2014-11-27 11:43:09

Changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi!


Ziara ya kikazi ya Baba Mtakatifu Francisko huko Strasbourg, Ufaransa, hapo tarehe 25 Novemba 2014 imeacha changamoto nyingi zinazopaswa kufanyiwa kazi na Jumuiya ya Ulaya kwa kushirikiana na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, CCEE, ambalo liliwakilishwa na viongoni wake wakuu chini ya Kardinali Peter Erdò, Rais wa Baraza.

Baba Mtakatifu anaitaka Jumuiya ya Ulaya kuwa ni kikolezo cha matumaini mapya yanayojikita katika misingi ya haki, amani na mshikamano wa dhati kati ya Watu wa Mataifa. Wajumbe wamepokea changamoto zilizotolewa na Baba Mtakatifu kwa mikono miwili kwani ni ujumbe ambao umegusa sakafu za mioyo yao, ndio maana hawakusita kushangilia, pale ambapo waliguswa kwa namna ya pekee kutoka katika undani wa maisha, shughuli na mikakati yao!

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Balani Ulaya linasema katika tamko lake kwamba, Baba Mtakatifu amewataka viongozi wa Jumuiya ya Ulaya kufikiri na kutenda kwa kuzingatia kanuni maadili zinazojikita katika historia ya Bara la Ulaya kama ilivyoasisiwa na waanzilishi wake waliotaka Bala la Ulaya lijengeke katika misingi ya ukweli, mshikamano, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wake.

Haya ni mambo ambayo yanapaswa kufanyiwa kazi, kwa kutambua kwamba, Kanisa pia lina mchango wake mkubwa katika mchakato wa maendeleo endelevu hususan katika kukuza na kudumisha Injili ya Uhai; tunu msingi za maisha ya ndoa na familia pamoja na kukuza na kudumisha utu na heshima ya binadamu. Ni matumaini ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Barani Ulaya kwamba, changamoto zilizotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kichungaji huko Strausbourg, Ufaransa zitafanyiwa kazi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ulaya.







All the contents on this site are copyrighted ©.