2014-11-26 09:55:58

Mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu!


Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, linatangaza kwamba, tarehe 8 Februari 2015 itakuwa ni siku maalum ya kuhamasisha uelewa juu ya biashara haramu ya binadamu; siku ambayo Mama Kanisa anaadhimisha Siku kuu ya Mtakatifu Josephine Bakhita, kutoka Sudan aliyetekwa nyara na kupelekwa utumwani na baadaye kuokolewa na Wasamaria wema waliomwezesha kukumbatia imani ya Kikristo, leo hii ni mfano bora wa kuigwa.

Itakumbukwa kwamba, alitangazwa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo II kuwa Mtakatifu kunako mwaka 2000, Kanisa lilipokua linaadhimisha Jubilee kuu ya Miaka 2000 ya Ukristo.

Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum kwa kushirikiana na Shirikisho la Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, wataandaa Siku ya kupinga biashara haramu ya binadamu na kwa mara ya kwanza itaadhimishwa kwenye majimbo mbali mbali hapo tarehe 8 Februari 2015.

Itakumbukwa kwamba, biashara haramu ya binadamu ni kati ya mambo yanayodhalilisha utu na heshima ya binadamu katika karne ya ishirini na moja. Umoja wa Mataifa unabainisha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni ishirini na moja ambao wametumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo. Hili ni kundi linalotoka katika nchi maskini na kutokana na umaskini huu, watu wengi kwa kupewa ahadi za uwongo wanajikuta wakiwa wametumbukizwa kwenye biasha haramu ya binadamu na utumwa mamboleo.

Ni watu wanaochomolewa viungo vyao, ili kuuzwa kwenye soko la biashara haramu ya viungo vya binadamu, linaloendelea kukua na kuongezeka maradufu kila mwaka. Baadhi ya wasichana na watoto wanafanyishwa kazi za sulubu, kiasi kwamba, wanajuta kwanini wamekimbia kutoka nyumbani kwao kwa tamaa ya kupata nafuu ya maisha, lakini huko wanafanyishwa kazi kama Punda pasi na utu! Baadhi ya wasichana na wanawake wanajikuta wakilazimika kuingia kwenye ndoa za shuruti hata pasipokuwa na ridhaa yao.

Takwimu zinaonesha kwamba, kila mwaka zaidi ya watu millioni 2.5 wanatumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo, kati yao asilimia 60% ni wanawake na watoto. Hii ni biashara inayotunisha mifuko ya watu ambao dhamiri zao zimekufa, kwani inaingiza kwa mwaka kiasi cha dolla za Kimarekani billioni 32. Hii ni biashara ya tatu kimataifa inayopata faida kubwa sana, ikifuatiwa na biashara haramu ya dawa za kulevya na biashara ya silaha duniani.

Kanisa limekuwa mstari wa mbele kupambana na biashara haramu ya binadamu pamoja na kuwasaidia waathirika wa biashara hii kwa hali na mali. Kanisa kwa kutumia Mashirika ya kitawa na kazi za kitume, limeendelea kuwahabarisha na kuwahamasisha watu kufahamu njama zinazotumika katika biashara hii haramu na madhara yake kwa utu na heshima ya binadamu. Baba Mtakatifu Francisko, amelivalia njuga tatizo hili, kwani linakwenda kinyume kabisa cha utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kusimama kidete kulinda, kutetea na kudumisha haki msingi za binadamu, utu na heshima ya binadamu, kwa wahanga wote wa biashara haramu ya binadamu. Wahusika wanapaswa kutambuliwa na kukamatwa ili sheria iweze kuchukua mkondo wake, kwa kugeuza watu kuwa kama bidhaa inayoweza kuuzwa na kununuliwa kutoka madukani na kusahau kwamba, hawa ni binadamu, wana utu na heshima yao.

Siku ya kupambana na biashara haramu ya binadamu ni muhimu sana, wakati huu Mama Kanisa anaposherehekea Mwaka wa Watawa, kwani haya ndiyo “majembe” yaliyoko mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.