2014-11-26 08:31:41

Kanisa liko tayari kuanzisha mchakato wa majadiliano ili kuboresha mahusiano kati ya Serikali na Kanisa


Askofu mkuu Hubertus Matheus Maria Van Megen, Balozi wa Vatican nchini Eritrea, hivi karibuni alianza utume wake kwa kuwasilisha hati zake za utambulisho kwa viongozi wa Serikali ya Eritrea. Alipowasili nchini Eritrea, Askofu mkuu Van Megen amekaribishwa na viongozi wa Serikali na Kanisa.

Hati zake za utambulisho zilipokelewa na viongozi wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa nchini Eritrea. Viongozi hawa wamejadili kuhusu uhusiano wa kidiplomasia kati ya Vatican na Eritrea sanjari na mchango wa Kanisa katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Eritrea katika ujumla wao, hususan katika sekta ya elimu, afya na maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Huu ndio Uinjilishaji wa kina unaofanywa na Mama Kanisa, Barani Afrika na sehemu mbali mbali za dunia.

Rais Isaia Afwerki, amemkaribisha Askofu mkuu Van Megen nchini Eritrea, kwa kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko, Vatican na Kanisa katika ujumla wake kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; ustawi, maendeleo na mafao ya wengi; mambo msingi yanayojikita katika amani, utulivu na maelewano kati ya watu. Serikali ya Eritrea itaendelea kukuza na kudumisha utamaduni na mapokeo yake pamoja na kutoa fursa kwa waamini wa dini mbali mbali kuweza kukiri na kushuhudia imani yao katika hali ya usalama, kwa mafao ya wengi.

Askofu mkuu Hubertus Matheus Maria van Megen kwa upande wake, amewashukuru wananchi wa Eritrea kwa kuonesha upendo na mshikamano. Ametumia fursa hii, kuwasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko, kwa kusema kwamba, Kanisa liko tayari kuanzisha mchakato wa majadiliano, ili kuboresha uhusiano kati ya Serikali na Kanisa, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.

Askofu mkuu Megen pamoja na Familia ya Mungu nchini Eritrea waliweza kuunganisha kwa pamoja, ili kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Mtakatifu Daniel Comboni, mtume hodari kwa Kanisa Barani Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.