2014-11-25 14:34:14

Tarehe 10 Januari Vatican kufanya mkutano maalum kwa ajili ya Haiti!


Kardinali Robert Sarah, aliyekuwa Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum, kuanzia tarehe 25 hadi tarehe 29 Novemba 2014 yuko nchini Haiti, kutembelea Haiti ambayo miaka mitano iliyopita ilikumbwa na tetemeko la ardhi na kusababisha watu laki mbili na thelathini kufariki dunia na wengine zaidi ya millioni tatu kuathirika vibaya sana kutokana na tetemeko hili.

Lengo la safari hii ya kichungaji ni kuonesha mshikamano wa Kanisa na wananchi wa Haiti katika mchakato wa ujenzi wa Haiti mpya pamoja na kuzindua shule mpya iliyojengwa kwa msaada wa Kanisa mahalia kwa kushirikiana na Ubalozi wa Vatican nchini Haiti. Akiwa nchini Haiti, Kardinali Sarah anakutana na kuzungumza na viongozi wawakilishi wa Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki nchini Haiti, Caritas Haiti, ili kuangalia hali ya utoaji wa misaada ya Kanisa nchini Haiti. Itakuwa ni nafasi kwa Kardinali Sarah kukutana na kuzungumza na viongozi wa Serikali nchini Haiti.

Tarehe 28 Novemba, Kardinali Sarah atakutana na kuzungumza na Familia ya Mungu nchini Haiti; watu wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya kuwahudumia jirani zao walioathirika kwa tetemeko la ardhi, lililoikumba nchi hiyo, miaka mitano iliyopita. Wote hawa watafikishiwa salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko.

Kutokana na kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wananchi wa Haiti, Baba Mtakatifu Francisko ameonesha nia ya kuitisha mkutano utakaofanyika mjini Vatican hapo tarehe 10 Januari 2015, ili kuzungumzia matatizo na changamoto zilizopo katika ujenzi wa Haiti mpya baada ya kuharibiwa vibaya na tetemeko la ardhi. Mkutano huu utaandaliwa na Tume ya Amerika ya Kusini kwa kushirikiana na Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum pamoja na Maaskofu mahalia.







All the contents on this site are copyrighted ©.