yao.

Baba Mtakatifu anawataka watawa kuchunguza dhamiri zao ili kuangalia kwa kina na mapana jinsi ambavyo wamejitahidi kumwilisha karama ya Shirika lao katika nyakati mbali mbali za kihistoria; wameonesha ugunduzi gani uliowasaidia kusonga mbele kwa imani na matumaini; ni matatizo na vikwazo gani walivyokutana navyo na jinsi walivyojitahidi kuvipatia ufumbuzi.

Hii ni nafasi ya kuangalia pale ambapo Shirika limepindisha karama yake kama sehemu ya mapungufu ya kibinadamu au wakati mwingine kwa kutokumbuka mambo msingi katika karama ya Shirika. Hapa anasema Baba Mtakatifu ni kuona jinsi ambavyo Shirika limethubutu katika kipindi cha miaka 50 iliyopita tangu baada ya Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ulioleta ari na mwamko mpya kutoka kwa Roho Mtakatifu ndani ya Kanisa.

Lengo la pili anasema Baba Mtakatifu ni kuhakikisha kwamba watawa wanaishi wakati huu kwa hamasa na moyo mkuu, kwa kutambua na kung'amua asili ya maisha na utume wa Shirika. Kwa Waanzilishi, anasema Baba Mtakatifu, Injili imekuwa kwao ni kanuni msingi na kwamba, Katiba za Mashirika yao ilikuwa ni sehemu ya mchakato wa kumwilisha Injili katika utimilifu wake, huku Yesu Kristo akipewa kipaumbele cha kwanza na kushikamana naye, hata kudiriki kusema pamoja na Mtakatifu Paulo "... kwangu mimi kuishi ni Kristo..." Nadhiri zilimaanisha kuonesha upendo wao wa dhati kwa Kristo.

Hii ndiyo hali inayopaswa kuwasukuma watawa kujiuliza wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa, jinsi gani wanavyotekeleza mashauri ya Kiinjili katika maisha na utume wao na ikiwa kama kweli nadhiri zimekuwa ni mwongozo na dira ya maisha ya kila siku katika uchaguzi wa mambo ambayo wanapaswa kuyatekeleza. Yesu anawataka kutekeleza, kumwilisha Neno lake pamoja na kusikia huruma yake, kwa kutambua kwamba, upendo hauna mipaka, bali umeendelea kufungua njia ili kupeleka upepo wa Injili katika tamaduni pamoja na medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu.

Mwaka wa Watawa Duniani ni fursa ya kujiuliza maswali msingi ikiwa kama kweli watawa wamekuwa waaminifu kwa utume waliokabidhiwa na Mama Kanisa, ikiwa kama wameutekeleza kwa moyo wa umoja hata pale ambapo kuna utofauti na kinzani, kwani waanzilishi wa Mashirika haya waliguswa kwa namna ya pekee na umoja uliooneshwa na Mitume walipokuwa wanamzunguka Yesu

Leo hii katika ulimwengu mamboleo, kuna kinzani nyingi ambazo zinagumisha maisha ya pamoja kati ya watu wenye tamaduni mbali mbali, kwa kuwanyanyasa wanyonge; kwa kukazia tofauti ambazo si jambo la msingi sana; watawa wanachangamotishwa kwa namna ya pekee kuhakikisha kwamba, wanajenga jumuiya ambayo ni mfano unaotambua utu na heshima ya kila mtu pamoja na kushirikisha karama zao mbali mbali sanjari na kujenga mahusiano ya kidugu.

Lengo la tatu, la Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni kukumbatia maisha yajayo kwa matumaini. Matatizo na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha ya kitawa na kazi za kitume zimepelekea kupungua kwa miito hasa kutokana na baadhi ya watu kuwa na mawazo mepesi mepesi. Ni katika mawazo kama haya anasema Baba Mtakatifu Francisko, watawa wanapaswa kujenga matumaini yao, ambayo kimsingi ni matunda ya imani kwa Bwana wa historia anayerudia kusema "... Usiogope ... maana mimi nipo pamoja nawe". Haya ni matumaini anasema Baba Mtakatifu ambayo hayakujengwa katika idadi wala kazi, bali kwa yule ambaye wamemwekea matumaini yao kiasi kwamba, hakuna lisilowezekana na kwamba, haya ni matumaini yasiyodanganya kamwe.

Baba Mtakatifu anawaalika watawa wasitumbukie katika kishawishi cha idadi ya watawa au kazi wanazozifanya au kwa kujiaminisha katika nguvu zao wenyewe. Watawa vijana wanahimizwa kwa namna ya pekee kuwa ni wadau wakuu katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani kwa kuanzisha mchakato wa majadiliano na watawa wazee ambao wamewatangulia katika utumishi. Kwa njia ya mshikamano wa kidugu wanaweza kutajirishana uzoefu na mang'amuzi pamoja na kuwashirikisha mawazo ambayo pengine tangu mwanzo hayakufahamika na wengi, ili kutoa mwelekeo na ari mpya, ili kwa njia nyingine tena kuweza kumwilisha Injili, jibu makini linalokidhi mahitaji ya ushuhuda na utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu.

Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa, analialika Kanisa kuonesha furaha inayobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kurutubishwa na udugu unaomwilishwa katika jumuiya kwa watawa kujisadaka katika huduma ndani ya Kanisa, kwenye Familia, kwa Vijana, Wazee, Maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Baba Mtakatifu anaonya kwamba, jamii inayokumbatia utamaduni wa ufanisi, ubora na mafanikio yanayowatenga maskini na wale wasiokuwa na mwelekeo, ionjeshwe ushuhuda kwa ya njia maisha na kweli kutoka katika Maandiko Matakatifu... Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, Kanisa haliwezi kukua kwa kuwaongoa watu, bali kwa kuonesha mvuto wenye mguso na mashiko. Hivi ndivyo ilivyo pia kwa maisha ya kitawa ambayo kamwe hayawezi kutegemea ufanisi pamoja na nguvu ya nyenzo zake. Thamani ya Kanisa inapata msingi wake kwa kuishi Injili na kutoa ushuhuda wa imani tendaji.

Kanisa ni chumvi na mwanga wa dunia linachangamotishwa kuonesha ile chachu ya uwepo wa Ufalme wa Mungu kwanza kabisa, kwa njia ya ushuhuda unaojikita katika upendo wa kidugu, mshikamano pamoja na kushirikishana, katika kushuhudia unabii, mwaliko kwa watawa kuamsha tena ulimwengu. Nabii anasema Baba Mtakatifu anapata uwezo wa kupembua historia anamoishi na kuipatia tafsiri sahihi.

Nabii ana uwezo kung'amua pamoja na kukemea dhambi na maovu ya kijamii na ukosefu wa haki kwa sababu ni mtu huru anayewajibika moja kwa moja mbele ya Mwenyezi Mungu na wala hana mpango na mambo mengine, isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake. Nabii daima ni mtu anayejishikamanisha na maskini, wasiokuwa na sauti kwani anatambua kwamba, Mwenyezi Mungu daima yuko upande wao.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka watawa kuondokana na dhana ya kuishi kwenye ombwe na badala yake wawe na uwezo wa kujenga maeneo ambamo wanaweza kuishi mantiki ya zawadi ya Kiinjili, yanayojikita kwa namna ya pekee katika udugu, kupokea utofauti sanjari na kuonjeshana upendo. Watawa ni watu wanaotambulikana kuwa ni mabingwa wa umoja, changamoto na mwaliko wa kuonesha tunu hii wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa, ili kukuza udugu uliooneshwa na Waanzilishi wa Mashirika ili uweze kukua na kuenea zaidi. Umoja ujioneshe katika jumuiya husika, ndani ya Shirika ambamo mara nyingi kuna kinzani, maseng'enyo, wivu usiokuwa na maendeleo, chuki na hasira.

Baba Mtakatifu anawaalika watawa kuonesha ushuhuda wa kinabii katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa, kwa kutoka katika mazingira ya Mashirika husika ili kuibua pamoja na Mashirika mengine, mbinu mkakati katika ngazi ya Makanisa mahalia na lile la Kiulimwengu; kuhusu: malezi, uinjilishaji na huduma za kijamii, kwa kujitambua katika ukweli pamoja na kugundua mahitaji mapya kwa watu wa nyakati hizi bila kugubikwa na ugonjwa wa kwa Mashirika haya kujitafuta yenyewe.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, anapenda kuona utekelezaji halisi wa mikakati inayopania kuwasaidia na kuwahudumia wakimbizi; uwepo wao wa karibu kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; kuonesha kipaji cha ugunduzi katika Katekesi, utangazaji wa Neno la Mungu pamoja na maisha ya sala; kwa kufanya marekebisho katika miundo mbinu, kwa kutumia majengo kwa ajili ya kutoa huduma kadiri ya mahitaji ya Uinjilishaji na huduma ya mapendo, kwa kusoma alama za nyakati.

Baba Mtakatifu Francisko katika Barua yake kwa Mwaka wa Watawa Duniani, anawaalika waamini walei wanaoshiriki katika karama na utume wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, kujitahidi kuuishi Mwaka huu kama kipindi cha neema, ili kutambua zawadi waliyokirimiwa na Mwenyezi Mungu. Anawaalika kuuadhimisha Mwaka wa Watawa kwa kushirikisha Familia nzima, ili kukua na kujibu kwa pamoja wito wa Roho Mtakatifu kutoka katika jamii mamboleo.

Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa, wakati watawa watakapokuwa wanakutanika kati yao, wajitahidi hata wao kushiriki kikamilifu ili kuonesha zawadi hii kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ili kuonja karama kutoka kwa Mashirika mengine na vyama vya kitume, ili kuweza kutajirishana na kusaidiana kwa pamoja.

Kwa moyo wa unyenyekevu, Baba Mtakatifu Francisko anawaalika watawa waliojiweka wakfu na washirika wa Mashirika tofauti na Makanisa tofauti na Kanisa Katoliki kushirikishana umoja na udugu, ili majadiliano ya Kiekumene katika maisha ya kitawa, yasaidie mchakato wa ujenzi wa umoja kati ya Makanisa pamoja na kukoleza moyo wa kuishi kwa amani na utulivu Mashirika yenye tamaduni na mapokeo mbali mbali.

Baba Mtakatifu anahitimisha Barua yake katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani kwa kuwaalika Maaskofu kuendeleza na kukuza karama mbali mbali katika Makanisa yao: kwa kupokea na kukumbatia karama mpya na zile za zamani, kwa kuwasaidia, kuwahamasisha na kuwaongoza, daima wakionesha ukaribu wao kwa njia ya upendo kwa wale wanaoteseka na wanyonge; ili waweze kupata watawa wengine watakaosaidia kuendeleza "Jahazi la Kristo". Maaskofu wawasaidie Watu wa Mungu kwa njia ya Mafundisho yao kuhusu umuhimu wa Maisha ya Kitawa, ili utakatifu uweze kung'aa ndani ya Kanisa.

Imehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.