2014-11-25 07:53:28

Siku ya Kimataifa ya kupambana na nyanyaso na dhuluma dhidi ya wanawake na wasichana duniani!


Dhuluma na nyanyaso za kijinsia dhidi ya wasichana na wanawake ni vitendo vinavyokwamisha juhudi za ujenzi wa usawa kati ya watu sehemu mbali mbali za dunia. Dhuluma na nyanyaso ni vitendo ambavyo havibagui wala kuchagua: rangi, mahali anapotoka mtu, cheo, hali yake ya kiuchumi, kijamii na kitamaduni.

Takwimu zinaonesha kwamba, kati ya wanawake watatu, kuna mwanamke mmoja ambaye amekwishawahi kunyanyaswa kijinsia, vitendo ambavyo vinafanyika ndani ya familia, katika maeneo ya kazi na kwenye mitandao ya kijamii.

Hii ni sehemu ya ujumbe Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa katika maadhimisho ya Siku ya Kupambana na Vitendo vya Unyanyasaji wa kijinsia kimataifa; siku inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 25 Novemba. Jumuiya ya Kimataifa inaadhimisha Siku hii, wakati kuna wasichana zaidi ya mia mbili waliotekwa nyara na kunyanyaswa kijinsia huko Nigeria.

Kuna ushahhidi wa kutosha kwamba, wanawake na wasichana nchini Iraq wanadhulumiwa utu na heshima yao kutokana na nyanyaso za kijinsia. Mambo si shwari huko India na Marekani kwani bado kuna vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinavyofanywa kwenye timu za michezo na kwenye maeneo ya vyuo vikuu. Kwa bahati mbaya wahusika wa vitendo hivi wanaendelea "kula kuku kwa mrija" bila ya kufikishwa kwenye mkondo wa sheria! Maadhimisho haya pamoja na mambo mengine yanapania kukomesha vitendo hivi na kuvunjilia mbali ukimya unnaoendelea kuhatarisha maisha ya wanawake na wasichana.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anabainisha kwamba, kila mtu anawajibu wa kuzuia pamoja na kupambana fika na vitendo vyote vinavyowanyanyasa na kuwadhulumu wanawake. Tabia ya kuendekeza mfumo dume imepitwa na wakati; wale wote wanaobainika kuhusika na vitendo hivi wafikishwe mbele ya sheria, ili kuunda na kujenga mazingira ya usawa katika maeneo ya kazi na majumbani, ili kuleta mabadiliko katika maisha ya wanawake na wasichana.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema, hivi karibuni amezindua kampeni inayopania kujenga na kuimarisha mshikamano, usawa, ili watu waweze kusaidiana, daima wakitafuta mafao ya wengi. Kila mtu atekeleze dhamana na wajibu wake, ili ubaguzi uweze kukomeshwa na wavunjaji wa sheria kufikishwa kwenye mkondo wa sheria pamoja na kuondokana na mila na desturi ambazo zimepitwa na wakati kwa kuendelea kuwanyanyasa na kuakandamiza wanawake na wasichana.







All the contents on this site are copyrighted ©.