2014-11-26 14:37:40

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, Mwaka Be wa Kanisa


Mpendwa mwana wa Mungu unayetegea sikio Radio Vatican, ninakutakieni Dominika ya furaha na mwanzo mzuri wa kipindi cha Majilio. Tunatafakari pamoja Neno la Mungu katika Dominika ya kwanza ya majilio, ujumbe kutoka Neno la Mungu ukiwa ni ule unaonaokudai KUKAA TAYARI KATIKA SALA KWA AJILI YA KUMSUBIRI MASIYA AJAYE KWA JINA LA BWANA. RealAudioMP3

Mpendwa, kwa kawaida Majilio ni kipindi cha matayarisho kwa ajili ya kuzaliwa Masiha. Hata hivyo Kanisa halitafakari tu kuzaliwa kwa Masiha na kuishia hapo bali pia hutafakari na kuwatayarisha waamini kwa ajili ya ujio wa pili wa Bwana. Ndiyo kusema Dominika ya kwanza hadi tarehe 16 Desemba, Mama Kanisa ametuwekea masomo ambayo hutuongoza katika maandalizi ya ujio wa pili.

Kwa maana hiyo litrujia yatutaka kungoja kwa matumaini yaliyojaa furaha na hamu kurudi kwake Yesu Kristu mara ya mwisho. Wote tunaalikwa kuitengeneza njia ya Bwana mwaliko ambao Yohane Mbatizaji aliwapatia Waisraeli.

Sehemu ya pili ya kipindi cha Majilio yaani kuanzia 17 Desemba hadi 25 Desemba yaani Sherehe ya kuzaliwa Mkombozi, Liturujia yatutaka kutafakari, kujikusanya na kuweka mawazo yetu katika kutayarisha sherehe hiyo ya Noeli. Kanisa linaimba daima Ewe mfalme, Ewe EMANUELI UJE KUTUOKOA.

Katika kipindi cha majilio, Mama Kanisa akitumia mafundisho ya Nabii Isaya atuhimiza kumtumaini Mungu na kuacha mambo ya kipagani, mwenendo mbaya na hivi kumfuasa Kristo katika maisha ya utakatifu. Mafundisho haya kusema yatudai kuongoka na kukaa tayari tukimsubiri Masiha. Kama Nabii Isaya alivyowatayarisha watu wa kale kumtumaini Mungu ndivyo anavyotutayarisha kujiandaa kumpokea Bwana mioyoni mwetu hivi leo.

Kama kielelezo cha matayarisho ya Noeli yaani ujio wa Bwana, iko desturi ya kuwasha mishumaa minne, katika majuma manne kielelezo cha mwanga wa Kristu na mishumaa hii huitwa mshumaa wa Nabii Isaya juma la kwanza, mshumaa wa Yohane Mbatizaji, juma la pili. Wote twatambua nafasi ya Yohane Mbatizaji katika kuandaa ujio wa Masiha, yeye ni mtangulizi mnyenyekevu ambaye anatualika kuitengeneza njia ya Bwana kwa ujio wa pili. Anamtambulisha Masiha kwa watu na hivi kabla anawatayarisha watu waongoke.

Katika juma la tatu tunawasha mshumaa wa Mtakatifu Yosefu. Hatuwezi kuzungumza Masiha bila kumtaja Yosefu. Ni Baba mlishi wa Yesu Kristu ni mme wa Bikira Maria. Ni Baba mnyenyekevu asiye na makuu na kwa namna hiyo basi, katika unyenyekevu wake ametekeleza mpango wa Mungu kwa upendo na unyenyekevu.

Na mwisho katika Dominika ya nne ya majilio, tunawasha mshumaa wa Mama Bikira Maria, mama wa Mkombozi, Mama asiye na doa, mama anayetufundisha kujitoa kiaminifu pasipo kujibakiza katika kutekeleza mapenzi ya Mungu na hivi anasema, “mimi ni mtumishi wa Bwana nitendewe kama ulivyonena”.

Tunapofungua mwaka wa Kanisa (2014 - 2016) kwa kipindi cha Majilio, tunayo furaha kuu pia, katika mwaka huu, Mama Kanisa anapofungua Mwaka wa Watawa Duniani, maisha ya kujitoa bila ya kujibakiza mbele ya Mungu na jirani. Katika mwaka wa Watawa Duniani, mwaliko kwanza kwa Watawa, ni kuwa tayari kuifanya Injili ipenye katika maisha ya watu kwa njia ya unabii wao, wakijaribu kwa unabii huo kujenga matumaini mapya.

Mama Kanisa anawaalika yakuwa uwepo wao uwe ni njia ya kutangaza ufalme wa Mungu, ufalme ambao ni kwa ajili ya amani, mapendo, furaha, imani na matumaini mapya tukikaribia mbingu mpya.

Mpendwa, jambo hili si tu kwa ajili ya Watawa bali ni la Kanisa zima, kumbe, tunaalikwa nasi sote kuongozwa na Injili ili kupeleka Neno la furaha na matumaini kwa watu. Huu ni wajibu wa kinabii, wajibu ambao kama Manabii walivyotekeleza mwaliko wa Mungu na kupeleka habari hiyo njema kwa watu, nasi tunaalikwa kuutekeleza mpango wa Mungu wa kupeleka furaha na mapendo kwa mataifa.

Mpendwa mwana wa Mungu, katika somo la kwanza, wana wa Israeli wako utumwani Babeli, wanahangaika na kuteseka na wanaona mateso yao yanatokana na dhambi zao na hivi wanasali kwa kulalamika kwa nini Mungu amewaacha na hata wakaweza kutenda dhambi ya kutokumcha yeye aliye Bwana! Wanajiuliza na kumwuliza Mungu je tutaokolewa? Kutokana maswali haya wanafikia hitimisho na kusema mbele ya Mungu, hakika wewe u Baba yetu sisi tu udongo nawe umfinyanzi, na sisi tu kazi ya mikono yako. Sala hii yaonesha toba, yaonesha uongofu ambao Nabii Isaya anatualika tuutafute.

Katika somo la II Mtume Paulo anamshukuru Mungu aliyewainua Wakorinto, akawapa utajiri wa imani na mapendo na hivi wanaweza kukaa tayari kwa kutazamia kufunuliwa kwa Bwana wetu Yesu Kristu. Huo ndio wito wa Majilio, kujiweka tayari kumsubiri Bwana atakayekuja.

Mwinjili Matayo anaweka wazi mbele yetu, fundisho la kuwa macho tukikesha ili Bwana ajapo atukute tu tayari. Anatumia mfano wa mtu mwenye nyumba yake, aliyesafiri na kuwaachia watumwa wake nyumba na kila mtu na wajibu yake. Anatarajia akirudi hata muda usiojulikana awakute watumwa hawa wakiwa macho wamefanya yote vema kama alivyowapangia. Kwako wewe mwana wa Mungu umekabidhiwa talanta ambazo unaalikwa kuziweka katika uzalishaji ili Bwana ajapo akukute unayo faida ndiyo kuwa macho na kukaa tayari. Kumbe kipindi cha majilio ni kipindi cha kuungama, kupatana na waliotukosea na kujiweka safi daima kwa virutubisho ndizo sakramenti na Neno la Mungu.

Ninakutakieni majilio njema iliyojaa heri na ustawi wa upendo, msamaha na huruma kwa wote ukilenga katika ujio wa Masiha. Tumsifu Yesu Kristo
Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.