2014-11-27 08:24:09

Papa ni mjumbe wa mshikamano wa upendo na udugu kati ya Makanisa!


Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox anasema, hija ya kiekumene ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Uturuki katika maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Andrea Mtume, inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 30 Novemba, ni fursa makini ya kutangaza na kushuhudia kwa matendo upendo na mshikamano wa kidugu miongoni mwa Wakristo.

Patriaki Bartolomeo akihojiwa na Jarida la “Famiglia Cristiana” anasema, kwa miaka mingi Makanisa haya mawili yamekuwa yakituma wajumbe katika maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo mjini Vatican na ile ya Mtakatifu Andrea inayofanyika mjini Costantinopoli, matukio ambayo yanaonesha kwa kiasi kikubwa Makanisa haya yanapania kushirikiana na kushikamana kwa dhati, ili kushuhudia umoja na udugu kwa Kristo na Kanisa lake.

Baba Mtakatifu Francisko anatembelea Uturuki nchi ambayo haina dini rasmi, changamoto na mwaliko kwa waamini wa dini mbali mbali kuendelea kushikamana na kusaidiana kama ndugu na kwamba, tofauti zao za kidini na kiimani zisiwe ni mwanzo wa chuki na vita kama inavyotokea sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu atajionea utajiri na kuonja ukarimu wa wananchi wa Uturuki atakapotembelea mjini Ankara na Istanbul.

Ni hija fupi ya Kiekumene, lakini inalenga kuimarisha ujumbe kwa watu kuishi kwa amani na udugu. Uturuki ina historia kubwa katika maisha na utume wa Kanisa. Hapa ni mahali ambapo Mababa wa Mitaguso kadhaa ya Kanisa walikutana na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa katika Karne za mwanzo mwanzo kabisa. Ni haki kabisa kwa Makanisa kutambua na kuthamini mchango uliotolewa na Kanisa la Kiorthodox katika maisha na utume wa Kanisa, lakini pia hata katika historia ya binadamu.

Baba Mtakatifu Francisko ni mtu wa kawaida, anayeonesha upendo na mshikamano kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Anaheshimiwa na kuthaminiwa na Makanisa ya Mashariki kwa kukazia kwamba, yeye ni Askofu wa Roma. Ni kiongozi anayelifahamu Kanisa la Mashariki, ndiyo maana anaendelea kuwashangaza wengi kwa kuteuwa Makardinali nane watakaomsaidia kufanya maamuzi makubwa katika maisha na utume wa Kanisa, kielelezo cha mchakato wa Sinodi.

Baba Mtakatifu Francisko anataka kuliongoza Kanisa kwa mfumo wa Kisinodi, dhana inayoweza kurahisisha majadiliano ya Kiekumene na Kitaalimungu ambayo yanazidi kusonga mbele miongoni mwa Makanisa haya mawili. Mahusiano kati ya viongozi wakuu wa Makanisa na kati ya waamini yameendelea kuimarika mwaka hadi mwaka, ili kwa pamoja, waweze kuwatangazia watu wa kizazi hiki, Injili ya Furaha na Matumaini yanayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake, kwa njia ya ushuhuda wa upendo na mshikamano wa kidugu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.